Fanya Matumizi Mazuri ya Biblia
1 Kuhusu kichapo chochote kile tunachopanga kutolea watu katika huduma, ni jambo lenye faida kuchagua andiko moja lenye kuchochea kufikiri na kulisomea wale watakaosikiliza. (Ebr. 4:12) Kuchagua andiko linalotumiwa katika kichapo unachotolea watu kutasaidia ili upate maneno unayoweza kutumia kwa matokeo wakati wa kutolea kitabu. Katika maeneo fulani, wahubiri wameona kuwa ni jambo lenye faida kuchukua Biblia mkononi wanapokaribia mtu au wanapohubiri nyumba kwa nyumba.
2 Anza Mazungumzo kwa Andiko: Wahubiri fulani wanaanza utoaji wao wakiuliza mwenye nyumba ulizo rahisi la maoni kuhusu andiko la Biblia na mara moja wanalisoma. Kufanya hivyo kunaelekeza uangalifu wa mtu moja kwa moja kwenye Neno la Mungu. Je, utoaji mbalimbali ufuatao utakuwa na matokeo katika eneo lenu?
◼ “Ungelikuwa na uwezo, je, wewe ungelileta mabadiliko haya?” Soma Ufunuo 21:4.
◼ “Kwa nini tunaishi katika nyakati za hatari?” Soma 2 Timotheo 3:1-5.
◼ “Je, unafikiri kwamba maisha yetu yangekuwa bora ikiwa kila mmoja angefuata shauri hili?” Soma Mathayo 7:12.
◼ “Je, unafikiri kwamba watoto wako wataweza kufurahia hali zinazozungumziwa hapa?” Soma Zaburi 37:10,11.
◼ “Je, unafikiri kwamba siku fulani maneno haya yatatimia?” Soma Isaya 33:24.
◼ “Je, unajua badiliko litakalofanywa na serikali inayozungumziwa hapa?” Soma Danieli 2:44.
◼ “Je, ungetaka kumwuliza Mungu ulizo hili?” Soma Yobu 21:7.
◼ “Je, inawezekana kuona tena wapendwa wetu waliokufa?” Soma Yohana 5:28, 29.
◼ “Je, wafu wanajua yale walio hai wanayofanya?” Soma Mhubiri 9:5.
3 Fafanua, Toa Mfano, Onyesha Jinsi ya Kutumia Andiko: Mtu anapokuwa tayari kuzungumza, usiende haraka haraka na mazungumzo. Chukua wakati wa kufafanua, kutoa mfano, na kuonyesha jinsi ya kutumia andiko unalosoma ili kwamba mtu alielewe. (Neh. 8:8) Watu wanapoelewa na kukubali yale Neno la Mungu linafundisha, hilo linaweza kutokeza mabadiliko ya ajabu katika maisha yao.—1 The. 2:13.
4 Endelea kufanya matumizi mazuri ya Biblia kadiri unavyoamsha kupendezwa. Unaweza kutumia ufundi huohuo unapofanya ziara za kurudia: (1) Chagua andiko linalofaa. (2) Tokeza ulizo la maoni lililo rahisi kuhusu andiko. Kisha usome andiko. (3) Fafanua, toa mfano, na uonyeshe jinsi ya kulitumia. Jitahidi kuongeza jambo fulani kwenye ujuzi wa Neno la Mungu ambao mtu anao kila wakati unapomtembelea. Kwa kufanya hivyo, hivi karibuni unaweza kuongoza funzo la Biblia!
[Maulizo ya Funzo]
1. Unaweza kufanya nini katika kujitarisha kwa ajili ya huduma ya shambani?
2. (a) Namna gani tunaweza kuanza mazungumzo yetu kwa andiko? (b) Ni habari gani za Kimaandiko zinazopendeza watu katika eneo lenu?
3. Namna gani tunaweza kusaidia watu waelewe maandiko ya Biblia tunayosoma?
4. Namna gani tunaweza kufanya matumizi mazuri ya Biblia kwenye ziara za kurudia?