Fanya Matumizi Yenye Hekima ya Vichapo Vyetu Vyenye Kutegemea Biblia
1 “Nimekuwa nikisoma vichapo vyenu tangu 1965. Ninachunguza Biblia ninapovisoma, na kila jambo katika vichapo vyenu linapatana na Biblia. Nimetaka sikuzote kujua ukweli halisi kuhusu Mungu na Yesu, na ninaweza kusema kwa unyoofu kwamba ninapata majibu ya kweli kupitia vichapo vyenu na Biblia.” Hayo ndiyo maneno ambayo mtu mmoja aliandikia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova. Kupitia barua hiyohiyo, yeye aliomba funzo la Biblia.
2 Kama mtu huyo mwenye uthamini, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanathamini vichapo vinavyosaidia kujifunza Biblia vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Kila mwaka, kiasi kikubwa sana cha vichapo kinatokezwa ili kusaidia watu wanyoofu “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Tunawezaje kufanya matumizi yenye hekima ya vichapo vyetu vyenye kutegemea Biblia?
3 Epuka Uharibifu: Kwa kipindi fulani cha wakati, huenda tulirundika vichapo zaidi kupita kiasi ambacho tutatumia kwa hakika. Tunaweza kufanya nini ili kuepuka kuharibu vichapo vyetu vyenye thamani? Utambuzi unahitajiwa tunapochukua vichapo vya kutumia katika huduma. Badala ya kuchukua nakala nyingi za kichapo ambacho tutakuwa tukitolea watu, tunaweza kuchukua tu nakala moja au mbili na baada ya kuzitolea watu kurudi ili kuchukua nyingine zaidi. Hilo litatuzuia kujirundikia katika nyumba zetu vichapo vingi kupita kiasi. Vivyo hivyo, ikiwa tuna kiasi kikubwa cha magazeti ambayo hatutolei watu, lingekuwa jambo lenye kufaa kupunguza kiasi tunachoomba.
4 Vichapo Vyenye Kupita Kiasi Katika Stoki: Ikiwa kutaniko lina vichapo fulani kupita kiasi katika stoki, msimamizi wa vichapo anaweza kutaka kuchunguza jambo hilo pamoja na makutaniko mengine ya karibuni ili kuona ikiwa yanaweza kutumia vichapo vya ziada. Wahubiri wanaweza kutolea washiriki wa familia wasioamini, wanafunzi wa Biblia, na wengine, vichapo vya zamani. Labda wale walio wapya katika kushirikiana na kutaniko watapenda kupata vichapo hivyo vya zamani kwa ajili ya maktaba ya kitheokrasi yao binafsi.
5 Tunataka vichapo vyetu vitimize kusudi lavyo, yaani, kusaidia watu wanyoofu kujifunza zaidi kuhusu makusudi ya ajabu ya Yehova. Kama vile Yesu hakuharibu chakula kilichobaki baada ya kulisha kimuujiza umati, mradi wetu unapaswa kuwa kutumia vizuri zaidi vichapo vyenye kutegemea Biblia tunavyotolewa. (Yoh. 6:11-13) Ujumbe wenye kuokoa uzima ulio katika vichapo vyetu hauwezi kufikia mioyo ya watu wenye mwelekeo wa uadilifu ikiwa unakaa kwenye makabati yetu au katika mifuko ya vitabu. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa wenye usawaziko tunapochukua vichapo kwa ajili ya huduma na kuvifanyia matumizi ya hekima ili kufaidi wengine.—Flp. 4:5.
[Maulizo ya Funzo]
1, 2. Watu wengi wana maoni gani kuhusu vichapo vyetu, na hilo linatokeza ulizo gani?
3. Tunawezaje kuepuka kuharibu vichapo?
4. Ni nini kinachoweza kufanywa ikiwa kutaniko lina vichapo vya kupita kiasi katika stoki?
5. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini vichapo vyetu?