Kuna Tumaini Gani kwa Maisha Marefu Zaidi?
“Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi tena amejawa na huzuni.”—Maneno ya Ayubu, yaliyorekodiwa katika Ayubu 14:1, “The Jerusalem Bible.”
JINSI ufupi wa maisha umefafanuliwa mara nyingi kwa maneno ya kishairi! Kama alivyosema Ayubu, mwandikaji mmoja wa karne ya kwanza alisema hivi: “Ninyi ni kama ukungu unaotokea kwa muda mfupi tu na kutoweka tena.”—Yakobo 4:14, Habari Njema kwa Watu Wote.
Je, wewe pia umeona kwamba maisha ni mafupi kiasi cha kuhuzunisha? Miaka 400 hivi iliyopita, William Shakespeare aliandika hivi: “Isha, isha, mshumaa usiodumu! Maisha si kitu kingine ila kivuli kipitacho.” Na katika karne iliyopita, chifu fulani aliye Mhindi wa Marekani aliuliza hivi: “Maisha ni nini?” Kisha akajibu: “Ni mafupi kama mmweko wa kimulimuli usiku.”
Binadamu wanaweza kutarajia muda wa uhai wao uwe na urefu wa kadiri gani? Nabii Musa alifafanua hali katika siku yake, yapata miaka 3,500 iliyopita: “Huenda tukaishi miaka sabini au tukiwa wenye afya themanini; lakini yote ni shida na taabu! Siku zapita mbio, nasi twatoweka mara!”—Zaburi 90:10, HNWW.
Miaka sabini—hiyo ni siku 25,567 tu. Na miaka 80 ina siku 29,219 tu. Kwa kweli, siku chache mno! Je, kuna chochote kiwezacho kufanywa ili kurefusha maisha ya binadamu?
Je, Sayansi ya Kitiba Yaweza Kusaidia?
Gazeti Science lilionelea hivi: “Matarajio ya kuishi wakati wa kuzaliwa [katika Marekani] yameongezeka kutoka miaka 47 katika mwaka 1900 hadi miaka 75 hivi katika mwaka 1988.” Kama tokeo la kupunguza kiwango cha vifo vya vitoto kupitia utunzaji afya na lishe bora zaidi, watu katika Marekani wanaweza sasa kutarajia kuishi karibu urefu wa maisha aliotaja Musa. Hata hivyo, je, kuna maongezeko yenye kutazamisha yanayotarajiwa kuhusu kadiri ya urefu ambao watu walio wengi huishi?
Kwa kutokeza, Leonard Hayflick, mtaalamu mkuu wa kuzeeka, alisema katika kitabu chake How and Why We Age: “Maendeleo katika utafiti wa tiba ya kibiolojia na utekelezwaji wa utunzaji wa kitiba ulioboreshwa katika karne hii kwa hakika umekuwa na matokeo makubwa kwa maisha marefu ya binadamu, lakini ni kwa kuruhusu tu watu zaidi wafikie kiwango cha juu kilichowekwa cha muda wa uhai wa binadamu.” Kwa hiyo yeye alieleza hivi: “Matarajio ya kuishi yameongezeka lakini muda wa kuishi haujaongezeka; tofauti hiyo ni ya maana sana.”
Ni kipi “kiwango cha juu kilichowekwa” cha muda wa kuishi wa binadamu? Wengine husema hakuna uhakika kwamba kuna yeyote katika nyakati za hivi majuzi aliyepata kuishi zaidi ya umri wa miaka 115. Hata hivyo, gazeti Science lilisema hivi: “Kuanzia mwaka 1990, umri mkubwa kuliko wote uliohakikishwa ambao mtu ameishi ni kupita tu miaka 120.” Na mapema mwaka huu waziri wa afya wa Ufaransa, pamoja na vikundi vikubwa vya maripota na wapiga-picha, walimtembelea Jeanne Calment wa Arles, Ufaransa, ili kusherehekea mwaka wake wa 120 wa kuzaliwa. Musa pia aliishi kufikia umri wa miaka 120, akipita kwa mbali sana wastani wa miaka.—Kumbukumbu la Torati 34:7.
Je, wanasayansi watoa tumaini kwamba watu kwa kawaida wataishi urefu huo au zaidi? La, wengi hawafanyi hivyo. Kichwa kikuu katika Detroit News kilisomeka hivi: “Watafiti Wasema Miaka 85 Huenda Ikawa Ndiyo ya Juu Zaidi ya Muda wa Maisha wa Wastani.” Katika makala hiyo mtaalamu anayetambulika wa kuzeeka, S. Jay Olshansky, alisema hivi: “Unapozidi miaka 85, watu hufa kutokana na kutofanya kazi kwa viungo vingi vya mwili. Wao hukoma kupumua. Kwa msingi, hufa kutokana na umri wa uzee. Na hakuna tiba kwa hilo.” Yeye aliongeza hivi: “Isipokuwa kuzeeka kuondolewe kuanzia molekuli zenyewe, hakutakuwa na maongezeko yenye kutazamisha ya kiwango cha kuishi.”
Gazeti Science lilionelea kwamba labda “kiwango cha juu cha maisha marefu tayari kimefikiwa na kwamba mapunguo makubwa ya wale wanaokufa hayaelekei kutokea.” Inasemekana kwamba ikiwa visababishi vyote vya kifo vilivyoripotiwa kwenye vyeti vya kifo vingeondolewa, matarajio ya kuishi yangeongezwa kwa miaka isiyozidi 20.
Hivyo, wanasayansi wengi hawaoni urefu wa muda wa maisha ya mwanadamu kuwa jambo geni wala jambo linaloelekea kubadilika. Hata hivyo kwa nini ni jambo la kiakili kuamini kwamba hatimaye binadamu wataishi muda mrefu zaidi?