Furahia Funzo Letu la Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
1 Kutolewa kwa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kwenye Mikusanyiko ya Wilaya “Utii wa Kimungu” lilikuwa jambo lenye kusisimua. Karibuni tutakitumia sana kitabu hicho katika huduma yetu ya shambani, hasa tunapoongoza mafunzo ya Biblia. Kwa hiyo, tunahitaji kujua vizuri kichapo hicho kipya. Jambo hilo litawezekana kwa sababu tutakuwa tukijifunza kitabu hicho kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko kuanzia juma toka Aprili 17, 2006.
2 Mwangalizi wa Funzo la Kitabu atavutia uangalifu wa wahudhuriaji kwenye maulizo yanayopatikana mwanzoni mwa kila sura. Kisha funzo litaongozwa kwa kutumia maulizo yaliyo chini ya ukurasa. Maandiko ya msingi (au yanayokazia mambo makuu) yatasomwa na kuzungumziwa, na kisanduku “Mambo Ambayo Biblia Inafundisha” kilicho kwenye mwisho wa kila sura kitasaidia kurudilia habari, kwa sababu kisanduku hicho kina majibu ya Kimaandiko kwa maulizo yanayopatikana mwanzoni mwa sura. Utafurahia kutoa maelezo, kwa kuwa kitabu hicho kinaeleza habari katika njia iliyo wazi, rahisi, na yenye kupendeza.
3 Nyongeza ya kitabu hicho inatoa maelezo ya habari mbalimbali. Wanafunzi wa Biblia wanapohitaji maelezo zaidi kuhusu vichwa fulani vya habari, tutakuwa tayari kutumia mambo hayo yaliyo katika Nyongeza. Nyakati fulanifulani sehemu za Nyongeza hiyo zitazungumziwa katika Funzo la Kitabu la Kutaniko. Mambo yote yaliyo katika Nyongeza kuhusiana na kichwa fulani cha habari kinachochunguzwa yatasomwa na msomaji wa funzo la kitabu, na makala zilizo ndefu zinaweza kugawanywa kwa sehemu. Maulizo hayatolewi katika Nyongeza. Lakini mwangalizi anaweza kufanya wasikilizaji watoe maelezo kutokana na habari hizo kwa kutokeza maulizo yanayokazia mambo makuu.
4 Kitabu Biblia Inafundisha kitaongozwa kwa haraka kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Lakini hatutafuata hatua hiyo tutakapojifunza kitabu hicho na watu wengine, hasa ikiwa wana ujuzi kidogo au hawana ujuzi wa Biblia. (Mdo. 26:28, 29) Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tutahitaji kuzungumzia maandiko kwa kirefu, kufasiria vielelezo, na kadhalika. Basi fanya iwe mradi wako kuhudhuria kila juma na kushiriki kikamili funzo letu la kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?