Fuata Mfano wa Mwalimu Mkuu Unapotumia Kitabu Biblia Inafundisha
1 Mwalimu Mkuu, Yesu alifasiria kila mara mambo kwa njia nyepesi na iliyo wazi. Nyakati nyingine, ili kufanya wasikilizaji wake wafikiri, aliwaomba waeleze kwanza maoni yao. (Mt. 17:24-27) Alielekeza uangalifu wa watu kwenye Neno la Mungu. (Mt. 26:31; Marko 7:6) Alikuwa mwangalifu ili asiwatolee wanafunzi wake habari nyingi sana, akijua kwamba walipaswa kuendelea kujifunza. (Yoh. 16:12) Pia, Yesu alipenda kujua ikiwa wanafunzi wake waliamini na kuelewa mambo aliyowafundisha. (Mt. 13:51) Kitabu Biblia Inafundisha kimefanywa ili kutusaidia tufundishe kama Yesu.
2 Maulizo ya Utangulizi: Mnapoanza kujifunza sura fulani, ni vizuri kuelekeza uangalifu wa mwanafunzi kwenye maulizo ya utangulizi yaliyo chini ya kichwa kikuu. Ili kuamsha kupendezwa kwa mwanafunzi, uliza maulizo kwa namna ambayo haitamlazimisha mwanafunzi kutoa jibu. Au unaweza kumwomba atoe maelezo mafupi kwa maulizo hayo. Si lazima kutoa maelezo mengi kuhusu majibu yake au kusahihisha kila jibu lisilofaa. Unaweza tu kumshukuru kwa mawazo yake na kuanza kuchunguza habari. Maelezo yake kuhusu maulizo ya utangulizi yatakusaidia kujua ikiwa unahitaji kutoa uangalifu mwingi kwenye sehemu fulani za sura.
3 Maandiko: Funzo linapaswa kutegemea Maandiko. (Ebr. 4:12) Hata hivyo, si jambo la lazima kusoma kila andiko linalotajwa. Kazia yale Maandiko yenye kutegemeza mambo tunayoamini. Labda si lazima kusoma Maandiko yanayotoa habari zaidi kuhusu mambo munayozungumzia. Kitabu Biblia Inafundisha kinafundisha kweli kwa namna iliyo nyepesi kuelewa. Fanya funzo liwe nyepesi. Kazia mambo makuu, na epuka kuzungumzia sana maelezo zaidi au kuleta isivyohitajiwa habari zisizohusiana na mazungumzo.
4 Nyongeza: Nyongeza ina vichwa 14 ambavyo vinaongezea habari kwenye vichwa vikuu. Hamulazimishwi kuzungumzia mambo hayo wakati wa funzo. Kuhusu habari fulani, unaweza kutia mwanafunzi moyo asome yeye peke yake habari hizo zingine, hasa ikiwa anaelewa na kukubali habari mnayojifunza. Kwa mfano, ikiwa mwanafunzi amekwisha kuamini tayari kwamba Yesu ni Masihi, halitakuwa jambo la lazima kuchunguza pamoja naye nyongeza inayozungumzia habari “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa,” mnapozungumzia sura ya 4, “Yesu Kristo Ni Nani?” Wakati mwingine, linaweza kuwa jambo lenye faida kuchukua wakati mnapojifunza ili kuzungumzia habari katika nyongeza au sehemu tu ya nyongeza hiyo.
5 Ikiwa unaamua kuzungumzia habari katika nyongeza, unaweza kutayarisha maulizo mbele ya wakati na kuchunguza mafungu na mwanafunzi kama tu mnavyofanya mnapojifunza habari kuu. Au kulingana na mahitaji ya mwanafunzi, unaweza kuamua ikiwa utachukua dakika chache wakati wa funzo ili kurudilia habari katika nyongeza pamoja naye. Jambo hilo litakusaidia kuwa hakika kwamba anaelewa habari ambayo alisoma yeye mwenyewe.
6 Kisanduku cha Kujikumbusha: Kisanduku mwishoni mwa kila sura kinatoa majibu ambayo mara nyingi yanajibu maulizo ya utangulizi. Unaweza kutumia majibu hayo ili kurudilia mawazo makuu ya sura. Wahubiri fulani wameona kuwa ni jambo lenye kusaidia kusoma pamoja na mwanafunzi kila jibu na labda maandiko yanayounga mkono majibu hayo. Kwa hiyo, wanaomba mwanafunzi aeleze kwa kifupi jinsi maandiko hayo yanaunga mkono majibu hayo. Hilo linasaidia mwalimu kujua ikiwa mwanafunzi anaelewa waziwazi mambo makuu ya sura na jinsi mambo hayo yanategemezwa na Biblia na ikiwa anayakubali. Hilo linazoeza pia mwanafunzi kutumia Biblia ili kufasiria wengine kweli.
7 Njia moja yenye matokeo zaidi ili kutimiza kazi yetu ya kufundisha watu na kufanya wanafunzi ni kufuata ufundi mbalimbali wa Yesu wa kufundisha. (Mt. 28:19, 20) Kitabu Biblia Inafundisha kinaweza kutusaidia kufanya hivyo. Tumia vizuri kitabu hicho ili kufundisha wengine kweli kwa namna iliyo nyepesi, wazi, na yenye kupendeza.
[Maulizo ya Funzo]
1. Namna gani Yesu alifundisha?
2. Namna gani tunaweza kutumia maulizo ya utangulizi ya kila sura?
3. Namna gani tunaweza kufanya funzo liwe nyepesi?
4. Ni jambo gani litakalokusaidia kujua ikiwa utachukua wakati ili kuchunguza habari katika nyongeza, wakati mnapojifunza?
5. Ikiwa tunaamua kuchunguza habari katika nyongeza, namna gani tunaweza kufanya hivyo?
6. Namna gani kisanduku cha kujikumbusha kinaweza kutumiwa mwishoni mwa kila funzo?
7. Namna gani tunaweza kutumia kitabu Biblia Inafundisha ili kutimiza kazi yetu?