Vijana Huuliza...
Ni Nani Awezaye Kunisaidia Kusuluhisha Matatizo Yangu?
“MWANADAMU huzaliwa ili apate mashaka.” Akasema hivyo mtu mmoja mwenye msononeko aliyeitwa Ayubu miaka ipatayo elfu nne iliyopita. (Ayubu 5:7) Labda maisha yako si yenye msiba kama ya Ayubu. Lakini bila shaka una matatizo na magumu mengi.
Kikundi kimoja cha vijana Waamerika kilipoulizwa, “Ni kitu gani huwasumbua zaidi?” wengi walijibu kwamba shule, wazazi, fedha, marafiki, na ndugu au dada zao ni vyanzo vya hangaiko lao.[1] Vipi wewe? Je! wakabiliwa na msongo wa marika, mahangaiko ya fedha, au matatizo ya shule? Je! wewe huona ugumu wa kukabiliana na hali za kihisia-moyo zenye kubadilika-badilika za ubalehe? Je! una mahangaiko juu ya wakati ujao wako?
Ukifikiria matatizo hayo yote inakuwa rahisi kulemewa na kushuka moyo. Kwa kweli, ukiyaweka mahangaiko hayo bila kueleza wengine, waweza kujikuta ukiwa umejitenga na wengine kihisia-moyo. (Linganisha Mithali 18:1.) Basi, wapaswa kushughulikiaje matatizo yako binafsi? Je! kwa kweli wapaswa kuyakabili peke yako?
La, kwa sababu matatizo yako—hata yaonekane kuwa makubwa kadiri gani—si ya kipekee. Baada ya kuchunguza kwa uangalifu tabia ya kibinadamu, Mfalme Sulemani mwenye hekima alikata kauli kwamba “jambo jipya hakuna chini ya jua.” (Mhubiri 1:9) Naam, wengine wamekabili na kusuluhisha kwa mafanikio matatizo kama yako. Kwa hiyo si lazima ujaribu kusuluhisha matatizo peke yako; nyakati nyingine waweza kupata msaada kutoka kwa mtu ambaye tayari amesuluhisha yake. Kwa vyovyote ukisafiri kwenda mahali usipopajua, je, usingalijaribu kujua namna ya kwenda kwa kumwuliza mtu ambaye tayari alikwisha kwenda huko? Swali ni hili, Wapaswa kumwendea nani ili upate msaada kama huo?
Marika—Chanzo Bora Zaidi cha Kupata Shauri?
Vijana wengi huchagua kueleza marika wao matatizo yao. “Nyakati nyingine mimi hufikiri kwamba matatizo fulani ninayopata ni ya kipekee,” aeleza Anita mchanga. “Nahisi, ‘Je! kuna mwingine yeyote anayepitia matatizo haya?’ Najiuliza kama mimi ni mjinga kufikiri hivyo.” [2] Waweza kuhisi kwamba mtu wa rika lako aweza kuelewa hisia zako na kwamba mtu mzima—hasa mzazi—aweza kuwa mwenye kuhukumu zaidi, au mwenye kuchambua zaidi.
Na ingawa marika wako huenda wakaelewa, wawe na hisia-mwenzi na wakuhurumie, huenda wasiweze kutoa shauri jema nyakati zote. Kama Biblia ielezavyo, ‘watu wazima wana akili zilizozoezwa kupambanua mema na mabaya.’ Kwa njia gani? Biblia yajibu hivi: “Kwa matumizi ya muda mrefu,” yaani maarifa! (Waebrania 5:14; The New English Bible) Wakiwa hawana maarifa kama hayo, mara nyingi vijana hawajasitawisha “hekima kamili na busara” kwa kiwango cha utu mzima. (Mithali 3:21) Kwa hiyo ni hatari kufuata shauri la kijana mwenzako. Mithali 11:14 (NW) laonya hivi: “Pasipo mwongozo wenye ustadi, watu huanguka.”
Thamani ya Wazazi Wanaomhofu Mungu
Kwa ujumla watu wazima huwa katika hali bora zaidi ya kuandaa mwelekezo wenye ustadi. Ayubu mwadilifu anataja jambo hilo hivi: “Wazee ndio walio na hekima, na katika kuishi siku nyingi iko fahamu.” (Ayubu 12:12) Yaelekea kwamba wazazi wako wenye kumhofu Mungu ndio wastahilio zaidi ya wote kukusaidia katika jambo hili. Kwanza, wao wanakujua kuliko akujuavyo mtu yeyote. Wakiwa wamekabili baadhi ya hali hizo unazokabili sasa, waweza kukusaidia sana uepuke matatizo. Akisema akiwa mzazi, Sulemani alishauri hivi: “Wanangu, yasikilizeni mausia ya baba yenu, tegeni masikio mpate kujua ufahamu. Kwa kuwa nawapa mafundisho mazuri; msiiache sheria yangu.”—Mithali 4:1, 2.
Fikiria kijana mmoja Mghana aitwaye Samuel. Alipokuwa katika shule ya sekondari, ilimbidi aamue kati ya kufuatia elimu ya kilimwengu ama kufuatia kazi-maisha akiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. “Kwa vile familia yetu ilikaribiana sana kwa mawasiliano mazuri,” yeye aeleza, “ilikuwa rahisi kuongea na wazazi wangu.” Wazazi wa Samuel walimwelekeza kwenye upande wa huduma ya wakati wote—kazi maisha ambayo bado aendelea nayo vizuri. Samuel apendekeza kwamba vijana wahusishe wazazi wao katika kusuluhisha matatizo ya kibinafsi kwa sababu “wao wana maarifa zaidi maishani na huenda waliyakabili matatizo ayo hayo . . . na wako katika hali bora zaidi ya kukupa wewe mwono wa wazi juu ya pande zote mbili za suala hilo.”[3]
Kwa kupendeza, kulingana na uchunguzi wa hivi karibuni wa Gallup, idadi kubwa ya vijana hutaka mwelekezo wa wazazi—hata katika masuala kama dawa za kulevya, shule, na ngono.[4]
‘Wao Hawanielewi!’
Hata hivyo, inasikitisha kwamba vijana wengi hujitenga na wazazi wao wanapofikia miaka yao ya utineja. Baadhi yao huhisi kama mvulana mmoja tineja aliyesema hivi: “Nimejaribu kuongea na wazazi wangu jinsi nilivyo na wasiwasi juu ya maksi zangu na nafikiri shule hii ni ngumu sana, lakini wao huniambia tu kwamba mimi ni mvivu na napaswa kujifunza zaidi.”[5] Msichana mmoja mchanga ambaye ni Mkristo katika Afrika alionyesha hangaiko kama hilo, aliposema hivi: “Ndani yangu, najua kwamba nina matatizo ya kibinafsi ambayo nahitaji msaada, lakini naogopa kwamba wazazi wangu hawatanielewa.”[6]
Bila shaka hata wazazi wenye kumhofu Mungu hupungukiwa nyakati fulani. Wao waweza kuitikia mambo kwa njia ya kupita kiasi, wakose kusikiliza, wakuelewe vibaya, au wawe wenye kuhukumu-hukumu. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba uwapuuze kabisa maishani mwako. Yesu Kristo alilelewa na wazazi ambao hawakuwa wakamilifu. Lakini, Biblia yaonyesha kwamba Yesu “alikuwa akiwatii.” Bila shaka uvutano wao ulimsaidia ‘aendelee katika hekima, akimpendeza Mungu na wanadamu.’—Luka 2:51, 52.
Je! unanufaika kutokana na hekima na maarifa ya wazazi wako wenyewe? Kama sivyo, fikiria jambo lisemwalo katika kitabu Adolescence, cha Eastwood Atwater: “Matineja wanapovutiwa isivyofaa na marika wao, yawezekana zaidi kwamba kuna kitu kinachokosa katika ule uhusiano wa kati ya mzazi na tineja kuliko sababu ya ule uvutio mkubwa zaidi wa marika wao.”[7] Wewe una uhusiano wa aina gani pamoja na wazazi wako? (Wagalatia 6:5) Je! yaweza kuwa kwamba umeepuka kuwasiliana nao karibuni? Basi kwa nini usifanye yote uwezayo ili kufanya mambo kuwa bora zaidi?a Hiyo ni sehemu ya kile Sulemani alichoita “mwana halisi” au binti halisi kwa wazazi wako.—Mithali 4:3, NW.
Malcolm, ambaye ni kijana Mghana aishiye sasa katika United States, alifikiria wakati fulani kwamba wazazi wake hawakuelewa hisia zake. Lakini wao walidumu katika kumpa yeye maono yao maishani na nidhamu ya Neno la Mungu. Katika barua moja ya karibuni aliyopelekea wazazi wake, Malcolm aliandika hivi: “Najua kwamba tumekuwa na tofauti zetu katika wakati uliopita. Lakini nikikumbuka, nastaajabia sana jinsi mlivyovumilia utundu wangu na kukubali kwa utulivu baadhi ya maamuzi niliyofanya maishani. Amini nawaambia, najua mambo yatendekayo katika nyumba nyinginezo, na kwa kweli Biblia ilitokeza tofauti [kwetu]. Asanteni tena.”[8]
Pata Hekima Itumikayo Wewe Mwenyewe!
Kukubali mwongozo wa wazazi wako hakukandimizi ukuzi wako bali kwaweza kuwa njia ya haraka zaidi ya kufikia utu mzima wenye ukomavu. Baada ya muda wewe pia waweza kusitawisha ‘werevu, maarifa, na hadhari.’ (Mithali 1:4) Utakuwa na uwezo wa kuchanganua matatizo na kufanya maamuzi yafaayo juu ya jinsi ya kuyasuluhisha.
Ni kweli kwamba si vijana wote wamebarikiwa kuwa na wazazi wanaomhofu Mungu. Lakini ingekuwa ni kosa kukata kauli kwamba hutasikiliza sana wanayosema wazazi wako eti kwa sababu tu wao si Wakristo. Bado wao ni wazazi wako, na wapaswa kuheshimiwa wakiwa wazazi. (Waefeso 6:1-3) Isitoshe, ukiwapa nafasi, waweza kugundua kwamba wana mengi ya kukupa kwa namna ya mashauri yenye kutumika. Uhitajipo mwelekezo wa kiroho, jaribu kusema na mshiriki anayetumainiwa wa kutaniko la Kikristo. Haitakuwa vigumu kumpata humo mtu mzima mwenye kumhofu Mungu atakayesikiliza vizuri, kwa moyo wenye kuelewa na huruma.
Kumbuka vilevile kwamba roho ya Yehova ni chanzo cha msaada kilichotayari nyakati zote kuandaa nguvu kwa wale wanaouliza. (Luka 11:13) Yehova ameandaa pia habari nyingi sana unazoweza kupata katika Biblia na katika vichapo vyenye kutegemea Biblia vya Watch Tower Society. Kwani, mfululizo uu huu wa vijana umesaidia maelfu ya vijana wapate majibu yatumikayo kwa ajili ya matatizo yao! Kwa kujifunza kuchimba na kufanya utafiti, waweza kusuluhisha matatizo mengi peke yako.—Mithali 2:4.
Bila shaka, kupata matatizo ni sehemu ya maisha. Lakini inasaidia kuwa na maoni yafaayo ambayo mtunga-zaburi alikuwa nayo. Aliandika hivi: “Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, nipate kujifunza amri zako.” (Zaburi 119:71) Naam, kusuluhisha matatizo kwaweza kukubadili na kukuzoeza. Lakini si lazima uyakabili peke yako. Tafuta msaada. Mara nyingi utaupata kwa kuuliza tu.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa madokezo kadhaa kuhusiana na hayo, ona sura 2 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kukubali mwongozo wa wazazi kwaweza kuwa njia ya haraka zaidi ya kufikia utu mzima wenye ukomavu