Waebrania
3 Kwa sababu hiyo, ndugu watakatifu, washiriki wa mwito wa kimbingu, mfikirieni mtume na kuhani wa cheo cha juu ambaye twaungama—Yesu. 2 Yeye alikuwa mwaminifu kwa Yule aliyemfanya kuwa namna hiyo, kama vile Musa alivyokuwa pia katika nyumba yote ya Huyo. 3 Kwa maana huyu wa mwisho ahesabiwa kustahili utukufu zaidi ya Musa, kwa kadiri yeye ajengaye alivyo na heshima zaidi ya nyumba. 4 Bila shaka, kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu. 5 Na Musa akiwa hadimu alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Huyo kuwa ushuhuda wa mambo yaliyopaswa kusemwa baadaye, 6 lakini Kristo alikuwa mwaminifu akiwa Mwana juu ya nyumba ya Huyo. Sisi ndio nyumba ya Huyo, ikiwa twashikilia kwa imara hadi mwisho uhuru wetu wa usemi na kujisifu kwetu juu ya tumaini.
7 Kwa sababu hiyo, kama vile roho takatifu husema: “Leo ikiwa nyinyi watu mtaisikiliza sauti yake mwenyewe, 8 msifanye mioyo yenu kuwa migumu kama katika pindi ya kusababisha hasira yenye uchungu, kama katika siku ya kufanya jaribu nyikani, 9 ambayo katika hiyo baba zenu wa zamani walinijaribu kwa uchunguzi, na bado wao walikuwa wameona kazi zangu kwa miaka arobaini. 10 Kwa sababu hiyo nikawa mwenye kuchukizwa sana na kizazi hiki nikasema, ‘Wao sikuzote hupotea njia katika mioyo yao, nao wenyewe hawajaja kujua njia zangu.’ 11 Kwa hiyo niliapa katika hasira yangu, ‘Hakika wao hawataingia katika pumziko langu.’”
12 Jihadharini, akina ndugu, kwa kuhofu kusije kamwe kukasitawi katika yeyote kati yenu moyo mwovu unaokosa imani kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai; 13 lakini fulizeni kuhimizana kwa bidii mtu na mwenzake kila siku, maadamu yaweza kuitwa “Leo,” kwa kuhofu yeyote kati yenu asije akafanywa kuwa mgumu kwa nguvu ya udanganyifu ya dhambi. 14 Kwa maana sisi kwa kweli twawa washiriki wa Kristo ikiwa tu twaushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni kwa imara hadi mwisho, 15 wakati inaposemwa: “Leo ikiwa nyinyi watu mwasikiliza sauti yake mwenyewe, msifanye mioyo yenu kuwa migumu kama katika pindi ya kusababisha hasira yenye uchungu.”
16 Kwa maana walikuwa akina nani waliosikia na bado wakachokoza kuwe na hasira yenye uchungu? Kwa kweli, je, hawakufanya hivyo wale wote walioenda kutoka Misri chini ya Musa? 17 Zaidi ya hayo, ni kwa akina nani Mungu alipata kuwa mwenye kuchukizwa sana kwa miaka arobaini? Je, haikuwa kwa wale waliofanya dhambi, ambao mizoga yao ilianguka nyikani? 18 Lakini ni kwa akina nani aliapa kwamba wasiingie katika pumziko lake ila kwa wale waliotenda kwa kutotii? 19 Kwa hiyo twaona kwamba hawakuweza kuingia kwa sababu ya ukosefu wa imani.