2 Wakorintho
6 Tukiwa tunafanya kazi pamoja naye, twawasihi sana nyinyi pia msiipokee fadhili isiyostahiliwa ya Mungu na kukosa kusudi layo. 2 Kwa maana yeye asema: “Wakati wenye kukubalika nilikusikia, na siku ya wokovu nilikusaidia.” Tazameni! Sasa ndio wakati wenye kukubalika hasa. Tazameni! Sasa ndiyo siku ya wokovu.
3 Katika njia yoyote sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili huduma yetu isitafutiwe kosa; 4 bali katika kila njia twajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu, kwa uvumilivu wa mengi, kwa dhiki nyingi, kwa visa vya uhitaji, kwa magumu, 5 kwa mapigo, kwa magereza, kwa mivurugo, kwa kazi za jasho, kwa masiku ya kukosa usingizi, kwa nyakati za kuwa bila chakula, 6 kwa utakato, kwa ujuzi, kwa ustahimilivu, kwa fadhili, kwa roho takatifu, kwa upendo bila unafiki, 7 kwa usemi wenye kweli, kwa nguvu ya Mungu; kupitia silaha za uadilifu katika mkono wa kuume na katika wa kushoto, 8 kupitia utukufu na fedheha, kupitia ripoti mbaya na ripoti njema; kama wadanganyi na bado wenye kusema kweli, 9 kama wasiojulikana na bado wenye kutambuliwa, kama wenye kufa na bado, tazameni! twaishi, kama wenye kutiwa nidhamu na bado wasiokabidhiwa kwenye kifo, 10 kama wenye kuona majonzi lakini wenye kushangilia daima, kama maskini lakini wenye kufanya wengi wawe matajiri, kama wasio na kitu chochote na bado wenye kumiliki vitu vyote.
11 Kinywa chetu kimefunguliwa kwenu, Wakorintho, moyo wetu umepanuka. 12 Nyinyi hamjafinywa mkakosa nafasi katika sisi, lakini mmefinywa mkakosa nafasi katika shauku nyororo zenu wenyewe. 13 Kwa hiyo, yakiwa malipo kwa kurudisha—mimi nasema kama kwa watoto—nyinyi, pia, panukeni.
14 Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini. Kwa maana uadilifu na uasi-sheria vina ushirika gani? Au nuru ina ushiriki gani na giza? 15 Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini? 16 Na hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu aliye hai; kama vile Mungu alivyosema: “Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” 17 “‘Kwa hiyo tokeni miongoni mwao, na jitengeni wenyewe,’ asema Yehova, ‘na komeni kugusa kitu kisicho safi’”; “‘na hakika mimi nitawakaribisha ndani.’” 18 “‘Na mimi nitakuwa baba kwenu, na nyinyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’ asema Yehova Mweza-Yote.”