Kwa Nini Ulimwengu Mpya Unatazamiwa kwa Hamu Hivyo?
Mwisho wa Ulimwengu—Ni Karibu Kadiri Gani?
MWISHO wa ulimwengu huu unamaanisha nini? Je! ni kuangamizwa kwa dunia kwa moto, kama vile dini nyinginezo hufundisha? La; hilo lingewezekanaje, hali Zaburi 104:5 husema: ‘Haitatikisika milele?’
Jibu linapatikana tunapotazama nyuma karne nyingi kwenye ulimwengu uliotangulia huu. Ulikuwa umekuwa mfisadi na ulikuwa umemwasi Mungu, kwa hiyo “dunia [ulimwengu, NW] ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.” Lakini ulimwengu huo uliotia ndani mbingu na dunia pia, ulipoharibiwa na Furiko la siku za Noa, mbingu na dunia halisi hazikupitilia mbali. Wala mwisho wa ulimwengu huu hautamaanisha uharibifu wa moto wa mbingu za nyota na Dunia sayari.—2 Petro 3:5, 6; Mwanzo 6:1-8.
Nyakati nyingine Biblia hutumia semi “mbingu” na “dunia” kwa njia za ufananisho. “Mbingu” zaweza kutumiwa kumaanisha Shetani, mungu wa ulimwengu huu; watawala wa ulimwengu walio chini ya udhibiti wake; na majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu—wote wakiwa na uvutano wa kishetani juu ya ainabinadamu. (2 Wakorintho 4:4; Waefeso 6:12) “Dunia” hutumiwa mara nyingi kurejezea watu walioko duniani. (Mwanzo 11:1; 1 Wafalme 2:1, 2; 1 Mambo ya Nyakati 16:31; Zaburi 96:1) Ni mbingu na dunia hizo za ufananisho za ulimwengu huu wa saa ulio mwovu ambazo 2 Petro 3:7 husema zitaharibiwa kwa “moto.”—Wagalatia 1:4.
Kisha Petro atoa habari zenye kufurahisha kwamba mahali pa ulimwengu huu wa kale patachukuliwa na mwingine mpya: “Kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki [uadilifu, NW] yakaa ndani yake.”—2 Petro 3:13.
Ulimwengu Mpya Bila Machozi Wala Kifo
Tangazo la Petro kwamba uadilifu ungekuwa katika ulimwengu huo mpya ni habari za kupendeza, lakini yale ambayo Yohana aongeza kuihusu humfanya mtu achachawe mno! Kuhusu hilo yeye husema kwenye Ufunuo 21:3, 4: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”
Badala ya kuharibu dunia kwa moto, Yehova akusudia kwamba ikaliwe milele: “Maana BWANA [Yehova, NW], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa [hakuiumba bure tu, NW], aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
Uadilifu utakaa humo kwa sababu hakuna watu wasio waadilifu watakaokuwako: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.
Chini ya upulizio, mtunga zaburi Daudi pia alitoa ushuhuda wa hilo: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
Yesu mwenyewe athibitisha hilo, akisema katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Heri wenye upole, maana hao watairithi nchi.” Ikiwa serikali yao, hao wapole watabarikiwa na mbingu mpya yenye uadilifu wanayoomba: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 5:5; 6:9, 10.
Amani nyingi ambayo wakazi wa ulimwengu huo mpya watafurahia huenea hata katika ulimwengu wa wanyama: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. . . . Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:6-9.
Karibu Kadiri Gani?
Ikiwa una mbetuko wa kupuuza yote hayo kuwa tumaini lisilowezekana, mambo mazuri zaidi kuweza kuaminika, tua tena na ufikiri. Kwa kuongezea mambo mbalimbali ya ishara ya jumla ya kuwapo kwa Kristo Yesu, kuna kronolojia ya Biblia iliyotaja 1914 kuwa mwanzo wa kuwapo kwake. Mashahidi wa Yehova walitangaza tarehe 1914 kuwa mwaka wa maana katika kusitawishwa kwa utawala wa Ufalme wa Yehova juu ya dunia, wakifanya hivyo katika gazeti Mnara wa Mlinzi wa Julai 1879. Wanahistoria na wachunguzi wengi wa mambo ya ulimwengu wameonelea kwamba mwaka 1914 ulileta kipindi tofauti kabisa na chenye umaana katika historia ya kibinadamu, kama vile sanduku linaloandamana linavyoonyesha.
Tukio jingine ambalo Yesu alitoa linapatikana kwenye Mathayo 24:21, 22: “Kutakuwa-po dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.”
Yesu pia alionyesha kwamba ishara hiyo ya jumla ingekamilishwa wakati wa uhai wa kizazi kilichoona ikianza katika 1914. Kwenye Mathayo 24:32-34, yeye alisema: “Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu; nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.”
Kuona ulimwengu huu wa kale—pamoja na vita, njaa, magonjwa, na vifo vyayo—umekomeshwa kutakuwa jambo la kushangilia. Kuona mahali pao pakichukuliwa na ulimwengu mpya wa Yehova Mungu wenye uadilifu—ukileta mwisho wa maombolezo, kilio, magonjwa, na kifo—kutakuwa sababu ya kusherehekea na kuonea shangwe daima na sifa za milele kwa Yehova Mungu, Muumba Mtukufu na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima.
Taraja hilo likiwa mbele, haishangazi kwamba wengi wana hamu sana kuona ulimwengu mpya wenye uadilifu ukija upesi na kuchukua mahali pa ule wa kale uliojaa vihoro, uhalifu, magonjwa, na vifo! Haishangazi kwamba hamu yao ni kubwa sana hivi kwamba wanaelekea kuweka tarehe za mapema kwa ajili ya kuwasili kwa huo. Hata hivyo, sasa hakuna tu visehemu mbalimbali vya ishara ya kuja kwa ulimwengu huo ili kutushawishi kutoa maonyo bandia. Sasa tunaweza kuona ishara ya jumla iliyo kamili ikifunguka kutoka msingi imara wa kutazamia kwetu kwa hamu kuona mwisho wa ulimwengu huu mwovu na ulimwengu mpya wa Yehova ukichukua mahali pao.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
1914—Mwaka wa Mabadiliko Makubwa Katika Historia
HATA baada ya vita ya ulimwengu ya pili, wengi hurejezea 1914 kuwa mwaka wa mabadiliko makubwa katika historia ya kisasa:
“Kwelikweli ni ule mwaka 1914 badala ya ule wa Hiroshima ndio unaotia alama kipindi cha mabadiliko makubwa katika wakati wetu.”—René Albrecht-Carrié, The Scientific Monthly, Julai 1951.
“Tangu 1914, kila mtu anayejua mielekeo ya ulimwengu amesumbuliwa sana na ule ambao umeonekana kuwa mwendo wenye msiba na ulioamuliwa kimbele kuelekea msiba mkubwa zaidi. Watu wengi wenye kufikiri sana wamefikia maoni ya kwamba hakuna linaloweza kufanywa kuzuia hatua ya kutumbukia katika uharibifu.”—Bertrand Russell, The New York Times Magazine, Septemba 27, 1953.
“Muhula wa kisasa . . . ulianza katika 1914, na hakuna ajuaye utakwisha wakati gani au jinsi gani. . . . Ungeweza kufikia kikomo kwa maangamizi makubwa.”—The Seattle Times, Januari 1, 1959.
“Ulimwengu mzima kwa kweli uliharibika karibu na Vita ya Ulimwengu 1 na bado hatujui sababu. . . . Hali bora zilikuwa zikitazamiwa. Kulikuwa na amani na ufanisi. Kisha kila kitu kikaharibika. Tangu wakati huo tumekuwa katika hali hoi kabisa.”—Dakt. Walker Percy, American Medical News, Novemba 21, 1977.
“Katika 1914 ulimwengu ulipoteza utegemeano ambao umeshindwa kuupata tena tangu wakati huo. . . . Huu umekuwa wakati wenye mchafuko na jeuri isiyo ya kawaida, nje na ndani ya mipaka ya kitaifa.”—The Economist, London, Agosti 4, 1979.
“Kila kitu kingeendelea kuwa bora zaidi na zaidi. Huo ndio ulimwengu nilimozaliwa. . . . Ghafula, bila kutazamiwa, asubuhi moja katika 1914 mambo yote yakakoma.”—Waziri wa serikali ya Uingereza Harold Macmillan, The New York Times, Novemba 23, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Amani nyingi kwa ajili ya wote katika ulimwengu mpya ulioahidiwa