Je, Unaweza Kutoa Nyumba Yako?
1 Katika karne ya kwanza, Wakristo wengi walitoa nyumba zao ili zitumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (1 Kor. 16:19; Kol. 4:15; Flm. 1, 2) Katika makutaniko fulani leo, hakuna mahali pa kutosha pa kufanyia Funzo la Kitabu la Kutaniko na mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani. Kwa sababu hiyo, kunaweza kuwa na vikundi vya funzo la kitabu vinavyohudhuriwa na watu 30 au zaidi, hesabu inavyozidi ile inayopendekezwa ya watu karibu 15.
2 Pendeleo Zuri: Je, umefikiria kutoa nyumba yako ili itumiwe kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko? Chumba chenye ukubwa wa kutosha ambacho ni safi, chenye kuangazwa vizuri, na chenye kupitisha hewa safi ya kutosha ndicho kinachofaa kwa kusudi hilo. Kwa kuwa funzo la kitabu ni mkutano wa kutaniko na ni sehemu ya mpango wa Yehova wa kuelimisha watu wake, kuwa na funzo la kitabu nyumbani mwako ni pendeleo zuri. Wengi wanaripoti kwamba wamefaidika kiroho kwa kutoa nyumba yao katika njia hiyo.
3 Ikiwa unafikiri kwamba nyumba yako inafaa, kwa vyovyote julisha wazee kuhusu jambo hilo. Huenda ikawa wanatafuta mahali pa ziada. Ikiwa haiwezekani kufanyia funzo la kitabu nyumbani mwako, je, mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani inaweza kufanyiwa humo? Hata ikiwa hakuna uhitaji kwa sasa, wazee watafurahi kujua kwamba nyumba yako inaweza kutumiwa. Unaweza kufurahia pendeleo hilo wakati ujao.
4 Tuonyeshe Adabu Nzuri: Wanapokusanyika katika nyumba ya mtu binafsi, wahudhuriaji wote wanapaswa kuheshimu mali ya mwenye nyumba. Wazazi wanapaswa kuhakikisha kwamba watoto wao wanabaki mahali palipotayarishwa kwa ajili ya funzo na kwamba hawaendi katika sehemu za siri za nyumba. Tunapaswa pia kuonyesha kwamba tunafikiria majirani kwa kuwa waangalifu ili kuepuka kuwasumbua isivyofaa.—2 Kor. 6:3, 4; 1 Pet. 2:12.
5 Andiko la Waebrania 13:16 linatutia moyo tusisahau “kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana kwa dhabihu za namna hiyo Mungu hupendezwa vema.” Kutoa nyumba yako kwa ajili ya mkutano wa kutaniko ni njia bora ya kushiriki vitu vizuri na wengine na ‘kuheshimu Yehova kwa mali yako.’—Mez. 3:9.