Muziki wa Kisasa—Kuepuka Mitego
WENGINE hubishana juu ya mambo yanayofaa na yasiyofaa ya kukaguliwa kwa muziki wa roki. Wengine hujadiliana juu ya madhara yao kwa vijana. Lakini kama wewe ni Mkristo, mambo hayo ni ya pili kwa lile suala kuu: Muziki waweza kuathirije uhusiano wako na Mungu?
Kiongozi cha Mkristo katika maisha ni Neno la Mungu, Biblia. Ina kanuni zinazohusu kila upande wa maisha, kutia ndani vitumbuizo. Mielekezo ya Biblia huwalinda wale wenye kutii kutokana na mambo yasiyofaa na yenye kudhuru. Isitoshe, kibali cha Mungu kinategemea utii wa Neno lake. Kwa hiyo, kanuni za Neno la Mungu huongoza Mkristo katika kuteua muziki. (Zaburi 43:3; 119:105; 2 Timotheo 3:16, 17) Basi, ni ipi miongozo ya Kimaandiko inayotusaidia kuteua muziki?
Uhitaji wa Usawaziko
Mhubiri 7:16 hutahadharisha: “Usiwe na haki kupita kiasi; wala usijiongezee hekima mno. Kwani kujiangamiza mwenyewe?” Kabla ya kukata kauli kwamba muziki fulani ni mbaya, jiulize mwenyewe kama suala labda ni mapendezi ya binafsi. Kumbuka, huenda usipende muziki fulani, lakini hilo halimaanishi kwamba muziki huo ni mbaya.
Upande mwingine wa usawaziko unaonyeshwa katika Mhubiri 7:17, 18: “Usiwe mwovu kupita kiasi; wala usiwe mpumbavu; kwani ufe kabla ya wakati wako? Ni vizuri kwamba ulishike neno hilo; naam, hata kwa neno hilo tena usiuondoe mkono wako; kwa kuwa mtu yule amchaye Mungu atatoka katika hayo yote.”
Basi, namna gani ikiwa Mkristo asikiliza muziki unaotia moyo ujeuri, ubaguzi wa rangi, ukosefu wa adili, ibada ya Ibilisi, na kujiua? Waefeso 5:3, 4 husema kihususa hivi: “Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru.” Naam, wale wanaotamani urafiki na Yehova hawawezi kufanya mambo yasiyofaa kuwa vitumbuizo vyao. Hawawezi kufikiria kwamba bora tu hawafanyi mambo hayo mabaya, ni sawa tu kuyafurahia.
Si maneno tu yanayofanya wimbo ufae au usifae kwa maoni ya Kimaandiko. wimbo huo unachochea roho gani? Tafadhali soma Wagalatia 5:19 hadi 23 katika Biblia yako. Ni orodha gani inayoeleza vema zaidi roho ya muziki unaosikiliza? Ikiwa muziki huo wafanana na “matendo ya mwili,” basi maoni ya Yehova kuuelekea ni wazi vya kutosha.
Mkristo akijaribu kuchanganya maisha yake ya utumishi mtakatifu kwa Mungu na vitumbuizo vya muziki wenye kupotoka, ataona kwamba mambo hayo mawili hayapatani kabisa. Ni kama kunywa maji ya matunda yaliyochanganywa na sumu. Maji hayo ya matunda hayatazuia sumu isikuue. Maneno yaliyo katika 2 Wakorintho 6:14-17 yanaelewesha wazi jambo hilo: “Msifungwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? . . . Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema Bwana [Yehova, NW], msiguse kitu kilicho kichafu.”
Basi, hayo ndiyo masuala ya Kimaandiko yanayokabili wale wanaotamani kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu. Kama unathamini kanuni za Biblia, basi chunguza kwa makini na kwa uzito muziki unaosikiliza. Pitia kwa uangalifu muziki na vidio zote ambazo unazo. Tupa zile zinazokaidi kanuni za Biblia. Ikiwa una shaka, uzitupe tu. Fanya vivyo hivyo na maonyesho ya muziki ya jukwaani na pia vitu vya kusoma—ondoa chochote ambacho hakistahili kushiriki na uadilifu.
Mwelekeo wa Kutoa Udhuru
Kama unavutiwa na muziki unaokaribia kuwa mbaya au unaovunja kanuni za Biblia, inaweza kuwa vigumu kwako kukabili suala hilo kwa njia ifaayo. Wengine hutoa udhuru katika jitihada ya kutetea msimamo wao usiofaa. Kama jambo hilo ni kweli kwako pia, tua na ufikiri. Je! kufikiri kwako ni timamu, au kunaonyesha tu upendo mwingi mno kwa muziki? Ebu fikiria hoja zinazofuata zinazotolewa na watu wengine na uone kwamba, hoja hizo zikichunguzwa, zinakuwa ni udhuru tu.
Ni sawa nikisikiliza beni hii ya muziki kwa sababu washiriki wayo hupinga matumizi ya dawa za kulevya. Lakini je, washiriki wa beni hiyo hupinga pia kwa njia iyo hiyo matendo mengine mabaya, kama vile uasherati, ujeuri, na kutostahi mamlaka? “Chachu kidogo huchachua donge zima,” husema Wagalatia 5:9.—Linganisha Yakobo 2:10.
Hakuna haki katika maisha ya ulimwengu huu. Je! twaweza kweli kulaumu beni hizo za muziki zikikasirikia hali za ulimwengu? Biblia hutia moyo ghadhabu ya uadilifu dhidi ya maovu ya mfumo huu lakini yaelekeza kwenye Ufalme wa Kimesiya kuwa ndio suluhisho.—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.
Matumaini maangavu ya Mkristo ni tofauti na matazamio mabaya ya wanamuziki wengi wanaoendeleza uasi wa mamlaka kuwa ndio suluhisho kwa taabu za ainabinadamu. Kwa kweli, hasira ya ulimwengu ni yenye uharibifu na ya kinyama, ikionyesha hekima ya mfumo huu wa mambo.—Warumi 12:9; Yakobo 3:15-18.
Wanamuziki hao ni stadi, hata wamepewa mafunzo bora. Lakini ustadi ambao mwanamuziki anatumia hauhusiki na kuchunguza maneno ya muziki kulingana na kanuni za Biblia, ama sivyo? Mfalme Sulemani alikuwa stadi katika mambo mengi, hata katika muziki. Lakini alipoasi ibada ya kweli, Biblia yaripoti, “BWANA [Yehova, NW] akamghadhibikia Sulemani kwa sababu moyo wake umegeuka, naye amemwacha BWANA [Yehova, NW].” Nimrodi vilevile alikuwa mjenzi na mwindaji hodari, lakini yeye na washirika wake hawakupendelewa na Mungu. Kwa nini? Kwa sababu Nimrodi alikuwa “mwindaji hodari katika kupingana na Yehova.”—1 Wafalme 11:9; Mwanzo 10:8, 9, NW.
Nyimbo chache za beni hiyo hazidhuru, zikitia ndani muziki wa roki usio na mdundo mzito. Hatari hapa ni kwamba wimbo mmoja usiodhuru waweza kufanya mmoja anunue na kusikiliza kaseti au rekodi nzima, ambazo zinakuwa na nyimbo nyingi ambazo kwa wazi hazifai. Kama vile kikombe cha maji hakiwezi kuosha matope mengi, wimbo mmoja usio na dhara wa mara kwa mara hauwezi kubadilisha roho ya ujumla ya kaseti au rekodi iliyopotoka au ya beni ya muziki.
Waimbaji hao mashuhuri kwa kweli hawaabudu Shetani wala hawaishi maisha yenye upotovu wa maadili. Wanaiga tu mambo hayo jukwaani. Mambo ya hakika ni kwamba muziki wanaotumia kuwatumbuiza wasikilizaji wao umenyunyiziwa, au kujazwa na ubaya. Wakolosai 3:8 huelekeza Wakristo wasitumbuizwe na vitu kama hasira na usemi mchafu, bali ‘wayaweke mbali.’ Paulo aliwaambia Waefeso ‘wasishirikiane na [wana wa uasi] katika matendo yasiyozaa ya giza, bali kuyakemea.’ Je! mtu yeyote anayetumbuizwa na matendo ya giza aweza kwa kweli kuwakemea wale wanaoyatenda?—Waefeso 5:6, 11.
Sisikilizi maneno. Nasikiliza melodia tu. Lakini maneno yanaweza kuingia katika akili na kutokeza matatizo baadaye. Ingawa tunafikiri habari fulani imetoka akilini mwetu, huenda ikawa haikusahauliwa kabisa. Basi, ni hatari jinsi gani kutaka kujihatarisha kwa ujumbe mbalimbali unaopinga moja kwa moja shauri lililopo katika Wafilipi 4:8, kwamba tukazie akili mambo yaliyo safi, yenye kupendeza, na yenye sifa njema.
Kumbuka pia kwamba yeyote anayetaka ‘kuwa rafiki wa ulimwengu anajiweka kuwa adui ya Mungu.’ Hiyo ni kwa sababu ulimwengu wa ainabinadamu ambao umetengwa na Mungu pamoja na roho ya ulimwengu ni mazao ya Mkinzani mkuu wa Yehova, Shetani Ibilisi. Wazia sasa juu ya jambo hili. Je! mwanamume angefurahi ikiwa mke wake angeonyesha picha ya mpenzi wake wa zamani hata kama angedai kwamba hampendi kikweli na kwamba picha hiyo ni maridadi tu? La, asingependa picha hiyo iwe nyumbani mwake na akilini mwa mke. Namna gani kama tunaingiza nyumbani na mioyoni mwetu muziki unaotumikia makusudi ya Mkinzani wa Yehova? Je! kweli Yehova ataona tofauti tukidai kwamba “Ninapendezwa na melodia tu; siyasikilizi maneno”?—Yakobo 4:4; 1 Wakorintho 10:21, 22.
Amua Mara Moja
Kama umekuwa ukijihatarisha kwa muziki unaokazia matendo mabaya, sababu yako hasa ni nini? Huenda usikubaliane na mawazo maovu, lakini huenda muziki huo ukakuvutia sana—huenda mdundo ukawa wenye kuvutia sana, na wenye kushawishi sana—hivi kwamba huwezi kuuepuka na hutaki kuuacha.
Lakini kufanya yaliyo sawa si rahisi nyakati zote. Tunajaribiwa hasa wakati viwango vya Mungu vinatuelekeza tuache kitu ambacho tunakipenda sana. Je! tutatoa hoja ya kwamba hali yetu ni ya kipekee sana na hivyo tuendelee ‘kusita-sita katikati ya mawazo mawili,’ au tutaamua mara moja tuache mambo ambayo Yehova anachukia?—1 Wafalme 18:21.
Hata tujidhabihu kadiri gani, tutafurahi zaidi kama tutafanya uamuzi unaompendeza Yehova. Hiyo inamaanisha kwamba ni lazima tusishike kitu kichafu. Na tusipokishika, basi Yehova aahidi kwamba atatukubali. Ndiyo, atatuona kuwa mmoja wa watu anaowapendelea.—2 Wakorintho 6:17.
Yehova hufikiria mapendezi yetu bora zaidi. Alifanyiza amri zake ili kufanya maisha yetu kuwa bora zaidi. Itikia sihi yake yenye moyo mweupe inayopatikana katika Isaya 48:17, 18. “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.”
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ikiwa Mkristo husikiliza muziki wenye kupotoka, je! anaweza kwa dhamiri safi kuwashauri wengine dhidi ya muziki huo?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Utafurahi zaidi ikiwa utatupilia mbali vitu ambavyo Yehova anachukia
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Daraka la Wazazi
Kama wewe ni mzazi, una daraka la Kimaandiko la kuwafundisha watoto wako kufahamu tofauti kati ya muziki mzuri na mbaya. Hiyo inamaanisha kwamba ufahamu muziki wanaosikiliza. Inamaanisha kwamba unakuwa thabiti kwa aina ya muziki utakaoruhusu na ambayo hutauruhusu nyumbani.
Toa sababu na watoto wako. Epuka mabishano yanayodhoofisha sababu zako. Maneno kama, “Sielewi ni kwa nini unasikiliza uchafu huo,” yaelekea yatafanya watoto washikilie hata zaidi mapendezi yao binafsi ya muziki. Kuelekeza kwenye mtindo wa kibinafsi wa maisha yaliyopotoka ya mwanamuziki kunaweza vilevile kukosa kufaulu, hasa ikiwa mtindo huo wa maisha hauonyeshwi katika muziki. Kijana mmoja alisema hivi: “Mtu akisema kwamba muziki wote wa rapu ni mbaya, ninafikiri yeye hajui tu!”
Hivyo pata habari zaidi. Jifunze maoni ya Mungu juu ya mambo hayo. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kwa kukupa vichapo vyenye msingi wa Biblia vinavyoongea juu ya mambo hayo kindani. Pata kujua mambo ya hakika. Ueleweshe wazi kwamba suala ni viwango vya Biblia wala si kuwawekea watoto wako mapendezi yako ya binafsi.—Waefeso 6:4.