Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 4: Kuzoeza Wanafunzi Kutayarisha Funzo
1 Mwanafunzi anayesoma kimbele somo litakalochunguzwa, anayepiga kistari chini ya majibu, na anayefikiri jinsi ya kujibu katika maneno yake mwenyewe atafanya maendeleo ya kiroho kwa haraka. Kwa hiyo, mara tu funzo la kawaida litakapokuwa limeanzishwa, tayarisha somo pamoja na mwanafunzi ili kumwonyesha jinsi ya kutayarisha. Kuhusu wanafunzi wengi, litakuwa jambo lenye kusaidia kutayarisha sura au somo nzima pamoja.
2 Kupiga Kistari Chini ya Majibu na Kuandika Maelezo Pembeni: Umuelezee jinsi ya kupata majibu moja kwa moja ya maulizo yenye kuchapishwa. Onyesha mwanafunzi kichapo chako cha funzo ambamo umepiga kistari chini ya maneno makuu au misemwa. Mnapochunguza habari, anaweza kutaka afuate mfano wako, kwa kutia kistari katika nakala yake, maneno yanayohitajiwa tu, yanayoweza kumsaidia akumbuke jibu. (Luka 6:40) Kisha umwombe ajibu katika maneno yake mwenyewe. Hilo litakusaidia kuona jinsi anavyoelewa vizuri habari mnayojifunza.
3 Kuchunguza kwa uangalifu maandiko ambayo hayatajwi moja kwa moja ni sehemu nyingine ya maana itakayomsaidia mwanafunzi kujitayarisha kwa ajili ya funzo. (Mdo. 17:11) Umsaidie aone kwamba kila andiko linaloonyeshwa na ambalo halitajwi moja kwa moja linategemeza jambo fulani katika fungu. Mwonyeshe jinsi ya kuandika maelezo kwa kifupi pembeni katika kichapo chake cha funzo. Kazia jambo la kwamba mambo yote anayojifunza yanategemezwa na Biblia. Wakati wa funzo, mtie moyo atumie sana katika maelezo yake, maandiko yanayotajwa.
4 Mwono wa Jumla na Kurudilia: Kabla ya mwanafunzi kuanza kutayarisha habari ya funzo kwa undani, litakuwa jambo lenye kusaidia kwake kuwa na mwono wa jumla wa habari. Onyesha kwamba anaweza kupata mwono wa jumla wa habari kwa kuchunguza kwa kifupi kichwa cha sura, vichwa vidogo, na picha. Mwonyeshe kwamba kabla ya kumaliza sehemu yake ya kutayarisha, lingekuwa jambo lenye hekima kwake kuchukua wakati mdogo ili kurudilia mambo makuu yanayoonyeshwa katika somo, akitumia kisanduku cha kujikumbusha ikiwa kinatolewa. Namna hiyo ya kurudilia itamsaidia kuchunga habari.
5 Kuzoeza mwanafunzi kutayarisha vizuri funzo lake kutamsaidia atoe maelezo yenye kufaa kwenye mikutano ya kutaniko. Kutamsaidia pia kukuza mazoezi ya kujifunza yatakayomfaidi muda mrefu baada ya kukamilisha funzo la Biblia pamoja naye.