Kisanduku Cha Maulizo
◼ Je, Mashahidi wa Yehova wanaweza kuwagawia wengine hotuba zilizorekodiwa ao zilizoandikwa?
Hotuba zenye kutegemea Biblia zinatujenga na kututia moyo. (Mdo. 15:32) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kuwatolea wale ambao hawakuwa kwenye mkutano habari hizo zenye kujenga. Kwa kuwa leo kuna vifaa mbalimbali vya kurekodi, ni rahisi kurekodi hotuba na kuitolea wengine. Watu fulani wamejikusanyia hotuba nyingi zilizorekodiwa, hata zile zilizotolewa miaka mingi iliyopita, na kwa nia nzuri wanazitolea wengine ao wanafanya kopi kwa ajili ya marafiki. Wengine wameunda vituo vya Internet na kutia hotuba kwenye vituo hivyo kwa ajili ya mutu yeyote anayetaka kuzichukua.
Kwa kweli, si vibaya ikiwa mutu anarekodi hotuba kwa ajili yake mwenyewe ao kwa ajili ya watu wa familia yake. Pia, wazee wanaweza kufanya mpango ili hotuba zirekodiwe kwa ajili ya washiriki wa kutaniko walio wagonjwa ambao hawana uwezo wa kufika kwenye mikutano. Lakini, kuna sababu zinazofanya isiwe vizuri kugawia wengine hotuba tulizoandika ao kurekodi.
Mara nyingi hotuba zinatolewa kulingana na mahitaji ya wasikilizaji. Kwa hiyo, ni rahisi tuelewe vibaya habari fulani katika hotuba iliyorekodiwa ambayo tunatolewa, kwa sababu hatujui kwa nini na katika hali gani hotuba hiyo ilitolewa. Pia, itakuwa vigumu kwetu kujua ni nani aliyetoa hotuba hiyo na wakati gani, ili tuwe na uhakika kwamba habari inayotolewa ni ya sasa na ya kweli. (Luka 1:1-4) Kwa kuongezea, kugawia watu hotuba tulizoandika ao kurekodi kunaweza kuwafanya watu fulani watoe ao wakubali heshima isiyofaa.—1 Kor.3:5-7.
Mtumwa mwaminifu na mwenye busara anatumika kwa bidii ili kututolea chakula cha kiroho kwa “kipimo” kinachofaa na kwa “wakati unaofaa.” (Luka 12:42) Hilo linahusisha pia mpango wa kufanya hotuba zitolewe katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova na habari za kusikiliza ambazo tunaweza kuchukua kwenye kituo chetu cha Internet jw.org. Tunaweza kuwa hakika kwamba mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza lake Linaloongoza watatutolea yale tunayohitaji ili tuwe imara katika imani.—Mdo. 16:4, 5.