Usijizuie Kuanzisha Funzo kwa Sababu Unawaza Hauna Uwezo
1. Sababu gani watu fulani wanajizuia kuanzisha funzo la Biblia?
1 Je, unajizuia kuanzisha funzo la Biblia kwa sababu unawaza hauna uwezo wa kuliongoza vizuri? Wakati fulani, watumishi waaminifu wa zamani, kama vile Musa na Yeremia, walijisikia kama hawana uwezo wa kutimiza migawo yao. (Kut. 3:10, 11; 4:10; Yer. 1:4-6) Kwa hiyo, ni kawaida kujisikia hivyo. Namna gani tunaweza kushindana na hali hiyo?
2. Sababu gani tusitosheke tu na mahubiri ya nyumba kwa nyumba na kuwaachia wengine kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia?
2 Tunapaswa kukumbuka kama Yehova hatuombe hata kidogo tufanye mambo yanayopita uwezo wetu. (Zab. 103:14) Kwa hiyo, kazi ya ‘kufanya wanafunzi’ na ‘kuwafundisha’ aliyotuomba tufanye haipite uwezo wetu. (Mt. 28:19, 20) Hilo si pendeleo ambalo Yehova amewatolea tu watu wenye uzoefu ao wenye ufundi mwingi kati yetu. (1 Kor. 1:26, 27) Ndiyo sababu tusitosheke tu na mahubiri ya nyumba kwa nyumba na kuwaachia wengine kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia.
3. Namna gani Yehova ametupatia uwezo wa kuongoza mafunzo ya Biblia?
3 Yehova Anatupatia Uwezo: Ni Yehova ndiye anayetupatia uwezo wa kufanya wanafunzi. (2 Kor. 3:5) Kupitia tengenezo lake, ametufundisha kweli za Biblia ambazo hata watu ambao wamesoma mingi katika ulimwengu huu hawajue. (1 Kor. 2:7, 8) Katika neno lake amelinda maandishi kuhusu njia za kufundisha za Yesu, Mwalimu Mukuu, ili tumuige, na anaendelea kutuzoeza kupitia kutaniko. Tena, Yehova ametutolea vyombo vya lazima ili vitusaidie kuwafundisha watu Biblia. Ametutolea vyombo, kama vile kitabu Biblia Inafundisha, vinavyofundisha kweli kwa njia nzuri na rahisi kuelewa. Inaweza kuwa rahisi kuongoza funzo la Biblia kuliko jinsi tunavyowazia.
4. Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atatusaidia?
4 Kwa musaada wa Yehova, Musa na Yeremia walitimiza migawo yao. (Kut. 4:11, 12; Yer. 1:7, 8) Sisi pia tunaweza kumuomba Yehova atusaidie. Tunapoongoza funzo la Biblia, tunamufundisha mutu kweli juu ya Yehova, na hilo linamufurahisha Mungu. (1 Yoh. 3:22) Ndiyo sababu, uwe na muradi wa kuongoza mafunzo ya Biblia; hiyo ni sehemu ya kazi ya kuhubiri yenye kufurahisha zaidi na yenye baraka nyingi.