Badilishano la Pekee la Kitia-Moyo
1 Hakuna siku inayopita bila watu wa Yehova kupambana na majaribu ya imani yao. Akijua kwamba ana kipindi kifupi tu cha wakati, Ibilisi anafanya shambulio la mwisho ili kuvunja uaminifu wetu kwa Yehova. (Ufu. 12:12) Ni jambo la maana sana ‘tuendelee kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezaji wa nguvu yake’ ili ‘tuweze kukinza katika siku ya uovu na, baada ya sisi kuwa tumefanya mambo yote kikamili, kusimama imara.’—Efe. 6:10, 13.
2 Kukusanyika pamoja na waamini wenzetu ni uandalizi kutoka kwa Yehova ili kutusaidia tujipatie nguvu. Mtume Paulo alifahamu umaana wa jambo hilo. Alikuwa na hamu nyingi ya kushirikiana na ndugu zake Wakristo ili “kuwa na badilishano la kitia-moyo” na ‘kufanywa imara.’ (Rom. 1:11, 12) Ili kututia nguvu katika kufanya mapenzi ya Mungu, Baraza Linaloongoza limepanga kwa upendo kututolea nafasi ya kufaidika na badilishano la kitia moyo kwenye Mkusanyiko wa Wilaya ujao, wenye kichwa “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme.”
3 Uwepo ili Ufaidike: Jiwekee mradi wa kuwako muda wa siku tatu zote. ‘Tunajifaidi’ kwa kufika kabla ya wimbo wa kwanza na kubaki mpaka tuseme “Ameni” ya kutoka moyoni baada ya sala ya kumalizia. (Isa. 48:17, 18) Wengi watahitaji kupanga programu yao ya kazi mapema vya kutosha ili wapate wakati wa kuhudhuria siku tatu zote. Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kufanya tajiri wako wa kazi akupe wakati wa mapumziko, lakini tuna uhakikisho wa Yehova kwamba atatusaidia kufanya mapenzi yake. (1 Yn. 5:14, 15) Ikiwa hatujachukua mipango kamili kwa ajili ya usafirishaji na mahali pa kupanga, huu ndio wakati wa kufanya hivyo; tusifikiri kwamba mambo yatajitokeza yenyewe. Tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kuhudhuria siku tatu zote.—Mez. 10:22.
4 Tazamia Kitia-Moyo: Je, umekwisha kutoka kwenye mkusanyiko wa wilaya ukisema: “Huu ulikuwa bora kupita yote!” Kwa nini yaelekea ulihisi hivyo? Ni kwa sababu, tukiwa wanadamu wasiokamilika, tunaweza kuchoka hatua kwa hatua, tukijikuta katika uhitaji wa kitia-moyo cha kiroho. (Isa. 40:30) Dada mmoja alieleza: “Mfumo huu unanichosha; mikusanyiko inanisaidia nikaze tena mtazamo wangu wa kiroho, ikinipa nguvu ya kiroho ninayohitaji. Inaonekana kana kwamba kitia-moyo kinakuja pa wakati ninapokihitaji zaidi.” Labda umekwisha kuhisi hivyo pia.
5 Tunapokea kitia-moyo kinachohitajiwa, si kupitia hotuba na mahojiano tu, lakini pia kupitia sehemu nyingine zenye kutajirisha za mikusanyiko yetu. Ndugu mmoja alieleza: “Ni yale matumizi yaliyo wazi na yenye kufaa ya kanuni za Biblia ndiyo ninayofurahia kwelikweli. Bila shaka, drama ni za thamani sana katika kuonyesha jinsi tunavyoweza kufaidika na mifano mizuri na mibaya ya wakati uliopita. Vichapo vipya vinavyotolewa ni kitu ninachokitazamia sikuzote, na ninavifurahia muda mrefu baada ya mkusanyiko.”
6 Mikusanyiko ni uandalizi wa maana sana kutoka kwa Yehova katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Inatusaidia kufuata shauri hili lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu: “Kaeni macho, simameni imara katika imani, endeleeni kama wanaume, kueni mwe wenye uweza.” (1 Kor. 16:13) Kwa hiyo, acheni tuazimie kuhudhuria kila kipindi cha mkusanyiko na kufurahia badilishano kubwa la kitia-moyo kwenye Mkusanyiko wetu wa Wilaya wenye kichwa “Watangazaji Wenye Bidii wa Ufalme”!
[Picture on page 3]
Panga Kuhudhuria
Siku Tatu Zote
[Picture on page 3]
■ Omba mapumziko kazini
■ Jiwekee mahali pa kupanga katika mji wa mkusanyiko
■ Panga jinsi ya kusafiri kwenda kwenye mkusanyiko