Programu ya Familia—Utumishi wa Shambani Pamoja na Familia
1 Yehova anapendezwa kuona watoto wakisifu jina lake. (Zab. 148:12, 13) Katika siku za Yesu hata ‘watoto na wanaonyonya walitoa sifa’ kwa Mungu. (Mt. 21:15, 16) Jambo hilohilo linatukia leo. Wazazi, mnawezaje kusaidia watoto wenu wakomae katika kuwa wasifaji wa Yehova wenye bidii katika huduma ya Kikristo? Tena, kama inavyokaziwa katika makala hapo juu kuhusu mikutano ya kutaniko, jambo la maana ni mfano wenu. Baba mmoja alionyesha mawazo ya wazazi wengi zaidi akisema: “Watoto wanafuata mfano wako wala si maneno yako!”
2 Dada mmoja aliyelelewa na wazazi wanaomwogopa Mungu anakumbuka: “Hatukuamka kamwe Jumamosi (Siku ya Posho) asubuhi tukiuliza ikiwa tungeenda kwenye huduma. Tulijua kwamba tungeenda.” Vivyohivyo, mnaweza kuingiza akilini mwa watoto wenu umaana wa kazi ya kuhubiri kwa kuweka kawaida ya kila juma na yenye upatano ili kushiriki katika utumishi wa shambani mkiwa familia. Jambo hilo haliruhusu tu watoto wenu kujifunza mambo kwa kuwatazama nyinyi, lakini linawawezesha nyinyi pia kuchunguza mtazamo wao, tabia yao, na ufundi wanaositawisha.
3 Kuzoezwa Hatua kwa Hatua: Ili watoto wafurahie huduma, wanahitaji kutayarishwa ili washiriki kwa matokeo. Dada tuliyemtaja hapo juu alisema pia: “Hatukuwa wafuasi tu walioandamana na wazazi wetu katika kazi yao. Tulijua tulikuwa na sehemu, hata ikiwa ilikuwa kupiga kengele tu mlangoni na kuacha kikaratasi cha kukaribisha watu. Kupitia matayarisho yenye uangalifu kabla ya utendaji wa kila mwisho-juma tulijua lile ambalo tungesema.” Mnaweza kuzoeza watoto wenu kwa kuchukua dakika chache kila juma ili kuwatayarisha kwa ajili ya huduma, hilo linaweza kufanyika wakati wa funzo la familia au wakati mwingine.
4 Kuhubiri pamoja mkiwa familia kunawatolea nafasi zaidi ya kukazia kweli katika watoto wenu. Baba mmoja Mkrito alienda pamoja na binti wake alipotembea kilometa 10 kwenda na kilometa 10 kurudi ili kugawanya trakti za Biblia kwa wana-kijiji katika bonde la karibu. Dada huyo alikumbuka kwa shauku: “Baba yangu aliikaza kweli kikiki moyoni mwangu, katika matembezi hayo.” (Kum. 6:7) Nanyi pia na mbarikiwe kwa kufanya utumishi wa shambani kuwa sehemu ya programu yenu ya familia ya kila juma.