-
Marko 11:27-33Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
27 Wakaja tena Yerusalemu. Na alipokuwa akitembea hekaluni, wakuu wa makuhani, waandishi, na wazee wakaja 28 na kumuuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Au ni nani aliyekupa mamlaka ya kufanya mambo haya?”+ 29 Yesu akawaambia: “Nitawauliza swali moja. Mkinijibu, nitawaambia ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani. 30 Je, ubatizo wa Yohana+ ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?* Nijibuni.”+ 31 Basi wakaanza kujadiliana kati yao, wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Basi, kwa nini hamkumwamini?’ 32 Lakini je, tutathubutu kusema, ‘Ulitoka kwa wanadamu’?” Kwa kuwa waliogopa umati, kwa maana umati wote uliamini kwa kweli Yohana alikuwa nabii.+ 33 Basi wakamjibu Yesu: “Hatujui.” Naye Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.”
-
-
Luka 20:1-8Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
20 Siku moja alipokuwa akifundisha watu hekaluni na kutangaza habari njema, wakuu wa makuhani, waandishi na wazee wakaja, 2 nao wakasema: “Tuambie, unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Au ni nani aliyekupa mamlaka hayo?”+ 3 Akawajibu: “Mimi pia nitawauliza swali, nanyi mnijibu: 4 Je, ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?”* 5 Wakaanza kujadiliana kati yao wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Kwa nini hamkumwamini?’ 6 Lakini tukisema, ‘Ulitoka kwa wanadamu,’ watu wote watatupiga mawe, kwa sababu wanaamini Yohana alikuwa nabii.”+ 7 Basi wakamjibu kwamba hawajui chanzo chake. 8 Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.”
-