Wanasayansi Wanatoa Onyo
“BINADAMU na ulimwengu wa asili wako katika mkondo wa kugongana. . . . Ni miongo michache tu imebaki ili kuepusha matisho [kuelekea mazingira].”
Onyo hili, lililotolewa na UCS (Muungano wa Wanasayansi Wenye Wasiwasi), lilichapishwa katika Annals, jarida la kitiba la Kikanada. Mazoea ya mwanadamu yenye kutisha uhai yakiendelea, ripoti hiyo yaongeza, “huenda yakabadili ulimwengu sana hivi kwamba itakuwa vigumu kutegemeza uhai katika namna tujuayo.”
Baadhi ya mambo yaliyotajwa miongoni mwa matatizo ya muhimu sana ambayo lazima yashughulikiwe ni kupungua kwa ozoni; uchafuzi wa maji; ukataji misitu; kupungua kwa uwezo wa udongo wa kutoa mazao; na kutoweka kwa spishi, ambako kufikia mwaka 2100 huenda kukatia ndani theluthi ya spishi zote zinazoishi sasa. “Kuharibu kwetu mfumo wa uhai wa kutegemeana,” wasema UCS, “kwaweza kusababisha athari zenye kuenea sana, kutia ndani kuharibika kwa mifumo ya kibiolojia ambayo mabadiliko ya kawaida yayo hatuyafahamu kikamilifu.”
Wasiwasi wa UCS ulihakikishwa na zaidi ya wanasayansi 1,600 ulimwenguni pote, kutia ndani watunukiwaji 104 wa tuzo ya Nobel. Kulingana na UCS, “washiriki hawa wa ngazi za juu wa jamii ya wanasayansi ulimwenguni wanaonya jamii yote ya kibinadamu kwamba badiliko katika usimamizi wetu wa dunia linahitajika ikiwa msiba mkubwa wa kibinadamu utaepukwa.”
Biblia yakubali kwamba mwanadamu kwa kweli ‘anaharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Hiyo hata hukubali kwamba badiliko katika usimamizi wa dunia linahitajika. (Yeremia 10:23; Danieli 2:44) Kwa hakika Biblia huahidi kwamba badiliko hilo litatukia, si kupitia jitihada za mwanadamu, bali kupitia Ufalme wa Mungu, serikali ya kimbingu ambayo Yesu alifunza wafuasi wake kuuomba.—Zaburi 145:16; Isaya 11:1-9; Mathayo 6:9, 10.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Picha: Godo-Foto