Yeremia
24 Kisha Yehova akanionyesha vikapu viwili vya tini vilivyowekwa mbele ya hekalu la Yehova, baada ya Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni kumpeleka uhamishoni Yekonia*+ mwana wa Yehoyakimu,+ mfalme wa Yuda, pamoja na wakuu wa Yuda, mafundi, na wahunzi;* aliwatoa Yerusalemu na kuwapeleka Babiloni.+ 2 Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini za mapema, lakini kile kikapu kingine kilikuwa na tini mbaya sana, zilikuwa mbaya sana hivi kwamba hazingeweza kuliwa.
3 Kisha Yehova akaniuliza: “Unaona nini, Yeremia?” Basi nikasema: “Tini; tini nzuri ni nzuri sana, na tini mbaya ni mbaya sana, hivi kwamba haziwezi kuliwa.”+
4 Ndipo neno la Yehova likanijia likisema: 5 “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kama hizi tini nzuri, ndivyo nitakavyowaona kwa njia nzuri wale watu wa Yuda waliohamishwa, ambao nimewatoa mahali hapa na kuwapeleka katika nchi ya Wakaldayo. 6 Jicho langu litaendelea kuwatazama kwa faida yao, nami nitawarudisha katika nchi hii.+ Nitawajenga, nami sitawabomoa; nitawapanda, nami sitawang’oa.+ 7 Nami nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova.+ Watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao,+ kwa maana watarudi kwangu kwa moyo wao wote.+
8 “‘Lakini kuhusu tini mbaya ambazo ni mbaya sana hivi kwamba haziwezi kuliwa,+ Yehova anasema hivi: “Ndivyo nitakavyomwona Mfalme Sedekia+ wa Yuda, wakuu wake, wakaaji wa Yerusalemu waliobaki katika nchi hii, na wale wanaokaa nchini Misri.+ 9 Nitawafanya wawe kitu cha kutisha na msiba kwa falme zote za dunia,+ shutuma, methali, kitu cha kudhihakiwa, na laana+ kila mahali nitakapowatawanya.+ 10 Nami nitawaletea upanga,+ njaa kali, na ugonjwa hatari,+ mpaka waangamie kutoka katika nchi niliyowapa wao na mababu zao.”’”