Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 10/8 kur. 17-19
  • Wakati wa Kuanza na Kiasi cha Yale Utakayosema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati wa Kuanza na Kiasi cha Yale Utakayosema
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kueleza Kuzaliwa
  • Mapema Kadiri Gani?
  • Si ya Kushtua
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Kuwa na Watoto— Daraka na Thawabu
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Daraka Lenu Kama Wazazi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 10/8 kur. 17-19

Wakati wa Kuanza na Kiasi cha Yale Utakayosema

WAZAZI wengi wenye kudhamiria huonekana kuwa wanafikiri kwamba mafunzo ya ngono yanaweza kufanywa wakati wa mazungumzo yenye haya kuhusu ‘ndege na nyuki’ kwenye matembezi ya dakika kumi mwituni wakiwa na mtoto wao wa umri wa miaka 13. Lakini mara nyingi hilo huthibitika kuwa, si mafunzo madogo mno tu bali pia kuchelewa mno kwa muda wa miaka mingi. Ni kawaida kwa mzazi mwenye upendo kusema: “Ilionekana kuwa karibu kila kitu nilichojaribu kuwaambia, tayari wao walikijua.”

Je! kuna njia bora zaidi ya kufunza mambo hayo ya maana? Ikiwa ndivyo, wazazi wanapaswa kuanza lini, na wanaweza kufanya na kusema nini?

Kwa hekima, karibu tangu kuzaliwa kwa mtoto, unapaswa kuanza kuweka msingi wa kutoa maagizo hayo ya maana. Ukianza wakati mtoto ni mchanga, unaweza kutoa habari kwa utulivu, katika vipimo vidogo anavyoweza kuelewa kwa kupatana na uwezo wake wa kufaidika.

Wazazi wanapoosha watoto wao, wanaweza kuwafunza sehemu za mwili wao: “Hiki ni kifua chako . . . tumbo lako . . . goti lako.” Kwa nini uruke kutoka kwa tumbo hadi kwa goti? Je! kilicho hapo katikati ni cha kuonewa haya? Au ni cha siri tu? Bila shaka, hatungetumia maneno yasiyo na heshima ya mtaani kwa sehemu hizo za siri. Lakini kwa nini usiseme tu “uume” au “uke”? Hizo pia ni sehemu za uumbaji ambao Mungu aliuita ‘mwema sana.’—Mwanzo 1:31; 1 Wakorintho 12:21-24.

Baadaye, labda mtoto anapoona nepi ikibadilishwa, unaweza kusema kwa heshima kwamba wavulana wana uume na wasichana wana uke. Unaweza kueleza kwa upole kwamba vitu hivyo ni vya binafsi. Ni vya kusemwa tu katika familia, si na watoto wengine au watu wasio wa familia.

Hivyo, unaweza kueleza mambo mengi labda kabla hayajakuwa yenye kuonewa haya, ukianza mapema na kuendelea hatua kwa hatua kwa kadiri uwezo wa mtoto wa kuelewa ukuapo.

Kueleza Kuzaliwa

Mtoto anapokuwa na umri wa miaka mitatu hadi mitano,a huenda akaanza kujiuliza kuhusu kuzaliwa na huenda akauliza: “Watoto hutoka wapi?” Unaweza kujibu kwa kusema tu: “Ulikulia katika mahali penye joto, na usalama ndani ya mama.” Hilo litaelekea kumridhisha kwa wakati huo. Baadaye mtoto huyo huenda akauliza: “Mtoto hutokaje nje?” Unaweza kujibu kwa kusema: “Mungu alifanya mlango wa pekee ili mtoto aweze kutoka.” Uwezo wa mtoto kukazia fikira ni mdogo, kwa hiyo majibu bora zaidi ni yale mepesi na ya moja kwa moja. Toa habari inayohitajiwa kwa kiasi kidogokidogo kila wakati, ukihifadhi nyingine kwa wakati ujao.

Ikiwa wazazi wako macho, wanaweza kupata fursa nyingi za kufundisha. Ikiwa mtu wa familia ya karibu anatazamia kupata mtoto, mama anaweza kusema: “Shangazi Susan huenda akapata mtoto hivi karibuni—nilikuwa na ukubwa kama huo majuma kadhaa kabla hujazaliwa.” Tazamio la kuzaliwa kwa ndugu au dada laweza kuandaa miezi ya mafunzo yenye kusisimua na kuchangamsha.

Baadaye huenda mtoto akauliza: “Mtoto alianzaje kuwako?” Jibu rahisi ni: “Mbegu kutoka kwa baba hukutana na yai ndani ya mama na mtoto huanza kukua, kama vile mbegu katika udongo hukua na kuwa ua au mti.” Katika pindi nyingine huenda mtoto akauliza: “Mbegu ya baba huingiaje ndani ya mama?” Waweza kusema kwa heshima: “Unajua jinsi mvulana ameumbwa. Yeye ana uume. Mama ana mlango mwilini mwake ambao uume huingia sawasawa, na mbegu hiyo inapandwa. Mungu alituumba kwa njia hiyo ili watoto waweze kukua katika mahali pazuri, penye joto hadi wanapokuwa wakubwa vya kutosha kuweza kuishi peke yao. Halafu ndipo mtoto mzuri anapozaliwa!” Unaweza kusema kwa hisi ya mshangao kwa jinsi Mungu alivyopanga mambo hayo vizuri ajabu.b

Unapaswa uwe mwangalifu usiepuke maswali na kusema kwa kuona haya kwamba: “Nitakuambia baadaye utakapokuwa mkubwa vya kutosha.” Hilo laweza kuongeza udadisi wa watoto na hata uwasukume watafute habari kwingineko kutoka kwa vyanzo visivyofaa. Mtoto ambaye ni mkubwa vya kutosha kuweza kuuliza swali hilo ni mkubwa vya kutosha kuweza kupata jibu rahisi na lenye staha. Kukosa kutoa jibu kwaweza kuwavunja moyo watoto wako wasije tena kwako kupata habari.

Mapema Kadiri Gani?

Wazazi wengi wanahisi kwamba watoto wao wanapaswa wapate kuelewa mambo hayo kimsingi angalau kabla hawajaanza shule, ambako huenda watasikia habari isiyo sahihi kutoka kwa watoto wengine.

Babu mmoja alieleza: “Mimi sikuwa nimeuliza maswali yoyote, lakini nilipokuwa na umri wa miaka sita, baba yangu aliamua kwamba ulikuwa wakati wa kueleza mahali watoto walikotoka. Alisema kwamba muungano wa kingono wa mwanamume na mwanamke uwezao kutokeza mtoto ulikuwa wa kawaida kama vile kula, lakini Mungu alisema kwamba hilo lilikuwa kwa watu waliooana tu. Hivyo, kungekuwako mama na baba pia wa kumpenda mtoto na kumtunza.” Babu huyo aliongezea: “Maelezo aliyotoa yalikuwa ya wakati wake. Nilikuwa tayari nimewaona watoto wa umri wa miaka sita wakicheka kuhusu picha zisizo za adili walizochora ambazo sikuzielewa.”

Bila shaka, maelezo kama hayo yapasa yatolewe, si yakiwa mambo ya kuonewa haya, bali yakiwa mambo ya kibinafsi. Unaweza kurudia kusema kwamba ni habari ya kifamilia ambayo haipaswi kutajwa kwa watoto wengine au watu wengine wasio wa familia. Ikiwa mtoto wako anasahau jambo hilo, unaweza kusema kwa upole: “Shhh! Kumbuka, hiyo ni habari ya kipeke yetu. Tunaizungumzia tu kifamilia.”

Si ya Kushtua

Ikiwa umaana wa mazungumzo haya washtua msomaji yeyote, ebu fikiria ni wazazi wangapi wachanga wenye kudhamiria wanaotafuta njia ya heshima ya kuelezea watoto wao mambo hayo. Je! si maelezo ya moja kwa moja katika nyumba yenye upendo ndiyo yanayofaa zaidi kuliko zile njia ambazo wazazi wengi walijifunzia mambo hayo, kutoka kwa vyanzo vibaya visivyo vya kifamilia?

Ukisikiliza kwelikweli na kujibu maswali kwa njia nyepesi na yenye heshima, utaifanya iwe rahisi zaidi kwa watoto wako kuja kwako wakiwa na maswali mengine huku miaka ikisonga na uhitaji wao wa habari ukikua.

[Maelezo ya Chini]

a Kila mtoto huwa tofauti. Hivyo, rejezeo lolote kwa umri katika makala haya limekusudiwa liwe kwa njia ya ujumla tu, ili kuonyesha jinsi mafunzo haya yalivyo ya kuendelea hatua kwa hatua

b Kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha kinazungumzia haya na mambo mengine mengi ya kulea watoto kwa adili na maisha ya familia. Unaweza kukiagiza kutoka kwa watu waliokuletea gazeti hili au kutoka watangazaji wacho kwa anwani zinazopatikana kwenye ukurasa 5.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Unapokaribia kuzaa, fursa ya kutoa maagizo ya thamani hujitokeza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki