Chakula cha Kiroho kwa Wakati Unaofaa
1 ‘Nami . . . nitaita nafaka na kuifanya iwe tele, nami sitaweka juu yenu njaa yoyote,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. (Ezek. 36:29) Maneno hayo ya kiunabii yanahusu watu wa Mungu leo. Kwa njia ya ufananisho, Yehova amefanya nafaka yenye kutegemeza uzima iote kwa wingi kwa ajili ya watu wake. Chakula cha kiroho kinachotolewa kwa wakati unaofaa kupitia mikusanyiko ya wilaya kinaonyesha wazi jambo hilo.
2 Kwenye mkusanyiko uliofanywa Columbus, Ohio, katika 1931, Yehova aliongoza waabudu wake wakubali kuitwa kwa jina jipya—Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Katika 1935 umati mkubwa wa Ufunuo 7:9-17 ulitambuliwa kwa usahihi. Katika 1942, Ndugu Knorr alitoa hotuba “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Hotuba hiyo ilichochea kufanya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote na kuongoza kwenye uundaji wa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Ijapokuwa mikusanyiko fulani ni ya kukumbukwa zaidi, kila mkusanyiko umeonekana kuwa meza yenye kujaa chakula cha kiroho chenye kutia nguvu kinachotolewa kwa wakati unaofaa.—Zab. 23:5; Mt. 24:45.
3 Je, Wewe Ni Mwenye Kula Vizuri Kabisa? Inawezekana kuwa na chakula kingi na bado kupatwa na ugonjwa unaotokana na kula vibaya ikiwa hatujitahidi kula. (Met. 26:15) Ni vilevile katika maana ya kiroho. Kwenye mikusanyiko fulani, wengi walionekana kuwa wanatembeatembea au kuzungumzazungumza na wengine wakati wa programu. Ijapokuwa ushirika unaojenga ni jambo la maana la mkusanyiko, wakati kwa ushirika huo ni kabla na baada ya kila sehemu ya mkusanyiko. (Mhu. 3:1, 7) Ikiwa sisi hatukae na kusikiliza kwa uangalifu, huenda tukakosa mambo ya maana. Waangalizi wa idara za Mkusanyiko na ndugu walio na migawo wanaweza mara kwa mara kuona kuwa jambo la lazima kuzungumzia mambo yanayohusu mkusanyiko wakati ambapo vipindi vya mkusanyiko ni vyenye kuendeshwa. Tofauti na hilo, wanapaswa kuonyesha mfano katika kusikiliza programu kwa uangalifu. Hakuna mmoja wetu anayepaswa kukosa sehemu yoyote ya chakula cha kiroho kinachotolewa—1 Kor. 10:12; Flp. 2:12.
4 Tunashangilia kama nini kuhusu kweli za kiroho ambazo Yehova anatoa kwa wingi, kweli zilizo tofauti na mafundisho makavu yasiyo ya kweli ya Jumuiya ya Wakristo! (Isa. 65:13, 14) Njia moja ambayo katika hiyo tunaweza ‘kujionyesha kuwa wenye shukrani’ ni kuona mkusanyiko kuwa nafasi ya kufundishwa na Yehova. (Kol. 3:15) Kazia fikira kwenye ujumbe wala si kwa ndugu aliye msemaji, na uone ujumbe kuwa unatoka kwa “Mfundishaji Mkuu.” (Isa. 30:20, 21; 54:13) Sikiliza kwa uangalifu. Andika kwa kifupi mambo makuu. Rudilia mambo makuu kila jioni. Tumia yale unayojifunza.
5 Kila mkusanyiko unaofanywa sasa kabla ya Har–Magedoni, iwe ni katika kambi ya wakimbizi, katika inchi iliyokumbwa na vita, au katika kikao kikubwa zaidi chenye hali ya amani, ni ushindi juu ya Shetani! Tukiwa muungano wa undugu, tunathamini pendeleo letu la kukusanyika pamoja kwenye mikusanyiko ya wilaya. (Ezek. 36:38) Tuna uhakika kwamba mara nyingine tena Yehova atatutolea kwa upendo ‘chakula kwa wakati unaofaa.’—Luka 12:42.
[Maulizo ya Funzo]
1. Andiko la Ezekieli 36:29 ni lenye kutimizwaje leo?
2. Yehova ametumiaje mikusanyiko ya wilaya ili kugawa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa?
3. Tunapaswa kufanya nini ili kufaidika na karamu ya kiroho kwenye mkusanyiko wa wilaya?
4. Tunawezaje kuonyesha shukrani kwa ajili ya chakula kingi cha kiroho ambacho Yehova anatutolea?
5. Mikusanyiko ya wilaya inatutolea sababu gani za kushangilia?
[Kisanduku Kwenye Ukurasa wa 4]
Onyesha Uthamini kwa Ajili ya Meza ya Yehova
◼ Sikiliza kwa uangalifu
◼ Andika mambo makuu
◼ Rudilia mambo makuu ya programu kila jioni
◼ Tumia yale unayojifunza