Waebrania
2 Hiyo ndiyo sababu ni lazima kwetu kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi, ili tusipate kamwe kupeperushwa mbali. 2 Kwa maana ikiwa neno lililosemwa kupitia malaika lilithibitika kuwa imara, na kila mkiuko-sheria na tendo la kutotii lilipokea malipo kwa kupatana na haki; 3 sisi tutaponyokaje ikiwa tumepuuza wokovu wa ukubwa wa namna hii kwa kuwa ulianza kusemwa kupitia Bwana wetu na ulithibitishwa kwa ajili yetu na wale waliomsikia, 4 wakati Mungu alipojiunga katika kutoa ushahidi kwa ishara nyingi na vilevile mambo ya ajabu na kazi za namna mbalimbali zenye nguvu na kwa ugawanyaji wa roho takatifu kulingana na mapenzi yake?
5 Kwa maana si kwa malaika kwamba ameitiisha dunia ijayo inayokaliwa, ambayo juu yayo sisi tunasema. 6 Bali shahidi fulani ametoa ithibati mahali fulani, akisema: “Binadamu ni nini hivi kwamba mmweke akilini, au mwana wa binadamu hivi kwamba mmjali? 7 Ulimfanya akawa chini kidogo kuliko malaika; kwa utukufu na heshima ulimvika taji, na kumweka rasmi juu ya kazi za mikono yako. 8 Vitu vyote ulivitiisha chini ya miguu yake.” Kwa maana alivitiisha vitu vyote kwake Mungu hakuacha kitu chochote kisichotiishwa kwake. Ingawa hivyo, sasa, sisi hatuoni bado vitu vyote katika ujitiisho kwake; 9 lakini twamwona Yesu, ambaye amefanywa akawa chini kidogo kuliko malaika, akavikwa taji la utukufu na heshima kwa kuwa alikwisha kupatwa na kifo, ili kwa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu aonje kifo kwa ajili ya kila mtu.
10 Kwa maana ilifaa yule ambaye kwa ajili yake vitu vyote vipo na kupitia kwake vitu vyote vipo, katika kuleta wana wengi kwenye utukufu, amfanye Wakili Mkuu wa wokovu wao kuwa mkamilifu kupitia mateso. 11 Kwa maana yeye anayetakasa na wale wanaotakaswa pia hutokana na mmoja, na kwa sababu hii yeye haaibiki kuwaita “ndugu,” 12 kama asemavyo: “Hakika nitatangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko hakika nitakusifu wewe kwa wimbo.” 13 Na tena: “Hakika nitakuwa na itibari yangu katika yeye.” Na tena: “Tazama! Mimi na watoto wachanga, ambao Yehova alinipa.”
14 Kwa hiyo, kwa kuwa “watoto wachanga” ni washiriki wa damu na mwili, yeye pia hivyohivyo alishiriki mambo yaleyale, ili kupitia kifo chake apate kumfanya kuwa si kitu yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi; 15 na kwamba apate kuwaweka huru wale wote ambao kwa hofu ya kifo walitiishwa kwenye utumwa maisha zao zote. 16 Kwa maana kwa kweli yeye hawasaidii malaika hata kidogo, bali anasaidia mbegu ya Abrahamu. 17 Kwa sababu hiyo aliwajibika kuwa kama “ndugu” zake katika mambo yote, ili apate kuwa kuhani wa cheo cha juu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu, kusudi atoe dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi za watu. 18 Kwa maana yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akitiwa kwenye jaribu, aweza kuja kusaidia wale wanaotiwa kwenye jaribu.