Ulimwengu Bila Maradhi
“Malaria ni mjanja kuliko vile kila mtu alivyofikiri,” asema mstadi wa kinga ya mwili Dakt. Dan Gordon. “Bado tunajaribu kuishinda.”[1]
“BADO hatujui mambo mengi kuhusu mabadiliko ya kikemikali ya [bakteria ya kifua-kikuu],” asema Barry Bloom wa Taasisi ya Kitiba ya Howard Hughes. “Hatujui kabisa jinsi dawa yoyote ifanyavyo kazi. Hatujui kabisa.”[2]
“Kuwa na ujuzi hakumaanishi kubadili tabia,” aomboleza msemaji wa Vituo vya Kudhibiti Maradhi, akifikiria kushindwa kwa zile kampeni za “ngono salama” za kumaliza kaswende.[3] Kama vile taarifa hizo zionyeshavyo, vita dhidi ya malaria, kifua-kikuu, na kaswende vimekuwa vyenye kufadhaisha sana. Je! wakati ujao utaleta ponyo bora zaidi kwa maradhi hayo?
Labda. Ingawa binadamu aweza kushinda magonjwa fulani na kufanya mengine yawe rahisi zaidi kuishi nayo, kuna sababu ya msingi inayofanya asiweze kushinda kabisa vita dhidi ya maradhi.
Chanzo cha Maradhi
Vita dhidi ya maradhi ni zaidi ya kupigana tu na vimelea na vijidudu. Biblia yaeleza kwamba maradhi ni tokeo la dhambi iliyoridhiwa kutoka kwa baba wa kwanza wa binadamu. (Warumi 5:12) Dhambi haikuharibu tu uhusiano wa mwanadamu pamoja na Muumba wake bali pia iliongoza kwenye kuzoroteka kwake kiakili, kihisia-moyo, na kimwili. Hivyo, badala ya kuendelea kuishi kwa ukamilifu katika dunia-paradiso, wanadamu wakawa wasiokamilika na kuzoroteka mpaka kifo kilipowapata.—Mwanzo 3:17-19.
Hata akiwa na dawa bora zaidi, mwanadamu hawezi kubadili hali yake ya dhambi wala matokeo yayo. Hali hiyo ngumu yaacha jamii ya kibinadamu ikiwa ‘imetiishwa chini ya ubatili [“haina uwezo wowote,” Phillips].’ (Warumi 8:20) Na ndivyo ilivyo kwa habari ya kushinda maradhi. Maendeleo yenye kuokoa uhai katika uwanja wa tiba mara nyingi hurudishwa nyuma kwa kuvunjika kwa jamii kwenye kutisha uhai.
“Twajikuta katika hali ngumu,” aandika Jerold M. Lowenstein katika gazeti Discover. “Kadiri tupatavyo mafanikio zaidi katika kupigana na maradhi na kurefusha uhai wa kibinadamu, ndivyo uwezekano wa kuharakisha uangamizo wetu unavyoongezeka” kwa sababu ya idadi kubwa ya watu kupita kiasi na kuharibiwa kwa mazingira.[4]
Ponyo Kamili
Ponyo kamili kwa maradhi halimo na mwanadamu bali limo na Muumba. Hiyo ndiyo sababu mtunga-zaburi alitangaza hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” Biblia yaendelea kusema hivi: “Heri ambaye . . . tumaini lake ni kwa BWANA [Yehova, New World Translation], Mungu wake. Aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zaburi 146:3, 5, 6) Ni Mungu pekee ndiye mwenye uwezo wa kuondoa ugonjwa kutoka kwenye chanzo chao. Na kulingana na Biblia, yeye akusudia kufanya hivyo. Wakati huo unakaribia.
Yesu Kristo alitabiri kwamba “magonjwa ya kipuku” yangekuwa mojayapo mathibitisho mengi kwamba twaishi katika umalizio wa mfumo uliopo wa mambo na kabla tu ya kuingia kwa ulimwengu mpya. Alitabiri pia juu ya ongezeko la hali zilezile zenye kuongeza maradhi, kama vile vita, njaa kubwa, na uasi wa sheria.—Luka 21:11; Mathayo 24:3, 7, 12; 2 Timotheo 3:1-5, 13.
Alipokuwa duniani, Yesu aliponya wagonjwa kimuujiza, hivyo akianza utimizo wa unabii huu: “Ameyachukua masikitiko [magonjwa, NW] yetu, amejitwika huzuni zetu.” (Isaya 53:4; Mathayo 8:17) Kwa kufanya hivyo alionyesha kwa kiwango kidogo mambo ambayo Mungu amekusudia kutimiza hivi karibuni ulimwenguni pote. Biblia yasema hivi kuhusu Yesu: “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; hata ule mkutano wakastaajabu, walipowaona mabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanakwenda, na vipofu wanaona.”—Mathayo 15:30, 31.
Watu walioona miujiza hiyo walimtukuza Mungu kwa sababu walielewa kwamba ilikuwa ni yeye aliyempa Yesu uwezo wa kuifanya miujiza hiyo. Uwezo ambao Yesu alitumia ulikuwa uwezo uleule uliotumiwa katika kuumba ulimwengu wetu wote mzima wenye kustaajabisha. Ilikuwa ni roho takatifu ya Mungu, kani yake ya utendaji.—Mwanzo 1:1, 2; Ufunuo 4:11.
Nabii Isaya aliandika juu ya wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Na Ufunuo 21:4, 5 hutangaza hivi: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita. Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, tazama, nayafanya yote kuwa mapya.”
Biblia yaonyesha kwamba twaishi katika wakati wa badiliko. (1 Yohana 2:15-17) Hivi karibuni ulimwengu huu, pamoja na magonjwa, huzuni, uhalifu, ujeuri, na kifo, utakuwa umekwisha kupita. Mungu atauondoa pamoja na misiba yao yote, ukitokeza njia kwa ajili ya ulimwengu mpya hapa duniani, ambamo “haki yakaa ndani yake.” (2 Petro 3:11-13) Yesu alirejezea ulimwengu huo mpya unaokuja kuwa “Paradiso,” kwa kuwa utakuwa kama ile Paradiso ya awali ya bustani ya Edeni, lakini ukiwa wa duniani pote.—Luka 23:43; Mwanzo 2:7, 8.
Kwa hiyo, Wakristo wana tumaini, si kwa ajili ya tiba ya muda mfupi tu, bali kwa kuwekwa huru daima kutokana na kutokamilika, maradhi, na kifo. Wanatazamia mbele kwenye utimizo kamili wa ahadi hii ya Mungu: “Mimi ndimi BWANA [Yehova, NW] nikuponyaye.” “Nami nitakuondolea ugonjwa kati yako.”—Kutoka 15:26; 23:25.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Yesu alipewa uwezo na Mungu afufue wafu na kuponya wagonjwa