Onyesha Kupendezwa Kibinafsi na Wengine—Kwa Kuwa Mtazamaji Mzuri
1 Yehova Mungu na Kristo Yesu hawalinganishwi na yeyote katika kutambua mahitaji kamili ya watu na kuwatolea msaada. (2 Nya. 16:9; Marko 6:34) Tunapotambua mambo yanayopendeza na yale yanayohangaisha wale tunaokutana nao katika huduma yetu, tunaweza kufanya utoaji wetu wa habari njema upatane na hali yao.
2 Uwe Mwangalifu Kuhusu Mambo Madogo-Madogo: Yesu alikuwa mtazamaji mzuri. (Marko 12:41-43; Luka 19:1-6) Vivyo hivyo, tunapokaribia mlango wa mtu na kuona mapambo ya kidini, maandishi kwenye magari, au vitu vya watoto vya kuchezea katika uwanja, jambo hilo linaweza kututolea nafasi za kutoa ushahidi wenye matokeo wa habari njema.
3 Hali ya uso wa mtu na mwenendo wake vinaweza kuonyesha jambo fulani kuhusu hisia zake. (Met. 15:13) Labda kupoteza mpendwa au hali nyingine yenye kutaabisha imemwacha katika uhitaji wa kufarijiwa. Huenda akathamini jambo la kushiriki maandiko fulani yanayolingana na hali yake. (Met. 16:24) Je, mwenye nyumba ni mwenye kuwa katika uharaka wa kuondoka au ni mwenye kubeba mtoto mchanga anayelia? Ikiwa ndivyo, huenda ikawa vizuri kupangia kumtembelea wakati mwingine. Kwa kufikiria wengine na ‘kuonyesha hisia-mwenzi,’ tunaweza kuchochea mtu asikilize tunaporudi.—1 Pet. 3:8.
4 Fanya Maelezo Yako Yapatane na Hali: Mtume Paulo alitazama na kuona kwamba jiji la Athene lilikuwa na madhabahu iliyotolewa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” Hilo lilikuwa na uvutano juu ya namna alivyotoa habari njema, kwa kuwa alisema: “Kile mnachokipa ujitoaji-kimungu bila kujua, hicho ninawatangazia ninyi.” Utangulizi wa Paulo wenye busara ulichochea wengine kati ya wale waliokuwa hapo kufikiria ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.—Mdo. 17:23, 34.
5 Kwa njia kama hiyo, kuwa watazamaji wazuri kunatusaidia kutambua mambo yanayompendeza mtu na hivyo kunatuwezesha kupatanisha utangulizi wetu na hali. Tumia maulizo yanayoweza kufanya mwenye nyumba atoe mawazo yake. Fikiri juu ya maandiko yanayoweza kutumiwa ili kuongeza kupendezwa kwake. (Met. 20:5) Tukiwa watazamaji wazuri na kuonyesha kwamba tunapendezwa kibinafsi kwa unyoofu na wengine, hilo litatusaidia kushiriki habari njema kwa ufundi.