Yehova Anastahili Kusifiwa Sana
Chakula cha Jioni cha Bwana Kitakachoadhimishwa Mnamo Aprili 16
1 Matarajio yanaongezeka tunapokaribia Aprili 16, 2003. Usiku huo tutakumbuka kifo cha Yesu, tukiungana na mamilioni ya waabudu wenzetu ulimwenguni pote ili kutukuza jina la Yehova. Yehova anastahili sifa yetu yote kwa sababu ya ule uandalizi bora wa ukombozi. Kupitia huo, atatoa baraka nzuri ajabu kwa wanadamu watiifu wote. Tunajiunga kwa moyo wote na mtunga-zaburi katika kupaza sauti: “BWANA ni mkubwa, na mwenye kusifiwa sana.”—Zab. 145:3.
2 Huu ni wakati wa kutafakari juu ya wema wa Mungu na deni ya shukrani tunayopaswa kumtolea Yehova kwa kutuma “Mwana wake mzaliwa-pekee kuingia katika ulimwengu ili tuweze kupata uhai kupitia kwake.” (1 Yn. 4:9, 10) Kuadhimisha kwa utii Chakula cha Jioni cha Bwana kunakazia katika mioyo yetu kwamba ‘Yehova ni mwenye neema na anajaa rehema; ni mwenye rehema nyingi.’ (Zab. 145:8) Kwa kweli, ukombozi ndilo onyesho kubwa zaidi la upendo wa Yehova kwa wanadamu wote. (Yn. 3:16) Tunapofikiri juu ya upendo wa Mungu na kutafakari juu ya mwenendo mwaminifu wa Yesu, tunachochewa kumsifu Yehova. Kwa umilele wote, tutamsifu yeye kwa sababu ya upendo usio na mipaka alioonyesha kwa kufanya uzima wa milele uwezekane kwetu.—Zab. 145:1, 2.
3 Saidieni Wengine Wamsifu Yehova: Shukrani kwa zawadi bora zaidi ya ukombozi aliyotoa Mungu zinatuchochea tualike wengine ili waungane nasi katika kumsifu Yehova. Mtunga-zaburi aliandika kwa uongozi wa Mungu: “Wao watasema ukumbusho wa wema wako mukubwa, na wataimba haki yako.” (Zab. 145:7) Mwaka uliopita peke yake, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walitumia zaidi ya saa bilioni moja katika kazi ya kuhubiri. Matokeo ya jitihada zao yalikuwa nini? Kila juma, wastani wa zaidi ya watu 5,100 walibatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova. Kukiwa na jumla ya watu 15,597,746 waliohudhuria Ukumbusho, kutia ndani zaidi ya watu milioni 9 ambao hawajaanza kumsifu Yehova wakiwa wahubiri wa habari njema, kuna uwezekano mkubwa wa kupata ongezeko zaidi! Tukiwa watangazaji wa Ufalme, tunathamini sana pendeleo letu la kutangaza habari njema na kuelekeza mioyo ya wengine kwa Yehova, kwa Mwana wake, na kwa Ufalme.
4 Njia nzuri ya kutia wengine moyo wamsifu Yehova ni kwa kuwaalika waungane nasi katika kuadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana. Je, umefanya orodha ya wale wote unaotaka kualika na pia wengine ambao labda wangehitaji kukumbushwa siku na saa? Je, umetoa kikaratasi cha mwaliko kwa wale wote wanaopatikana kwenye orodha yako? Ikiwa sivyo, fanya hivyo kwa bidii muda wa wakati unaobaki. Wasaidie waelewe kusudi la sherehe hiyo. Kwenye mwadhimisho, uwe tayari kuwasalimu wageni. Wafanye wajisikie kuwa wenye kukaribishwa, watambulishe kwa wengine, na uwapongeze kwa kuwapo.
5 Kuhudhuria Ukumbusho kunaweza kuchochea wapya wafanye maendeleo ya kiroho. Mwanafunzi mmoja wa Biblia anayesumbuliwa na mkazo wa akili uliotokea baada ya kupatwa na msiba, mkazo unaofanya iwe vigumu sana kwake kwenda mahali atakapozungukwa na watu wengi, alikuja kwenye Ukumbusho. Alipoulizwa alilowaza kuhusu mkutano huo, alisema: “Ulikuwa usiku mtakatifu sana, nami nilikuwapo.” Tangu wakati huo, ameanza kuhudhuria mikutano.
6 Baada ya Ukumbusho: Ni jambo gani linaloweza kufanywa ili kusaidia watu hao wanaopendezwa wawe wasifaji wa Yehova? Wazee watakuwa waangalifu kuhusu wapya wanaohudhuria Ukumbusho na kuchukua mipango ili wahubiri wenye kustahili wawatembelee muda kidogo baadaye ili kurudilia mambo yenye kuburudisha waliyojifunza na kuona. Wengine wanaweza kutamani kuwa na funzo la Biblia la nyumbani. Wanapaswa pia kualikwa wahudhurie mikutano yote ya kila juma, kwa kuwa kuhudhuria kwa ukawaida kunaweza kuongeza ujuzi wao wa Biblia.
7 Mipango inachukuliwa ili kutia moyo wale wote wasiohubiri kwa ukawaida na wale wasiotenda wahudhurie mikutano kwa ukawaida. Ikiwa unaombwa na wazee usaidie mtu fulani ambaye amekuwa asiyetenda aanze tena kushiriki katika utumishi wa shambani, uwe tayari kuitikia. Kuonyesha hivyo kwamba tunahangaikia kwa upendo ndugu na dada zetu kunapatana na himizo la mtume Paulo: “Maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Gal. 6:10.
8 Sisi sote na tufanye jitihada ya pekee ili kuwa kwenye Ukumbusho mnamo Aprili 16. Hatutapenda kukosa tukio hilo takatifu zaidi ili kumsifu Yehova. Ndiyo, acheni tumsifu Yehova kwa kazi zake kubwa sasa na milele!—Zab. 145:21.