Vijana Wanauliza . . .
Nishughulikeje na Mzazi Wangu Aliyeondoka Nyumbani?
“Siku ambazo Baba alikuwa ameahidi kuja kutuchukua twende matembezi, Mama alikuwa akituvisha vizuri mimi na dada yangu vizuri sana. Na kisha tulikuwa tukiketi na kumngojea. Na kungojea. Saa baada ya saa ilikuwa ikipita. Mwishowe, Mama angezema, ‘Ni saa ya kulala.’ Tungeanzakulia na kusema, “Atakuja, atakuja!’ Hata asubuhi ifuatayo, tulikuwa tukimngojea lakini wapi, Baba hakuonekana. Nyakati nyingine hiyo ilionekana kuwa ndiyo hadithi ya maisha yetu.”—Anne.a
IKIWA, kama Anne, umeona wazazi wako wakiachana, labda unaweza kufahamu ni kwa nini Yehova, Mbuni wa ndoa, hupinga sana talaka. (Linganisha Malaki 2:16.) Talaka huumiza kila mtu anayehusika—hata wakati mzazi aliyekosewa anapokuwa na haki ya Kimaandiko ya kutaliki yule mwingine.b
Lakini wazazi wanapoachana hatimaye, labda kupitia talaka halali, kwa lazima hilo halimalizi matatizo yote ambayo kutopatana kwao kwaweza kukuletea. Kwa hakika, huenda sasa ukawa na tatizo gumu la kukabili: kuamua kama utadumisha aina fulani ya uhusiano na mzazi aliyeondoka nyumbani. Meg akumbuka jinsi jambo hilo linavyoweza kuwa gumu: “Niliduwaa sana hivi kwamba sikuwa tena na hisia zozote za moyoni. Kwa hiyo kwa wakati fulani, sikuhisi lolote. Ilikuwa kana kwamba baba yangu alikuwa amekufa.” Na Mike akumbuka: “Nilianza kumchukia baba yangu, na hisia hiyo iliendelea kwa muda mrefu. Nilipokuwa nikifikiria jinsi alivyoacha mwanamke na watoto wanne, akifanya ujanja wa kumpa riziki ndogo kadiri ingewezekana—basi, jambo hilo lilinikasirisha sana.”
Jenga Madaraja, Usiyachome
Katika mvurugo na msukosuko wa kipindi hiki maishani mwako, ni rahisi sana kufungia mmoja wa wazazi wako mlango wa shauku zako na kuachilia hasira na uchungu zikujae. Lakini kuweka kinyongo cha aina hiyo kwaweza kuharibu mtazamo wako wa maisha. Hasira kama hiyo yaweza kukuongoza uchome madaraja yako, na kuharibu uhusiano wako na mzazi mmoja mpaka karibu usiwezekane kuimarishwa tena.
Biblia haitupi kibali cha kutoheshimu wazazi wetu. (Linganisha Luka 18:20.) Wastadi wanakubali kwamba mara nyingi unapaswa kujaribu kudumisha uhusiano na wazazi wote wawili baada ya wao kuachana. Profesa wa kutibu ugonjwa wa akili Dkt. Robert E. Gould aliandika katika gazeti Seventeen kwamba kuona wazazi wote wawili kwa ukawaida huenda kukasaidia ujirekebishe kupatana na hiyo talaka. Watafiti Wallerstein na Kelly pia waligundua kwamba vijana waliofaulu baada ya talaka ya wazazi wao, kwa ujumla walikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wote wawili. Lakini unaweza kuwaje na ukaribu pamoja na mzazi aliyeondoka nyumbani mwenu au amekosea?c
Ufahamu—Ufunguo wa Kuleta Amani
Mwanzoni hasira yako ya kiasili, inaweza kukuzuia. Lakini ukifanya mradi wako uwe kufahamu mzazi wako vizuri zaidi, mwono-ndani unaotokana na hilo unaweza kusaidia kuondosha hasira yako. Ni kama Mithali 19:11 inavyosema: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” Hilo bila shaka ni rahisi zaidi wakati huzuni au toba imeonyeshwa na aliye na hatia. Kumbuka, kupata ufahamu juu ya maoni, utu, na udhaifu wa kibinadamu wa mzazi aliyeondoka hakumaanishi kwa lazima kwamba unafunika hatia ya mzazi huyo au unaunga mkono mzazi huyo katika ugomvi wa talaka; wala haimaanishi kwamba unamsaliti mzazi unayekaa naye. Inamaanisha tu kukuza mtazamo ulio halisi zaidi wa mzazi wako.
Kwa mfano, vijana wengi husadiki kwamba ni lazima mzazi aliyeondoka nyumbani iwe awachukia—ikiwa sivyo, mbona mzazi huyo akaondoka? Lakini kwa kweli, mwachano ulikuwa kwa sababu ya matatizo ya ndoa, si kwa sababu yako. Ni yamkini kwamba mzazi aliyeondoka hakutaka kukutupilia mbali, kwa kuondoka—ingawa huenda ukahisi hivyo. Ni kama vile Dkt. Gould alivyosema juu ya jambo hilo: “Yawezekana sana kwamba, wazazi waliokupenda kabla ya talaka watakupenda kwa kadiri hiyo hiyo baadaye.”
‘Basi mbona yeye hatutembelei sana?’ huenda ukauliza. Mzazi anapokosa tena na tena wakati wa ziara zilizoratibiwa, au iwapo anawasiliana nawe mara kwa mara tu, inaweza kuonekana kwamba kwa kweli hataki kukuona. Lakini huenda isiwe hivyo hata kidogo. Nyakati nyingine, mzazi ajua kwamba tabia yake kabla ya kuachana iliacha familia imeudhika sana. Kama umewahi kuumiza hisia za rafiki yako, unajua jinsi inavyoweza kuwa vigumu kukabiliana naye uso kwa uso baadaye! Ni kama Mithali 18:19 inavyosema: “Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu.”
Kwa sababu ya hisia za hatia, huenda mzazi wako akaogopa kwa njia hiyo hiyo pia kuonana na familia. Kiburi kinaweza kuwa sababu pia. Huenda hata ikawa kwamba mzazi aliyeondoka hawezi kuonana na aliyekuwa mwenzi wake wa ndoa, hasa kama ndoa imefanywa upya; kulikokuwa “nyumbani” kunaweza sasa kuonekana ugenini. Sababu hizo na nyinginezo zaweza kufanya iwe vigumu kwa mzazi wako kukutembelea. Unaweza kufanyaje ili kurahisisha mambo? Katika Warumi 12:18 twasoma hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea nyinyi, mkae katika amani na watu wote.” (New International Version) Unaweza kufanyaje hivyo?
Jambo moja ni kwamba, labda ungehitaji kupunguza matumaini yako kidogo. Kutumaini kupata wakati na uangalifu mwingi zaidi wa mzazi wako kupita ule unaopata sasa hivi kutakufadhaisha na kukukatisha tamaa tu. Badala ya hivyo jaribu kufurahia wakati mchache mlio nao pamoja.
‘Lakini tuongee juu ya nini?’ huenda ukastaajabu. Ni kweli, matembezi hayo huenda yakawa magumu mwanzoni. Lakini yawezekana kwamba kuna mengi ambayo mzazi wako anataka kujua—kuhusu marafiki wako, maendeleo yako ya shuleni, na mapendezi yako nje ya shule. Na kuna mengi unaweza kuuliza. Talaka, bila shaka imeacha pengo tupu maishani mwa mzazi wako, kama vile katika yako pia. Kwa hiyo uwe kama “mtu mwenye ufahamu” anayezungumzwa katika Mithali 20:5, ambaye ‘huteka’ yale ‘maji ya kilindi’ ya mashauri yaliyo katika mwingine. Uliza maswali. Fahamiana na nyumba au kazi mpya ya mzazi wako, au mapendezi katika shughuli za kujifurahisha, michezo, na marafiki. Na kama huwezi kuondoa uchungu ambao mzazi wako amekusababishia, labda baada ya muda fulani, unaweza kupata njia ya mlizungumze kwa amani.
Kudumisha Usawaziko Wako
Ingawaje, kuna hatari ya kutoona makosa ya mzazi waliyeondoka. Baba ya Randy, aliyekuwa mlevi na mbembe, aliacha familia yake mara nyingi na mwishowe akataliki mama ya Randy. Hata hivyo, Randy akumbuka: “Kwa sababu fulani, kwa kweli nilimheshimu mno mwanamume huyo.”
Heshima hiyo yenye kupindukia iliyoongozwa vibaya si jambo lisilo la kawaida. Katika United States, asilimia 90 ya watoto wa wazazi waliotalikana huishi na mama na hutembelea baba. Kwa hiyo, mara nyingi mama anakuwa na daraka la kila siku la utunzi wa watoto wake—kutia na kuwatia nidhamu. Na ijapokuwa malipo ya kuwategemeza, hali ya kiuchumi ya mama hushuka chini sana baada ya talaka; hali ya baba huenda hata ikapanda. Tokeo ni: kumtembelea Baba humaanisha kupata zawadi na kuwa na wakati mzuri! Maisha pamoja na Mama humaanisha kuwa na shida za kifedha na kuambiwa la kufanya na la kutofanya. Inahuzunisha kusema, vijana wengine hata wameacha mzazi Mkristo ili kuishi na mzazi asiyeamini aliye tajiri na mwenye kuendekeza.—Linganisha Mithali 19:4.
Ikiwa unashawishwa kufanya uamuzi kama huo, changanua thamani zako. Kumbuka kwamba Muumba wako huthamini zaidi kile unachohitaji kikweli—uongozi wa kiadili na nidhamu. Hakuna kingine chochote ambacho mzazi anaweza kukutolea kitakachoathiri kwa kina kirefu mwenendo wako na thamani ya uhai wako. Nidhamu ni ishara ya upendo wa kweli.—Ona Mithali 4:13; 13:24.
Kumbuka, pia, kwamba Muumba wako ana kiwango kimoja tu cha uzuri na ubaya, hata ikiwa mzazi anakuruhusu kufanya mambo gani. Tom asema hivi: “Mama yangu hakutupinga kamwe kuonana na baba yangu. Lakini kila Ijumaa tulipoenda kumtembelea, yeye alikuwa akisema, ‘Kumbuka tu kwamba wewe ni Mkristo na kwamba Yehova huona unayoyafanya.’ Hilo lilinisaidia kusimama imara katika imani yangu wakati nilipomtembelea baba yangu.”
Hata hivyo, hata ukijaribu namna gani, huwezi sikuzote kupata kibali cha mzazi. Madokezo katika makala hii yanaweza kukusaidia ufaulu katika kuziba pengo kati yako na mzazi wako. Lakini hata ikiwa jitihada zako zote hazifaulu, usikate tamaa. Watu hubadilika. Na angalau utakuwa na uradhi wa kujua kwamba ‘kwa kadiri inavyokutegemea wewe,’ amani imedumishwa. Na jambo bora zaidi ni kwamba, utaweza kufurahia tabasamu yenye uchangamfu ya kibali cha mzazi. Ni kama Yehova asemavyo kwenye Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Unaposhikilia viwango vya Mungu kwa utiifu, na kufanya kazi ili kuonyesha mwono-ndani wenye rehema katika uhusiano wako na wazazi wako, anapendezwa. Naye ni Rafiki na Mzazi ambaye si lazima ufarakane naye.
[Maelezo ya Chini]
a Majina mengine yamebadilishwa.
b Ona sura “Kwa Nini Baba na Mama Waliachana?” katika kitabu Questions Young People Ask—Answers That Work, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
c Hapa hatuzungumzi juu ya wazazi walio na hatia ya kuwatenda watoto wao vibaya kingono au kimwili. Katika hali hizo, uhusiano wa ukaribu kati ya mzazi na mtoto huenda usiwezekane au usiwe wa hekima.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nyakati nyingine ni jaribu kuacha mzazi mmoja ili kutumia wakati na yule mwingine