Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 10/22 kur. 23-25
  • Je, Safari za Matembezi ya Darasa Zinafaa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Safari za Matembezi ya Darasa Zinafaa?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuihesabu Gharama
  • Kumpendeza Mungu Kikamili
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1995
  • Safari za Kwenda Yerusalemu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Safari za Kwenda Yerusalemu
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Familia ya Yesu Yasafiri Kwenda Yerusalemu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 10/22 kur. 23-25

Vijana Huuliza. . .

Je, Safari za Matembezi ya Darasa Zinafaa?

“WAPATA wakati wa pumziko kutoka shuleni.” “Waona kitu kipya cha mazingira tofauti.” ”Wapata kuwajua wanadarasa wenzako vizuri zaidi.”

Hivyo ndivyo vijana watatu Wajerumani walivyoeleza ni kwa nini wao hufurahia safari za matembezi ya darasa. Safari hizo hupendwa sana na vijana ulimwenguni pote.

Hata hivyo, si wanafunzi tu wathaminio sana safari za matembezi ya darasa. “Safari ya matembezi ya darasa iliyopangwa vizuri hunufaisha kijana kwelikweli, ikipanua maoni yake na kumsaidia aweze kujitegemea mwenyewe,” adai mwalimu mmoja. “Tena, uhusiano kati ya mwalimu na darasa hutiwa nguvu.” Hakuna shaka kwamba walimu wenye kudhamiria kazi yao na darasa lenye tabia njema waweza kuungana kufanya safari ya matembezi ya darasa iwe ya kuelimisha na kufurahisha zaidi.

Hata hivyo, huenda kukawa na mambo kadhaa yapasayo kuhangaisha vijana na wazazi Wakristo. Kwa kielelezo, katika Ujerumani na mabara mengine ya Ulaya, wanafunzi wa jinsia zote mbili husafiri pamoja kishirika katika safari ndefu za matembezi ya darasa. Mara nyingi hii huhusisha kulala siku kadhaa mbali na nyumbani. Mara nyingi mno hii humaanisha matata. Anna-Laura mwenye miaka 14 akumbuka hivi: “Baada ya siku chache za safari, mambo yaliruka mipaka. Hata usiku hatukupata amani na utulivu. Walio wengi darasani walijiendesha kwa ubinafsi na bila ufikirio.”

Basi, ufanye nini ukipewa fursa ya kwenda safari ya matembezi ya darasa?

Kuihesabu Gharama

Kwenye Luka 14:28, Yesu Kristo alisema hivi: “Ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia?” Kabla wewe na wazazi wako hamjaamua kama inafaa uende safari ya matembezi ya darasa, yachunguze kwa uangalifu yote yahusikayo. Haya ni baadhi ya maswali ya kufikiria:

Safari hiyo itakupeleka wapi? Kungeweza kuwa na tofauti kubwa kama safari hiyo ni ya kuzuru jengo la hifadhi mchana mmoja au ni safari ndefu zaidi ya kulala nje siku kadhaa. Kwa kuongezea, ikiwa wazazi wako ndio wanaoilipia, watataka kuamua kama wataweza kuigharimia.

Ni nini kilicho katika programu? Ikiwa kila siku imepangiwa vizuri utendaji ufaao na wa kupendeza, hii itashughulisha darasa na kupunguza hatari ya kufanya kosa fulani. Kwa hiyo itazame sana ratiba ya programu kabla ya kuamua juu ya safari ya darasa. Kuzuru majengo ya hifadhi au kwenda safari ya matembezi ya kuchunguza asili za maumbile huenda kukaelimisha. Lakini kujaribu kuonja dini za Yoga na za Kiasia—kama ilivyopangiwa safari ya matembezi ya darasa moja—hakumfai Mkristo kamwe.—1 Wakorintho 10:21.

Je, kutakuwa na usimamizi wenye matokeo mazuri na wa daima? Msichana Mkristo wa miaka 15 aitwaye Julia akumbuka hivi: “Mimi nilikuwa katika darasa lenye tabia njema sana, kwa hiyo Mama na Baba hawakujali kujiunga kwangu na safari hiyo. Walimu walituchunga kwa uangalifu sana.” Lakini, usimamizi huo huenda ukawa haba siku hizi. Kama vile mwalimu mmoja Mjerumani akirivyo, ‘hakuna kamwe uhakikishio’ wa kuwapo usimamizi wa uangalifu na wenye kutegemeka. Kwa kweli, kijana mmoja alijisifu hivi baada ya safari moja ya matembezi ya darasa: “Tulipokwisha kuwachanganya akili walimu wote wawili, tulifanya vile hasa tulivyotaka.”

Wanafunzi fulani watafanya matata hata walimu wajitahidipo sana kuwanyoosha. Mwalimu mmoja wa zamani akumbuka hivi: “Wale vijana walitafuta njia za werevu mwingi za kupenyeza alkoholi, kwa hiyo ilikuwa kazi-bure kupekua vyumba vyao. Niling’amua kwamba walikuwa wakinywa alkoholi nyingi wakati mmoja wa wasichana alipoanza kutapika.” Kwa wazi, huenda ikawa vigumu sana kuhakikisha kwamba safari itasimamiwa ifaavyo. Hata hivyo huenda wewe ukaepuka hangaiko na aibu nyingi ikiwa wewe na wazazi wako mtachunguza kwa uangalifu ni mipango gani imefanywa kuhusu usimamizi. Yasema hivi Mithali 22:3: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”

Wanashule wenzako huitikiaje kwa jumla mielekezo ya walimu wako? Hii itakupa wazo zuri juu ya jinsi watakavyojiendesha katika safari ya matembezi ya shule. Yaripotiwa kwamba shule moja ya sekondari ya Ujerumani ililazimika kufupisha safari ya siku tatu ya matembezi ya darasa kwa sababu wanafunzi watukutu walipuuza kabisa “yale maagizo ya wazi yenye subira” ya walimu.

Mwanamke mmoja kijana Mjerumani aitwaye Stephanie alienda safari hizo zamani na kutokana na aliyojionea apendekeza ujiulize maswali yanayofuata: ‘Je, wanadarasa wenzangu wana akili za kutosha kuwasikiliza walimu? Je, shule hujitahidi kudumisha sifa njema? Je, walimu ni imara vya kutosha kuandaa uongozi ufaao? Je, vijana huchukua maadili yafaayo kwa uzito? Je, wao hutumia alkoholi na dawa za kulevya?’ Ni kweli, Stephanie akiri kwamba mengi “hutegemea utu wako ulivyo, kama wewe hujilegeza au hujilegezi kwa urahisi.” Lakini ungewezaje kusali kwamba Yehova ‘asikuingize katika kishawishi’ halafu ujiweke kimakusudi katika hali ya kuridhiana?—Mathayo 6:13, New World Translation.

Hivyo Petra mwenye miaka 17 alikataa kwenda safari ya matembezi ya darasa. “Nilijua jinsi wanadarasa wenzangu wangejiendesha,” aeleza. “Ningeweza kuona mapema kwamba hali zinazohusu alkoholi na ngono zingetahini dhamiri yangu kwelikweli. Ikawa kwamba, wavulana watano walivua msichana mmoja mavazi wakampiga picha, na baadaye picha hizo zikazungushwa zikipokezanwa katika ua wa shule.”

Je, masadikisho yako ya kidini yatastahiwa? Kwa kielelezo, Timon kijana, alisema hivi: “Mara nyingi kuna karamu ya kukumbuka siku ya kuzaliwa, na ni vigumu kuiepa.” Kwa kuwa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yeye hukataa kushiriki katika misherehekeo hiyo.a Je, walimu wako na wanadarasa wenzako wangestahi maoni yako ikiwa msherehekeo kama huo ungekuwa sehemu ya safari ya matembezi ya darasa?

Utawekwa kwenye ushirika wa namna gani? Wakristo wajua kwamba Mungu hushutumu kuvuta sigareti, kutumia dawa za kulevya, kutumia alkoholi vibaya, au kujitia katika ngono ya kabla ya ndoa. (1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1) Ndiyo sababu ni hekima kuepuka kushirikiana na vijana wazoeao mambo ya jinsi hiyo. (1 Wakorintho 15:33, NW) Mithali 13:20 huonya hivi: “Rafiki wa wapumbavu ataumia.” Katika safari ya matembezi ya darasa, washinda wakati mwingi zaidi ukiwa na vijana wa jinsi hiyo, tena katika hali ya kustarehe. Andreas kijana alieleza hilo hivi: “Katika safari ya matembezi ya darasa, unawekwa saa zote kwenye roho ya ulimwengu, pamoja na ule muziki wote wa kilimwengu na maongezi yenye aibu.”

Jambo jingine ni kwamba ni rahisi kujihisi mpweke uwapo mbali na nyumbani. Safari za matembezi ya darasa zimewasha cheche za kutaka mahaba katika matineja wengi. Je, kungekuwa na hatari ya wewe kuhusika kimahaba na mtu asiye mwamini? Wakorintho wa Kwanza 10:12 waonya hivi: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” Na hata ingekuwa una nguvu za kutosha kukinza kishawishi, je, kuwapo kwako katika safari hiyo kungeweza kuwa kikwazo kwa vijana wengine Wakristo?—Linganisha 1 Wakorintho 8:7-13; 10:28, 29.

Yvonne mwenye miaka 14 alikataa kwenda safari ya matembezi ya darasa ya kuteleza kwenye theluji. Aeleza hivi: “Ningalitumia juma zima nikiwa na vijana na walimu walimwengu tu. Isitoshe, uandamani wa ndugu zangu, kazi ya kuhubiri, na mikutano—hayo ndiyo mambo ambayo ningeyakosa hasa. Sababu nyingine ilikuwa jinsi vijana walio wengi hujiendesha wasipoangaliwa na mtu yeyote.”

Kumpendeza Mungu Kikamili

Kwa kuwa safari za matembezi ya darasa kwa kawaida hazihusu dini, siasa, wala utendaji mwingine ambao Wakristo hukatazwa, mwanafunzi na wazazi wake watalazimika kuamua kama safari hiyo yafaa. (Linganisha Isaya 2:4; Ufunuo 18:4.) Hali na mambo hutofautiana mahali na mahali na darasa moja na jingine; kwa hiyo Wakristo katika eneo moja huenda wakalazimika kushindana na matatizo yaliyo tofauti na yale ya eneo jingine.

“Mama yangu alifahamu vizuri vijana walio katika darasa langu na alimjua mwalimu kuwa mwenye kujali daraka lake. Kwa hiyo safari ya matembezi ya darasa ilifanikiwa,” aeleza Stephan. “Lakini nilipokuwa na umri mkubwa zaidi na ile safari ya mwisho kabla ya kuhitimu ilipokaribia, suala la kwenda kwangu lilikuwa tofauti kabisa.” Kwa nini? Aendelea kusema hivi: “Miaka mitatu tu mapema kidogo, wanadarasa wenzangu walikuwa wenye kupendeza na kustahika. Lakini dawa za kulevya na ukosefu wa adili tangu wakati huo ulikuwa umekuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku. Kwa hiyo sikujiunga na safari hiyo. Bila kutarajia, ikawa lazima kukomesha ile safari ya mwisho kabla haijamalizwa.”

Ingawa hivyo, ni lazima wewe na wazazi wako mpime mambo yote yahusikayo na ufanye uamuzi wako mwenyewe. Hakikisha kwamba, lolote lile uamualo, mradi wako ni ‘kujiendesha kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili.’—Wakolosai 1:10, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Sikukuu—Sababu Inayofanya Watoto Fulani Wasizisherehekee” katika toleo letu la Novemba 22, 1993.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ungewekwa kwenye ushirika wa namna gani kama ungeenda safari ya matembezi ya darasa ya kulala nje?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki