Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w24 Mwezi wa 7 uku. 20-25
  • Mufano wa Wafalme wa Israeli Unatufundisha Nini?

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Mufano wa Wafalme wa Israeli Unatufundisha Nini?
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2024
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • WALIMUTUMIKIA YEHOVA KWA MOYO WOTE
  • WALITUBU ZAMBI ZAO
  • WALIMUABUDU YEHOVA MU NJIA YENYE KUFAA
  • Maneno ya Mwisho-Mwisho ya Banaume Baaminifu Inakufundisha Nini?
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2024
  • Maamuzi Yenye Inaonyesha Kama Tunamutegemea Yehova
    Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo—2023
  • Kumbuka Kama Yehova Ni “Mungu Mwenye Kuishi”
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2024
  • Itika Kama Kuko Mambo Yenye Haujue
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2025
Ona Habari Zaidi
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2024
w24 Mwezi wa 7 uku. 20-25

HABARI YA KUJIFUNZA YA 30

WIMBO 36 Tulinde Moyo Wetu

Mufano wa Wafalme wa Israeli Unatufundisha Nini?

“Mutaona tena tofauti kati ya mutu mwenye haki na mutu muovu, kati ya mutu mwenye kumutumikia Mungu na mwenye hamutumikie.”—MAL. 3:18.

WAZO KUBWA

Kujifunza namna Yehova aliona wafalme wa Israeli kutatusaidia kuelewa mambo yenye Yehova anatazamia waabudu wake wafanye.

1-2. Biblia inasema nini kuhusu wafalme fulani wa Israeli?

BIBLIA inazungumuzia zaidi ya wanaume 40 wenye walikuwa wafalme wa Israeli.a Inazungumuzia pia mambo fulani ya pekee juu ya wamoja kati yao. Kwa mufano, hata wafalme wazuri walifanya mambo fulani ya mubaya. Fikiria mufalme muzuri Daudi. Yehova alisema hivi juu yake: “Mutumishi wangu . . . alinifuata kwa moyo wake wote, akifanya tu mambo yenye yalikuwa sawa mbele ya macho yangu.” (1 Fa. 14:8) Lakini Daudi alifanya uzinifu na bibi ya mwanaume mwingine, na akafanya mipango juu bwana yake auawe mu vita.—2 Sa. 11:4, 14, 15.

2 Kuko pia wafalme wengi wabaya wenye walifanya mambo fulani ya muzuri. Fikiria Mufalme Rehoboamu. Biblia inasema kama “alifanya mambo ya mubaya.” (2 Ny. 12:14) Lakini alitii amri ya Yehova ya kuruhusu makabila kumi itoke mu ufalme wake na ikuwe na mufalme mwingine. Alisaidia pia kulinda watu wake kwa kutia nguvu miji.—1 Fa. 12:21-24; 2 Ny. 11:5-12.

3. Unaweza kujiuliza ulizo gani ya maana, na tutazungumuzia nini mu hii habari?

3 Unaweza kujiuliza hii ulizo ya maana: Kama wafalme wa Israeli walifanya mambo ya muzuri na ya mubaya, ni nini njo ilifanya Yehova aamue ikiwa Mufalme fulani alikuwa muaminifu? Jibu ya ile ulizo itatusaidia kuelewa mambo yenye Yehova anapenda tufanye juu atukubali. Tutazungumuzia mambo tatu yenye inawezekana Yehova aliangalia ili kuamua ikiwa wafalme fulani wa Israeli walikuwa waaminifu ao hapana: Hali ya moyo wao, ikiwa walitubu, na ikiwa walimuabudu mu njia yenye kufaa.

WALIMUTUMIKIA YEHOVA KWA MOYO WOTE

4. Kulikuwa tofauti gani kati ya wafalme wa Israeli waaminifu na wenye hawakukuwa waaminifu?

4 Wafalme wenye walimufurahisha Yehova walimuabudu kwa moyo wote.b Mufalme muzuri Yehoshafati “alitafuta Yehova kwa moyo wake wote.” (2 Ny. 22:9) Biblia inasema hivi juu ya Yosia: “Hakuna mufalme mwenye alikuwa kama yeye, mwenye alimurudilia Yehova kwa moyo wake wote.” (2 Fa. 23:25) Halafu Sulemani, mwenye ku mwisho wa maisha yake alifanya mambo ya mubaya? Biblia inasema hivi juu yake: “Moyo wake haukukuwa kamili.” (1 Fa. 11:4) Na kuhusu Abiyamu, mufalme mwingine mubaya, Biblia inasema hivi: “Moyo wake haukukuwa kamili kumuelekea Yehova.”—1 Fa. 15:3.

5. Kumutumikia Yehova kwa moyo wote maana yake nini?

5 Sasa, kumutumikia Yehova kwa moyo wote maana yake nini? Mutu mwenye anamutumikia Mungu kwa moyo wote hamuabudu juu tu anajua kama ile njo jambo yenye anapaswa kufanya. Lakini anamutumikia kwa sababu anamupenda na anapenda kujitoa kabisa kwake. Zaidi ya ile, anaendelea kumupenda Mungu na kumuheshimia mu maisha yake yote.

6. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kumutumikia Mungu kwa moyo wote? (Mezali 4:23; Matayo 5:29, 30)

6 Namna gani tunaweza kuiga mufano wa wafalme waaminifu na kuendelea kumutumikia Yehova kwa moyo wote? Tunapaswa kuepuka mambo yenye inaweza kutuongoza ku zambi. Kwa mufano, mambo ya kujifurahisha yenye haifae, marafiki wabaya, na kupenda sana vitu vya kimwili, kunaweza kugawanya moyo wetu. Kama tunatambua kama jambo fulani inaanza kupunguza upendo wetu kwa Yehova, tutende bila kukawia na tuepuke kabisa ile jambo.—Soma Mezali 4:23; Matayo 5:29, 30.

7. Juu ya nini tunapaswa kuepuka jambo yoyote yenye inaweza kupunguza upendo wetu kwa Yehova?

7 Hatupaswe kuacha moyo wetu ugawanyike. Kama hatuko waangalifu, tunaweza kujidanganya kwa kuwaza kama ikiwa tunaongeza bidii yetu mu mambo ya kiroho, mambo ya mubaya haitakuwa na matokeo juu yetu. Ili kuelewa, fikiria hii mufano: Wazia kuko baridi sana na upepo. Wakati unafika ku nyumba, unakonga moto. Lakini, ile moto itakusaidia kabisa kama unaacha mulango wazi? Hapana. Hewa ya baridi itaingia tena na kujaa mu nyumba yote. Somo ni nini? Haitoshe tu kula chakula ya kiroho yenye inafanya tubakie karibu na Yehova. Tunapaswa pia kufungia mulango mambo ya mubaya. Ile itafanya “hewa” ya mubaya ya huu ulimwengu, ni kusema tabia zenye hazimufurahishe Mungu zisiingie mu moyo wetu na kuugawanya.—Efe. 2:2.

WALITUBU ZAMBI ZAO

8-9. Mufalme Daudi na Mufalme Hezekia walitenda namna gani wakati walirekebishwa? (Ona picha.)

8 Sawa vile tuliona, Mufalme Daudi alifanya makosa makubwa. Lakini wakati nabii Natani alimukaripia kwa sababu ya zambi zake, Daudi alitubu kwa unyenyekevu. (2 Sa. 12:13) Maneno yake yenye kuwa mu Zaburi 51, inaonyesha kama alitubu kutoka ku moyo. Daudi hakufanya sawa vile anahuzunikia makosa yake juu tu ya kumudanganya Natani ao juu tu ya kuepuka malipizi.—Zb. 51:3, 4, 17, utangulizi.

9 Mufalme Hezekia naye alimukosea Yehova. Biblia inasema hivi: “Moyo wake ulikuwa na majivuno, na hilo likaleta kasirani juu yake na juu ya Yuda na Yerusalemu.” (2 Ny. 32:25) Juu ya nini Hezekia alifikia kuwa na kiburi? Pengine alijiona kuwa wa maana sana kwa sababu ya utajiri wake, ao kwa sababu alishinda Waashuri, ao tena kwa sababu alipona kwa muujiza. Inawezekana ni kiburi njo ilimuchochea aonyeshe Wababiloni mali yake. Na ile ilifanya nabii Isaya amukaripie. (2 Fa. 20:12-18) Lakini kama Daudi, Hezekia alitubu kwa unyenyekevu. (2 Ny. 32:26) Na ku mwisho, Yehova alimuona kuwa mufalme muaminifu, mwenye “aliendelea kufanya mambo yenye yalikuwa sawa.”—2 Fa. 18:3.

Picha: 1. Mufalme Daudi iko naangalia juu kwa huzuni wakati Natani iko nazungumuza naye. 2. Mufalme Hezekia anajikamata ku kichwa kwa huzuni wakati Isaya iko nazungumuza naye.

Mufalme Daudi na Mufalme Hezekia walijinyenyekeza na wakatubu wakati walirekebishwa kwa sababu ya zambi zao (Ona fungu ya 8-9)


10. Mufalme Amazia alitenda namna gani wakati alirekebishwa?

10 Mufalme Amazia alitenda namna gani wakati alirekebishwa? Mufalme Amazia wa Yuda alifanya mambo ya muzuri “lakini hapana kwa moyo kamili.” (2 Ny. 25:2) Mambo ilikuwa namna gani? Kisha Yehova kumusaidia kushinda Waedomu, aliabudu miungu yao.c Wakati nabii wa Yehova alikuya kumurekebisha, Amazia hakupenda kabisa kumusikiliza na akamufukuza.—2 Ny. 25:14-16.

11. Kulingana na 2 Wakorinto 7:9, 11, tunapaswa kufanya nini juu Mungu atusamehe? (Ona pia picha.)

11 Hii mi fano inatufundisha nini? Tunapaswa kutubu zambi zetu na kufanya yetu yote ili tusizirudilie. Sasa, tutafanya nini kama wazee wa kutaniko wanatutolea mashauri hata mu mambo yenye inaonekana kuwa ya kidogo? Hatupaswe kuwaza kama Yehova hatukubali tena ao kama wazee hawatupendi. Hata wafalme wazuri wa Israeli walishauriwa na kurekebishwa. (Ebr. 12:6) Wakati tunarekebishwa tunapaswa (1) kukubali mashauri kwa unyenyekevu, (2) kufanya mabadiliko, na (3) kuendelea kumutumikia Yehova kwa moyo wote. Kama tunatubu zambi zetu Yehova atatusamehe.—Soma 2 Wakorinto 7:9, 11.

Picha: 1. Muzee wa kutaniko mweye ni kijana anazungumuza na ndugu fulani wakati ule ndugu iko naangalia chupa ya pombe na vere yenye muko pombe ya kidogo. 2. Ule ndugu anafanya utafiti kwa kutumia Biblia na kitabu “Furahia Maisha Milele!” 3. Ule muzee wa kutaniko mwenye ni kijana iko mu mahubiri ya nyumba kwa nyumba pamoja na ule ndugu.

Wakati tunarekebishwa tunapaswa (1) kukubali mashauri kwa unyenyekevu, (2) kufanya mabadiliko, na (3) kuendelea kumutumikia Yehova kwa moyo wote (Ona fungu ya 11)f


WALIMUABUDU YEHOVA MU NJIA YENYE KUFAA

12. Ni nini ilifanya wafalme waaminifu wakuwe tofauti kabisa na wafalme wabaya?

12 Wafalme wenye Yehova aliona kuwa waaminifu walimuabudu mu njia yenye anapenda. Na walitia watu moyo wafanye vile. Sawa vile tumeona, ni kweli kama walifanya makosa. Lakini walikuwa wameshikamana na Yehova na hata walifanya yao yote ili kuondoa kabisa ibada ya sanamu mu inchi.d

13. Juu ya nini Yehova alimuona Ahabu kuwa mufalme mubaya?

13 Tuseme nini juu ya wafalme wenye Yehova aliona kuwa wabaya? Kwa kweli haiko mambo yote yenye walifanya njo ilikuwa ya mubaya. Hata mufalme muovu Ahabu alionyesha unyenyekevu kwa kiasi fulani na kuhuzunika juu ya namna alichangia kumuua Naboti. (1 Fa. 21:27-29) Pia alijenga miji na alishinda vita mbalimbali kwa ajili ya Israeli. (1 Fa. 20:21, 29; 22:39) Lakini, kwa kuchochewa na bibi yake, Ahabu alieneza sana ibada ya uongo. Na hakutubu hata siku moya juu ya ile.—1 Fa. 21:25, 26.

14. (a) Juu ya nini Yehova alimuona Mufalme Rehoboamu kuwa mufalme mubaya? (b) Mambo ilikuwa namna gani wakati wa utawala wa wafalme wabaya?

14 Fikiria mufano wa Rehoboamu, mufalme mwingine mubaya. Sawa vile tuliona, alifanya mambo fulani ya muzuri wakati wa utawala wake. Lakini wakati ufalme wake ulikuwa wenye nguvu, aliacha Sheria ya Yehova na akaanza kuabudu miungu ya uongo. (2 Ny. 12:1) Kisha aliendelea kuchanga ibada ya kweli na ibada ya uongo. (1 Fa. 14:21-24) Haiko tu Rehoboamu na Ahabu njo wafalme wenye waliacha ibada safi. Kwa kweli, wafalme wengi wabaya waliunga mukono ibada ya uongo mu njia fulani. Ni wazi kama kuunga mukono ibada safi ilikuwa jambo ya maana sana yenye Yehova aliangalia ili kuamua ikiwa mufalme alikuwa muzuri ao mubaya.

15. Juu ya nini kuabudu Yehova mu njia yenye anapenda ni jambo ya maana sana kwake?

15 Sababu gani mambo yenye kuhusu ibada ilikuwa ya maana sana kwa Yehova? Sababu moya ni hii: Wafalme walipaswa kusaidia watu wamuabudu Yehova mu njia ya muzuri. Pia ibada ya uongo inachocheaka watu kufanya zambi zingine nzito na inaletaka matendo ya ukosefu wa haki. (Hos. 4:1, 2) Zaidi ya ile, wafalme na watu wenye walikuwa chini ya mamlaka yao, walikuwa wamejitoa kwa Yehova. Njo maana Biblia inalinganisha ibada ya uongo na uzinifu. (Yer. 3:8, 9) Mutu mwenye anafanya uzinifu anakosea sana tena sana bibi ao bwana yake. Ni vile pia wakati mutumishi wa Yehova mwenye kujitoa kwake anajiingiza mu ibada ya uongo, anamukosea Yehova sana tena sana.e—Kum. 4:23, 24.

16. Nini njo inafanya watu wenye haki wakuwe tofauti na watu wabaya?

16 Tunajifunza nini? Tunapaswa kuazimia kuepuka ibada ya uongo. Lakini tunapaswa pia kubakia mu ibada ya kweli na kuendelea kumutumikia Yehova kwa bidii. Nabii Malaki alisema waziwazi jambo yenye inafanya Yehova aamue ikiwa mutu fulani ni muzuri ao ni mutu mubaya. Malaki aliandika hivi: “Mutaona tena tofauti kati ya mutu mwenye haki na mutu muovu, kati ya mutu mwenye kumutumikia Mungu na mwenye hamutumikie.” (Mal. 3:18) Njo maana hatupaswe kuruhusu kitu yoyote, hata uzaifu wetu na makosa yetu, ituvunje moyo mupaka tufikie kuacha kumutumikia Mungu. Juu ya nini? Juu kuacha kumutumikia Yehova nayo ni zambi nzito.

17. Juu ya nini tunapaswa kuwa waangalifu wakati tunachagua mutu mwenye tutaoana naye?

17 Kama uko nafikiria kufunga ndoa, maneno ya nabii Malaki inaweza kukusaidia uchague muzuri mutu mwenye utaoana naye. Fikiria hii jambo: Mutu anaweza kuwa na sifa za muzuri, lakini kama haiko namutumikia Mungu wa kweli, Je, Yehova anaona ule mutu kuwa mwenye haki? (2 Ko. 6:14) Kama unafunga ndoa na ule mutu, atakusaidia uendelee kumutumikia Yehova kwa uaminifu? Fikiria mufano wa Sulemani. Pengine bibi zake wapagani walikuwa na sifa fulani za muzuri, lakini hawakukuwa namuabudu Yehova. Na polepole waligeuza moyo wa Sulemani na akaanza kuabudu miungu ya uongo.—1 Fa. 11:1, 4.

18. Wazazi wanapaswa kufundisha watoto wao nini?

18 Wazazi, munaweza kutumia habari za wafalme wenye kuwa mu Biblia ili kusaidia watoto wenu wamutumikie Yehova kwa bidii. Muwasadie waelewe kama kuunga mukono ibada safi ao hapana njo ilifanya Yehova aamue ikiwa mutu fulani alikuwa mufalme muzuri ao mubaya. Mufundishe watoto wenu kupitia maneno na matendo kama mambo ya kiroho sawa vile kujifunza Biblia, kuhuzuria mikutano, na kuhubiri, njo mambo ya maana zaidi kupita mambo ingine yote. (Mt. 6:33) Kama hamufanye vile, watoto wenu wanaweza kumutumikia Yehova juu tu nyie wazazi wao muko Mashahidi wa Yehova, haiko juu wao wenyewe wanamupenda kabisa. Matokeo itakuwa nini? Hawatatia ibada ya kweli pa nafasi ya kwanza ao hata wanaweza kuacha kabisa kumutumikia Yehova.

19. Kuko tumaini gani kwa wale wenye wameacha kumutumikia Yehova? (Ona pia kisanduku “Unaweza Kumurudilia Yehova!”)

19 Kama mutu ameacha kumutumikia Yehova, ni kusema hakuna tena tumaini? Hapana, kuko tumaini juu anaweza kutubu na kurudilia tena ibada safi. Lakini juu afanye vile, anapaswa kujishusha na kukubali musaada wa wazee wa kutaniko. (Yak. 5:14) Mambo yote yenye mutu anaweza kujikaza kufanya juu ya kumurudilia Yehova, haiko kitu tukiilinganisha na furaha ya kuwa tena rafiki yake!

Unaweza Kumurudilia Yehova!

Fikiria mufano wa Mufalme Manase, mwenye “alifanya kwa kiasi kikubwa mambo ya mubaya mbele ya macho ya Yehova.” “Alimwanga damu nyingi sana,” alifanya mambo mbalimbali ya uchawi, na hata alitoa watoto wake kuwa zabihu kwa miungu ya uongo! (2 Fa. 21:6, 16) Alichochea taifa ya Yuda ‘kufanya uovu mukubwa zaidi kuliko mataifa’ ingine. (2 Fa. 21:9; 2 Ny. 33:1-6) Lakini wakati alipelekwa mu utekwa Babiloni, alitubu. Juu alikuwa amefanya zambi nzito kwa wakati murefu, hakuomba Yehova musamaha mara moya tu. Wakati alijikuta mu hali ya mubaya, Manase ‘aliendelea kujinyenyekeza’ na “aliendelea kusali.” Matokeo ilikuwa nini? Yehova alimusikiliza na ‘aliguswa na ombi lake.’ Yehova alimusamehe, alimurudisha Yerusalemu, na akamurudishia ufalme wake.—2 Ny. 33:12, 13.

Ni vile Yehova atatendea pia wale wenye wameacha ibada safi lakini wanaonyesha kama wanatubu kwa moyo wote. Isaya 55:7 inasema: “Mutu muovu aache njia yake na mutu mubaya mawazo yake; na amurudilie Yehova, mwenye atamuonyesha rehema, kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.” Kwa hiyo, usisite kufanya mambo yenye inaombwa ili kumurudilia Yehova!

20. Yehova atatuona namna gani kama tunaiga wafalme waaminifu?

20 Mufano wa wafalme wa Israeli umetufundisha nini? Tunaweza kuwa kama wafalme waaminifu ikiwa tunaendelea kumutumikia Yehova kwa moyo wote. Tukifanya makosa, tutubu na tubadilike. Na tukumbuke kama ni jambo ya maana sana tuendelee kuabudu tu Mungu mumoja wa kweli, Yehova. Kama unaendelea kushikamana na Yehova, atakuona kuwa mutu mwenye kufanya mambo yenye kuwa sawa.

NAMNA GANI TUNAWEZA . . .

  • kuendelea kumutumikia Yehova kwa moyo wote?

  • kuonyesha kama tumetubu?

  • kuendelea kuabudu Yehova mu njia yenye kufaa?

WIMBO 45 Mawazo ya Moyo Wangu

a Mu hii habari, maneno “wafalme wa Israeli” inamaanisha wafalme wote wenye walitawala watu wa Yehova, ikuwe walitawala mu ufalme wa Yuda wa makabila mbili, ao ufalme wa Israeli wa makabila kumi, ao tena ufalme wa makabila yote kumi na mbili.

b MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Mara mingi Biblia inatumia neno “moyo” ili kuzungumuzia mutu wa ndani, ni kusema tamaa, mawazo, muelekeo, mutazamo, uwezo, nia, na miradi ya mutu.

c Inaonekana kama wafalme wapagani walizoea kuabudu miungu ya mataifa yenye walishinda mu vita.

d Mufalme Asa alifanya zambi nzito za mingi. (2 Ny. 16:7, 10) Lakini, Biblia inasema kama alifanya mambo yenye kuwa sawa mbele ya macho ya Yehova. Hata kama ku mwanzo hakukubali wakati alirekebishwa, inawezekana alifikia kutubu. Inawezekana sifa zake za muzuri zilifikia kuwa za mingi kupita makosa yake. Kwa ujumla Asa alimuabudu Yehova tu na alijikaza kuondoa ibada ya sanamu mu ufalme wake.—1 Fa. 15:11-13; 2 Ny. 14:2-5.

e Tunaelewa juu ya nini amri za kwanza za Sheria ya Musa zilikataza kuabudu mutu mwingine ao kitu ingine isipokuwa tu Yehova.—Kut. 20:1-6.

f MAFASIRIO YA PICHA: Kijana mwenye kuwa muzee wa kutaniko iko nazungumuza na ndugu fulani juu ya tabia yake ya kunywa sana. Kwa unyenyekevu ule ndugu anakubali mashauri, anafanya mabadiliko, na anaendelea kumutumikia Yehova kwa uaminifu.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine