Kisanduku Cha Maulizo
◼ Ni njia gani iliyo bora zaidi ambayo katika hiyo tunaweza kutoa michango ya kifedha kwa faida ya akina ndugu wenye uhitaji katika nchi nyingine?
Nyakati nyingine, tunapata habari kuhusu akina ndugu walio katika nchi nyingine ambao wana uhitaji wa vitu vya kimwili kwa sababu ya mateso, msiba, au hali zingine ngumu. Ndugu fulani wamejisikia kuchochewa ili kutuma fedha moja kwa moja kwenye ofisi za tawi katika nchi hizo. Wakiomba kwamba fedha hizo zitumiwe ili kusaidia mtu fulani, kutaniko fulani, au mpango wa ujenzi fulani uliotajwa.—2 Kor. 8:1-4.
Ingawa hangaiko lenye upendo kama hilo kwa waamini wenzetu linastahili pongezi, mara nyingi kuna mahitaji ya haraka zaidi kuliko yale yaliyo akilini mwa mtoaji wa mchango. Katika hali fulani, uhitaji ambao umetajwa na mtoaji wa mchango huenda tayari umekwisha kutoshelezwa. Bila shaka, tunaweza kuwa hakika kwamba michango inapotumwa kwenye ofisi ya tawi kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, Hazina ya Majumba ya Ufalme, au msaada wa kitulizo baada ya msiba, zile fedha zinazotolewa zitatumiwa kama vile mtoaji wa mchango alivyokusudia.
Ndugu katika matawi yote wamezoezwa kikamili ili kushughulikia kwa haraka mahitaji yasiyotazamiwa. Katika hali zote hizo, ofisi ya tawi inajulisha Baraza Linaloongoza kuhusu jambo hilo. Ikiwa kuna uhitaji wa msaada zaidi, Baraza Linaloongoza linaweza kuomba matawi ya kandokando ili yasaidie, au fedha zinaweza kutumwa moja kwa moja kutoka makao makuu.—2 Kor. 8:14, 15.
Kwa hiyo, michango yote inayotolewa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, mipango ya ujenzi katika nchi nyingine, au msaada wa kitulizo baada ya msiba, inapaswa kutumwa kwenye ofisi ya tawi katika nchi ambamo mnaishi, ama kupitia kutaniko au moja kwa moja. Katika njia hii, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” kupitia mipango ya kitengenezo iliyowekwa na Baraza Linaloongoza, anashughulikia mahitaji ya ndugu ulimwenguni pote kwa namna yenye utaratibu.—Mt. 24:45-47; 1 Kor. 14:33, 40.