Kuwa Wenye Ujasiri, Lakini Wenye Kufanya Amani
1 Watu wengi ambao tunahubiria wanaeleza mambo wanayoamini kabisa, ambayo yanapingana na kweli ya Biblia. Ijapokuwa tunapaswa kuhubiri kwa ujasiri (uhodari), tunataka pia “kufanya amani na watu wote” na kuepuka kuwachukiza bila sababu. (Rom. 12:18; Mdo. 4:29) Namna gani tunaweza kuwa wenye ujasiri (uhodari) lakini wenye kufanya amani tunapohubiri habari ya Ufalme?
2 Tafuta Mambo Ambayo Munakubaliana: Mtu mwenye kufanya amani anaepuka ubishi. Kupinga waziwazi mambo ambayo msikilizaji anaamini kabisa kutamfanya asitusikilize. Ikiwa anasema jambo fulani lisilo la kweli, labda tunaweza kutumia ufundi na hivyo kuzungumzia wazo lingine ambalo labda tunakubaliana. Kwa kukazia mambo ambayo sisi na yeye tunaamini, tunaweza kuondoa katika msikilizaji mawazo yoyote yasiyofaa na kufanya hivyo habari tunayomtolea ivutie moyo wake.
3 Ikiwa tunaachilia wazo lisilo la kweli la msikilizaji wetu, je, ni kusema kwamba tunakubaliana na wazo hilo au kupunguza uzito wa ukweli? Hapana. Mgawo wetu tukiwa wahudumu wa Kikristo si kupinga kila wazo la uongo ambalo mtu anatokeza, lakini ni kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Kuliko kupinga kila wakati kwa sababu msikilizaji anatoa wazo lisilo la kweli, tunaweza kutumia nafasi hiyo ili kukuza ufundi wa kutambua mawazo ya mtu.—Met. 16:23.
4 Heshimu Msikilizaji Wako: Kuna nyakati ambazo tunapaswa kuwa hodari na wenye bidii tunapopinga mafundisho ya uongo. Hata hivyo, tukiwa watu wenye kufanya amani, tunajizuia kuzihaki na kutumia maneno ya kuzarau wale wenye kuamini na kufundisha mambo yenye makosa. Kujionyesha kuwa sisi tunajua mengi kushinda wengine kutawafanya watu wasitupokee, lakini kuonyesha unyenyekevu na wema tunapozungumza na watu kutawafanya wale wanaopenda ukweli watusikilize. Kuheshimu wasikilizaji wetu na mambo wanayoamini kutawafanya wajisikie kuwa watu wa lazima na hilo litawafanya wakubali kwa vyepesi habari tunayowatolea.
5 Mtume Paulo alifikiria kwa uangalifu mambo ambayo wasikilizaji wake waliamini na kuwatolea habari njema kwa namna ambayo ingevutia mioyo yao. (Mdo. 17:22-31) Alikubali kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote” ili ‘kwa vyovyote, awaokoe wengine.’ (1 Kor. 9:22) Tunaweza kufanya vivyo hivyo kwa kuwa watu wenye kufanya amani tunapohubiri habari njema kwa uhodari.