Vijana Wanauliza...
Naweza Kukabilianaje na Ulemavu Wangu?
“BADO anaweza kutembea,” asema mama ya msichana mchanga ambaye tutamwita Maggie. “Lakini mwili wake haufanyi kazi kwa upatano, na usemi wake si dhahiri.” Maggie anaugua ugonjwa wa kushupaa kwa mishipa na yeye ni mmoja wa mamilioni ya vijana ulimwenguni wanaougua ulemavu wa kimwili.
Labda wewe ni mmoja wao. Na hata kama ulizaliwa na ulemavu au uliupata kutokana na ugonjwa au aksidenti,a hakuna haja ya kuamua kwamba huwezi kuwa na maisha yenye furaha na yenye utendaji. Ukiweka jitihada yenye subira, unaweza kuchukua hatua zifaazo za kukabiliana na hali yako.
Mtego wa Mawazo ya Kutamani
Bila shaka, ni asili ya kibinadamu kutotaka kukubali jambo halisi lisilopendeza bali kutamani kwamba ulemavu huo utaondoka wenyewe tu. Inaonekana kwamba mtume Paulo aliugua aina fulani ya ugonjwa ulioathiri macho yake. (Linganisha Wagalatia 6:11.) Akirejezea ziara yake ya kwanza kwa Wakristo katika Galatia, Paulo alisema hivi: “Naliwahubiri injili mara ya kwanza kwa sababu ya udhaifu wa mwili; na jaribu lililowapata katika mwili wangu hamkulidharau wala kulikataa.” (Wagalatia 4:13, 14) Wasomi wengine hufikiria kwamba ugonjwa wa Paulo ulifanya macho yake yatokeze usaha au ulifanya sura yake ionekane yenye kuchukiza kwa njia fulani. Basi, haishangazi kwamba Paulo ‘alimsihi Bwana mara tatu’ kwamba ugonjwa huo umtoke. Lakini haukutoka. (2 Wakorintho 12:8, 9) Ingawa hivyo, ajapokuwa na ulemavu, alifurahia kazi-maisha yenye kutokeza ya umishonari, ya usomi, na ya uandikaji.
Huenda wewe pia ukahitaji kukubali kwamba ulemavu wako ni wa kudumu. Katika kitabu Living With the Disabled, mwandikaji Jan Coombs aandika hivi: “Ili mgonjwa azoee ulemavu wake ni lazima akubali kwanza kwamba yeye ni mlemavu. Ni lazima ajifunze kwamba kizuizi chake kinaweza kupunguza utendaji wake na kumsumbua lakini hakimshushi hali akiwa mtu.” Kama hakuna tumaini la kweli la ponyo, kukana hali yako kutakuingiza tu katika hali ya kujilaumu, huzuni, na kukata tamaa. Kwa upande mwingine, “hekima hukaa na wanyenyekevu,” yasema Biblia katika Mithali 11:2, na mtu mwenye kiasi anajua na anakubali vizuizi vyake. Hiyo haimaanishi kwamba ujitenge au kuamua kuishi maisha yenye maudhiko yasiyo na furaha. Badala ya hivyo, kiasi kunatia ndani kuchunguza hali yako kwa unyoofu na kujiwekea miradi halisi.
Tenda kwa Ujuzi
Unahitaji kujua kwa usahihi asili ya ulemavu wako. “Kila aliye na busara hutenda kazi kwa maarifa,” chasema Mithali 13:16. (Linganisha Mithali 10:14.) Hiyo yaweza kumaanisha kusoma vichapo vya kitiba au kuuliza daktari wako na matabibu wengine wowote wanaokutibu maswali hususa. Kujielimisha kwa habari hiyo kwaweza kukuondolea mawazo yoyote ya kimakosa yanayoweza kukuzuia usifanye utendaji zaidi.
Kunaweza kusaidia pia kujua maendeleo ya kitiba na utibabu unaoweza kufanya hali yako kuwa bora zaidi. Kwa mfano, viungo bandia vinavyofanyizwa kwa vifaa vipya visivyo vizito na ambavyo vinakupa ustarehe zaidi na uwezo kufanya mambo kwa urahisi zaidi vimetengenezwa. Kwa kweli, gazeti Time laripoti “ongezeko kubwa la ghafula” la vitu vya kuwasaidia watu wenye ulemavu. Labda vitu hivyo vinapatikana kwenu na familia yako yaweza kuvigharimia.
Vitu vingine vya kawaida zaidi, kama visaidizi vya kusikia, fimbo, mikongojo, na magango ya kutegemeza viungo dhaifu vinaweza kufaa sana. Sasa, vijana wengine huenda wakaona haya sana na kujihisi ovyo wakitumia vitu hivyo vyenye kusaidia. Lakini Mfalme Sulemani alionelea hivi kwa hekima: “Shoka yako ikisenea na ukose kuitia makali, ni lazima ufanye kazi kwa bidii zaidi ukiitumia.” (Mhubiri 10:10; Today’s English Version) Wewe nawe unaweza kujichosha—au kuepuka utendaji wenye kufurahisha—ukikosa kutumia vizuri vyombo vinavyoweza kukusaidia. Kwa nini uache kiburi kikusababishe ufanye maisha yako kuwa magumu zaidi? Sulemani alimalizia kwa kusema: “Yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa.”
Naam, ni mafaa kwako kutumia kitu ambacho kitakusaidia kutembea, kuona, au kusikia kwa njia bora zaidi. Ni kweli, inaweza kuchukua mazoezi mengi na saburi nyingi ili kuweza kutumia kwa njia nzuri mkongojo, viungo bandia, au visaidizi vya kusikia. Na vyombo hivyo huenda yasifanye uonekane vizuri zaidi. Lakini fikiria uhuru zaidi ambao vinaweza kukupa na fursa ambazo vinaweza kukufungulia! Msichana mmoja mwafrika mwenye ulemavu anayeitwa Jay aliishi maisha ya upweke, akitoka nje ya ua ya mahali alipoishi mara moja tu katika miaka yake 18. Baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hiyo ilimbidi “atembee” akipita nyumba kadhaa, akienda kwa mikono yake ya mbele na kukokota mwili wake mzima. Shahidi mmoja katika Ulaya alipopata kujua shida ya Jay, alimpelekea kigari cha kusukumwa chenye magurudumu matatu. Kigari hicho kililetwa kikiwa na mnyororo wa kukiendesha ambao Jay angeweza kuendesha kwa mikono yake. Je! hiyo ilimfanya aonekane mzuri? Hapana. Lakini namna hiyo ya usafiri iliyoonekana kuwa haifai ilimsaidia kwenda mikutanoni na kushiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba.
Jiwekee Miradi!
Hata hivyo, ujihadhari usije ukasitawisha mtazamo wa akili usiofaa! Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; naye ayatazamaye mawingu hatavuna.” (Mhubiri 11:4) Je! unaruhusu woga au kutokuwa na uhakika kukuzuie usifanye mambo unayotaka na unayohitaji kufanya? Fikiria Musa. Mungu alipomchagua aokoe Waisraeli kutoka utumwani katika Misri, Musa alijaribu kutoa udhuru kwa sababu ya kuwa na tatizo la usemi. ‘Mimi nina midomo isiyo tohara,’ akasema Musa, labda jambo hilo likionyesha kwamba alikuwa na ulemavu fulani uliofanya asiseme kwa udhahiri. (Kutoka 6:12) Lakini Musa alikuwa akijishusha hali. Baada ya muda, alithibitisha kwamba aliweza kusema kwa ufasaha—akihutubia taifa zima la Israeli.—Kumbukumbu la Torati 1:1.
Usifanye kosa lilo hilo la kujishusha hali. Jisukume na ujiwekee miradi! Kwa mfano, Becky mchanga ana matatizo ya kusema kwa sababu ya aksidenti aliyopata akiwa na miaka mitano. Lakini wazazi wake hawakumruhusu akate tamaa. Badala ya kufanya hivyo, walimwandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Alipofikia umri wa miaka saba, Becky alikuwa akitoa hotuba fupi mbele ya wasikilizaji. Becky akumbuka: “Kutoa hotuba kulisaidia. Kulinichochea nijitahidi zaidi katika usemi wangu.” Becky alihimizwa pia ashiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri nyu-mba kwa nyumba. “Nyakati nyingine mimi hufikiri watu huchukia sana kunisikiliza nikiongea; mimi huhangaika juu ya yale wanayofikiri. Lakini ndipo mimi hujiambia, ‘Ninafanya hili kwa ajili ya Yehova,’ kisha namwomba anisaidie nishinde hisia hizo.” Leo, Becky anatumikia akiwa mweneza evanjeli wa wakati wote.
Craig, ambaye sasa ni mtu mzima, anaugua ugonjwa wa kupooza ubongo. Yeye pia amekataa kuruhusu ulemavu wake umzuie asiwe mshiriki wa kundi la Kikristo anayethaminiwa. Yeye asema: “Ninamtegemea Yehova, na ameniruhusu nifurahie baraka zake nyingi. Nimeweza kutumikia nikiwa painia msaidizi [mweneza evanjeli] mara tano. Ninatoa hotuba za Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na ninaweza kushughulikia hesabu ya kundi.”
Kuna “wakati wa kucheka” pia, na kwa mazoezi ya kadiri fulani, huenda hata ukaweza kufurahia baadhi ya utendaji wenye kufurahisha ambao vijana wengine hufurahia. (Mhubiri 3:4) Becky akiri hivi: “Siwezi kucheza michezo kama voliboli kwa sababu mwili wangu huitikia polepole sana. Lakini ninaweza kukimbia. Na muda mfupi baada ya aksidenti, mama yangu alinitia moyo nijifunze kuendesha baiskeli. Nyakati zote alinitia moyo nijaribu kufanya mambo mapya.”
Usijaribu Kukabiliana Peke Yako
Kukabiliana na ulemavu wa kimwili si rahisi. Mtume Paulo aliuita ulemavu wake “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Kwa uzuri, si lazima ukabili matatizo yako peke yako. Sarne, mwanamke mchanga mwenye ulemavu wa nyonga moja, asema hivi: “Ninaona kwamba kuwa na ushirika unaofaa wa Kikristo na utegemezo wenye upendo kutoka kwa familia na kutoka kwa marafiki kundini kumenisaidia sana.” Ndiyo, usijitenge. (Mithali 18:1) Kwa kadiri iwezekanavyo, uwe na ‘mengi sana katika kutenda kazi ya Bwana sikuzote.’ (1 Wakorintho 15:58) Sarne aeleza manufaa zinazotokea: “Kuwa mtendaji katika miradi ya Ufalme kunanisaidia niwe na maoni yanayofaa juu ya matatizo yangu.” Becky aonelea hivi: “Unapata kuongea na watu ambao hali yao ni mbaya zaidi kuliko yako kwa sababu hawana tumaini la wakati ujao. Hiyo inanisaidia nisahau matatizo yangu.”
Zaidi ya yote, mwendee Yehova Mungu kwa ajili ya utegemezo. Yeye anaelewa mahitaji yako na hisi zako na hata anaweza kukuandalia “adhama kuu ya uwezo” ili ukabiliane na hali. (2 Wakorintho 4:7) Labda baada ya muda unaweza kuwa na maoni mazuri kama ya kijana Mkristo ambaye ni mlemavu anayeitwa Terrence. Akiwa na umri wa miaka tisa, Terrence alipoteza uwezo wake wa kuona lakini alikataa kuacha jambo hilo limshinde, akisema: “Upofu wangu si kizuizi; ni usumbufu tu.”
[Maelezo ya Chini]
a Kama ulilemaa hivi karibuni tu, kwa kueleweka huenda ikawa unakabili hisi za uchungu, hasira, na huzuni. Kwa kweli, hilo ni jambo la kawaida kabisa—na linafaa—kupitia wakati wa huzuni ikiwa umepatwa na potezo kubwa. (Linganisha Waamuzi 11:37; Mhubiri 7:1-3.) Uwe na hakika kwamba baada ya muda fulani na utegemezo wenye upendo wa familia na marafiki, hisi nyingi za uchungu zitapunguka hatimaye.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Jifunze kadiri uwezavyo juu ya ulemavu wakoy