Kisanduku Cha Maulizo
◼ Kuna hatari gani za kutumia Internete ili kupashana habari na mtu fulani tusiyemjua?
Vituo vingi vya Internete vimefanywa ili kusaidia watu wakutane na wapashane habari na watu wengine. Kati ya vituo hivyo, vingi vinafanya iwezekane watu waingize na kutangaza maelezo mafupi kuwahusu, maelezo hayo yanaweza kutia ndani picha na habari zingine za kipekee. Watu wanapoona maelezo kumhusu mtu fulani, wanaweza hivyo kuanzisha mazungumzo na mtu huyo. Vituo kama hivyo vinatumiwa sana na vijana, na vijana fulani katika kutaniko wamevitumia ili kuanzisha mazungumzo na wengine wanaojiita kuwa Mashahidi wa Yehova.
Ni vyepesi sana mtu unayepashana naye habari kupitia Internete akudanganye kuhusu jinsi alivyo, kuhusu hali yake ya kiroho, au kuhusu makusudi yake. (Zab. 26:4) Mtu anayejiita kuwa Shahidi wa Yehova anaweza kuwa mtu asiyeamini, mtu aliyetengwa na ushirika, au hata mwasi-imani anayejikaza sana ili kuangusha Wakristo wengine. (Gal. 2:4) Inaripotiwa kwamba watu wengi wanaofanya ngono na watoto wanatumia vituo hivyo ili kuwapata watoto hao.
Hata ikiwa tunasadikishwa kwamba watu ambao tunapashana habari nao wana msimamo mzuri katika kutaniko, mazungumzo kupitia njia hiyo yanaweza kugeuka na kuwa mazungumzo yasiyofaa. Hilo ni kwa sababu watu wanashindwa kujizuia wanapozungumza na watu ambao hawajapata kukutana nao moja kwa moja. Pia wanaweza kuona mazungumzo kupitia Internete kuwa ya kisiri na kufikiri kwamba jambo lolote wanalosema halitajulikana na watu wengine, kama vile wazazi wao au wazee. Ni jambo lenye kuhuzunisha kwamba vijana wengi walio katika familia za Kikristo, wamenaswa hivyo na wamejiingiza katika mazungumzo machafu. (Efe. 5:3, 4; Kol. 3:8) Wengine wametia picha zao zinazochochea tamaa ya ngono, majina ya kujibandika yasiyofaa, au wametia video za miziki zisizofaa katika maelezo wanayotia ndani ya kompyuta (ordinateur) zao.
Kuhusiana na mambo yanayotoka kutajwa, wazazi wanapaswa kuchunguza ili kujua mambo ambayo watoto wao wanafanya katika kutumia kompyuta. (Met. 29:15) Itakuwa hatari kualika mgeni katika nyumba yetu au kumruhusu abaki yeye mwenyewe na watoto wetu. Vivyo hivyo, ni jambo lenye hatari kwetu au kwa watoto wetu kufanya urafiki na watu tusiowajua kupitia Internete, hata ikiwa watu hao wanajiita eti wao ni Mashahidi wa Yehova.—Met. 22:3.