Maoni ya Biblia
Fungu Lako Katika Sala Zako
KWENYE upande wa mlima ulio juu ya jiji, mfalme mwenye matatizo mengi asimama kifupi ili kutafakari jumba lake la kifalme lenye fahari, jiji kuu lililoenea, na mkasa wenye kusikitisha wa nyumba yake. Jeshi kubwa limejikusanya upande wa kusini na sasa lapiga miguu kuelekea jiji. Maofisa wa ngazi za juu wa serikali wamekuwa wapinzani, na wengi wa watu wamegeukia kuunga mkono waasi. Akiwa mwenye huzuni, huyo mfalme atoa sala kwa Mungu. Akiwa mwanamume wa kidini sana, uhakika wake unaongezeka kwamba Mungu atasikiliza ombi lake na kuharibu mipango ya hao wahaini. Kisha, akigeukia mbali na jiji lake lenye fahari, yeye ateremka mlima na kuelekea kaskazini upande wa jangwani ng’ambo ya mto. Afanye nini zaidi? Hiyo hali sasa iko mikononi mwa Mungu.
Vivyo hivyo, waumini wanyenyekevu leo wanamgeukia Mungu katika sala wakati wa magumu wakiwa na uhakika wenye kufariji kwamba pamoja na kutoa miongozo iliyo wazi ya jinsi ya kusali, Biblia yafunua kwamba Yehova Mungu ndiye “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, New World Translation) Twahakikishiwa kwamba watafutaji wote wa Mungu wenye moyo mweupe watasikilizwa na Mungu.
Hata hivyo, je, imani na sala zatosha? Sisi huwa na fungu gani katika matokeo ya sala zetu?
Twaweza Kuchangiaje?
Mfalme aliyetajwa mwanzoni alikuwa Mfalme Daudi wa Israeli la kale. Akikabiliwa na uhaini wa mwana wake Absalomu mwenye kutenda kwa hila na mshauri wake mnafiki Ahithofeli, yeye alichagua kutoroka Yerusalemu na kutafuta usalama katika jiji lenye ngome la jangwani la Mahanaimu kwenye upande wa mashariki wa Mto Yordani. Yaelekea akiwa amejawa na utamauko, mshuko-moyo, na hangaiko, yeye alimwomba Yehova katika sala, akisema hivi: “Ee BWANA, nakusihi, uligeuze shauri la Ahithofeli liwe ubatili.” (2 Samweli 15:11-15, 30, 31) Hata hivyo, Daudi alifanya zaidi ya kusali. Yeye alichangia kwa njia ifaayo kuelekea matokeo yenye mafanikio ya sala yake. Jinsi gani?
Kuchangia kwake kulianza muda mrefu kabla ya matatizo aliyokabili. Kwa kipindi cha miaka mingi, hata kabla ya kuwa mfalme, Daudi alijithibitisha kuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova. (1 Samweli 16:12, 13; Matendo 13:22) Yeye alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu. Hivyo, alipokuwa chini ya jaribu Daudi alikuwa na imani kwamba Yehova angesikiliza sala yake na kuitikia katika njia ifaayo.
Ndivyo ilivyo leo. Mara nyingi njia ya msingi ya kuchangia matokeo ya sala zetu ni kufuata shauri la Biblia likiwa namna ya kawaida ya maisha. Kufuata huko kwa uaminifu kanuni za kupewa na Mungu huleta uhusiano wa karibu pamoja naye. Ukaribu huu na Mungu na namna ya imani yapasa kuwapo kabla ya majaribu kuanza. Yapasa kuwa kama msingi wenye nguvu ambao juu ya huo nyumba itajengwa; wapaswa kuwapo kabla ya uzito wa jengo kuwekelewa. Hivyo twaweza—hata sasa, kabla ya majaribu kuja—kuchangia matokeo yenye mafanikio ya nyingi za sala zetu.
Uwe na Fungu Tendaji!
Ingawa ni kweli kwamba uhusiano wa Daudi pamoja na Mungu ulikuwa na fungu muhimu sana, yeye pia alitambua kwamba hangekuwa mtazamaji asiyetenda katika kutimizwa kwa sala yake. Kinyume na hilo, Daudi alikuwa na fungu tendaji kama ilivyo wazi katika mwendo wenye hekima uliofuata sala yake.
Miongoni mwa rafiki za Daudi waliokuwa waaminifu mlikuwa na Mwarki aliyeitwa Hushai. Hushai alikutana na huyo mfalme aliyekuwa akitoroka kwenye Mlima wa Mizeituni. Ingawa alitamani kuandamana na Daudi uhamishoni, Hushai alitii sihi la Daudi la kwamba abaki katika jiji. Alikuwa ajisingizie uaminifu-mshikamanifu kwa Absalomu, ajaribu kuharibu shauri lenye usaliti la mshauri Ahithofeli, na kumwarifu Daudi kuhusu matukio. (2 Samweli 15:32-37) Kama ilivyotarajiwa, Hushai alikuwa na mafanikio katika kupata tumaini la Absalomu. Sasa Yehova alikuwa aingilie.
Ahithofeli mwenye maarifa, ingawa hakuwa akifuata mwendo ufaao, alidokeza mpango wenye busara nyingi. Yeye alisihi Absalomu ampe wanaume 12,000 ili kushambulia Daudi usiku huohuo alipokuwa akitoroka, akiwa asiye na mpango na rahisi kushambuliwa—pigo la kifo ambalo lingekamilisha mapinduzi yenye mafanikio! Hata hivyo, kwa mshangao wa wengi, Absalomu alitafuta shauri kutoka kwa Hushai kuhusu hilo jambo. Yeye alimshauri Absalomu achukue muda fulani kukusanya jeshi lenye nguvu mno la wanaume, ambalo halingeongozwa na mwingine yeyote ila Absalomu mwenyewe. Kwa mwongozo wa Yehova, shauri la Hushai lilikubaliwa. Ahithofeli, kwa wazi akitambua kwamba kufuata shauri la Hushai kulimaanisha kushindwa kwa hakika, alirudi nyumbani na kujiua.—2 Samweli 17:1-14, 23.
Hakuna shaka kwamba Yehova alikuwa amejibu sala ya Daudi—kama tu alivyokuwa amesali. Kielelezo cha Daudi cha kufanya kwa kupatana na sala yake chaandaa somo lenye thamani kwa wote wanaotafuta msaada wa Mungu kupitia sala.
Yehova Atafanya Sehemu Yake
Ni kweli, Yesu alifunza wafuasi wake wasali kwa ajili ya mkate wao wa kila siku naye akaahidi kwamba ikiwa waliweka faida za Mungu kwanza, Yeye angeshughulikia mahitaji yao. (Mathayo 6:11, 33) Kwa kielelezo, ikiwa mtu hajaajiriwa, lazima atende kulingana na sala yake ambayo katika hiyo aliomba kuruzukiwa kwa kufanya yote awezayo ili kutafuta au kufanyiza kazi.
Hata sala zetu ziwe ni za jambo gani, uwezo wetu wa kuchangia matokeo hutofautiana sana. Kuna nyakati tuwezapo kufanya mengi na nyakati tuwezapo kufanya machache sana, ikiwa tutafanya chochote. Jambo la maana si kile tuwezacho au tusichoweza kuchangia, bali ikiwa tunafanya kadiri tuwezavyo.
Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ajua hali zetu na uwezo wetu. Yeye atambua kwa ukamili kile tuwezacho kufanya, naye hatatuhitaji kufanya zaidi ya tuwezacho kutimiza. Iwe tutaweza kufanya mengi au machache mno, Yehova atajazilia upungufu wowote. Yeye huthamini na kutegemeza jitihada zetu na atafanya kazi nazo ili kuleta matokeo bora zaidi kwa wote wanaohusika.—Zaburi 3:3-7.
Katikati ya magumu, Mfalme Daudi angetangaza akiwa na uhakika hivi: “Wokovu una BWANA; baraka yako na iwe juu ya watu wako.” (Zaburi 3:8) Uhakika wetu katika uwezo wa Yehova pamoja na kuchangia kwetu sehemu yetu, kwa wingi au kwa uchache, na uongoze kwa matokeo yenye mafanikio ya sala zetu.