Maoni ya Biblia
Je, Kujinyima Sana Raha na Anasa Ndio Ufunguo wa Kupata Hekima?
“MAWALII walivaa pingu za chuma, minyororo, mishipi yenye vitu vyenye ncha kali na kola zenye misumari . . . Wengine walijivingirisha kwenye miiba na mimea yenye kuwasha, wakavutia wadudu kimakusudi ili waumwe, wakajichoma kwa moto na kuchokora majeraha yao hadi yakawa na usaha usiopona. Ulaji wa kujinyima sana ulikuwa njia ya maisha, wengine hata walipita kiasi sana kwa kula tu vitu vilivyooza au vyakula vyenye kuchukiza sana.”—The Saints, kilichoandikwa na Edith Simon.
Hawa walikuwa wenye kujinyima sana raha na anasa. Kwa nini walijitenda vibaya hivyo? Katika kitabu For the Sake of the World—The Spirit of Buddhist and Christian Monasticism, watungaji waeleza kuwa “tangu wakati wa Socrates (karne ya tano K.W.K.) angalau, ilikuwa imeeleweka sana kwamba maisha sahili sana yasiyo na anasa za kingono na za kimwili, yalikuwa sharti la kwanza kabla ya kupata hekima ya kweli.” Hawa wenye kujinyima sana raha na anasa walifikiri kuwa mateso ya kimwili yangeongezea uwezo wa hisi zao za kiroho na kuongoza kwenye mnurisho wa kweli.
Ni vigumu kufafanua sawasawa hali hii ya kujinyima sana raha na anasa. Kwa wengine yamaanisha tu kujitia nidhamu au kujikana mwenyewe. Wakristo wa mapema walithamini sifa kama hizo. (Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:5) Yesu Kristo mwenyewe alipendekeza maisha sahili yasiyozuiwa na mahangaiko ambayo maisha ya ufuatiaji wa mambo ya kimwili waweza kuleta. (Mathayo 6:19-33) Hata hivyo, mara nyingi kujinyima sana raha na anasa huhusianishwa na matendo ya kushika sana maadili fulani na mara nyingi kwa njia ya kupita kiasi, kama yale maisha yaliyotajwa hapo juu. Je, mazoea haya ya kujinyima sana raha na anasa, hasa kwa njia ya kupita kiasi sana, kweli ndio ufunguo wa kupata hekima?
Yategemea Mawazo Yasiyo ya Kweli
Miongoni mwa falsafa zilizotokeza kujinyima sana raha na anasa ni lile wazo la kwamba vitu vya kimwili na raha za kimwili ni mbaya kiasili na kwa sababu hiyo ni vizuizi vya maendeleo ya kiroho. Dhana nyingine inayoruhusu kujinyima sana raha na anasa ni ile itikadi inayokubalika kwa wengi kwamba mwanadamu ana mwili na nafsi. Wenye kujinyima sana raha na anasa huamini kwamba mwili halisi ni gereza la nafsi na kwamba nyama ni adui yake.
Biblia husema nini? Maandiko yaonyesha kwamba wakati Mungu alipomaliza uumbaji wake wa dunia, alisema kuwa kila kitu alichokuwa ameumba—uumbaji wake wote wa vitu vya kiasili na vya kimwili—kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Mungu alikusudia mwanamume na mwanamke katika bustani ya Edeni wafurahie vitu vya kimwili. Jina lenyewe Edeni lamaanisha “Raha” au “Upendezi.” (Mwanzo 2:8, 9) Adamu na Hawa walikuwa wakamilifu na walifurahia uhusiano mzuri na Muumba wao hadi walipofanya dhambi. Tokea wakati huo na kuendelea, kutokamilika kukawa kizuizi kati ya Mungu na mwanadamu. Na bado, kutosheleza tamaa halali za kibinadamu au kufurahia raha za kimwili za kupewa na Mungu iwapo zinapatana na sheria za maadili za Mungu hakungeweza kamwe kutokeza kizuizi cha uwasiliano kati ya Mungu na waabudu wake!—Zaburi 145:16.
Kwa kuongezea, Biblia hufundisha kwa wazi kuwa mwanadamu, akiwa ameumbwa kutokana na mavumbi na akiwa na mwili wenye nyama, ni nafsi. Maandiko hayategemezi wazo la kwamba nafsi ni kitu fulani kisicho na mwili na kisichoweza kufa kilichofungiwa ndani ya mwili wenye nyama wala hayategemezi wazo la kwamba kwa njia fulani mwili wenye nyama humzuia mtu kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu.—Mwanzo 2:7.
Kwa wazi, dhana ya maisha ya kujinyima sana raha na anasa huonyesha picha iliyopotoka juu ya uhusiano wa mwanadamu na Mungu. Mtume Paulo alionya kuwa wengine waliodai kuwa Wakristo wangependelea falsafa za kibinadamu zenye kudanganya kuliko kweli za msingi za Biblia. (1 Timotheo 4:1-5) Kuhusu wengine walioshikilia kauli hii, mwanahistoria mmoja wa kidini asema: “Itikadi ya kwamba mata ni yenye uovu . . . na kwamba nafsi ya mwanadamu lazima iwekwe huru kutokana na uhusiano na mata, ilitokeza maisha ya kujinyima sana raha na anasa na ikizuia kula nyama, ngono na kadhalika, ambayo yangefuatwa tu na walio bora ‘wakamilifu’ au perfecti ambao walipewa mafunzo ya kipekee.” Njia hii ya kufikiri haina tegemezo lolote la Kibiblia na haikuwa itikadi ya Wakristo wa mapema.—Mithali 5:15-19; 1 Wakorintho 7:4, 5; Waebrania 13:4.
Hakuna Haja ya Kujinyima Sana Raha na Anasa
Yesu na wanafunzi wake hawakuwa wenye kujinyima sana raha na anasa. Walivumilia majaribu na dhiki za namna mbalimbali, lakini hawakujiletea kamwe dhiki hizi. Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wawe waangalifu ili falsafa za kibinadamu za udanganyo zisije zikawashawishi kutoka kwenye kweli ya Neno la Mungu na kuwaongoza kwenye mazoea yasiyo ya akili na yenye kupita kiasi. Paulo hasa alitaja “kutendea mwili kwa ukali.” Alisema: “Kwa kweli, mambo hayahaya yana mwonekano wa kuwa na hekima katika namna ya ibada ya kujitwika na unyenyekevu wa dhihaka, kutendea mwili kwa ukali; lakini hayana thamani yoyote katika kupigana na utoshelezaji wa mwili wenye nyama.” (Wakolosai 2:8, 23) Kujinyima sana raha na anasa hakuongozi kwenye utakatifu wa kipekee au mnurisho halisi.
Kweli, mwendo wa utii wa Kikristo hudokeza kujitahidi sana na kujitia nidhamu. (Luka 13:24; 1 Wakorintho 9:27) Mmoja lazima ajitahidi kujipatia ujuzi juu ya Mungu. (Mithali 2:1-6) Pia, Biblia ina onyo kali dhidi ya kuwa mtumwa wa “tamaa na raha” na kuwa “wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.” (Tito 3:3; 2 Timotheo 3:4, 5) Hata hivyo, vifungu hivi vya Kimaandiko havikubali zoea la kujinyima sana raha na anasa. Yesu Kristo, mwanadamu mkamilifu, alifurahia pindi zenye furaha ambazo zilitia ndani chakula, kinywaji, muziki, na dansi.—Luka 5:29; Yohana 2:1-10.
Hekima ya kweli ni yenye kukubali sababu, si yenye kupita kiasi. (Yakobo 3:17) Yehova Mungu aliiumba miili yetu yenye nyama ikiwa na uwezo wa kufurahia raha nyingi maishani. Yeye ataka tuwe na furaha. Neno lake hutuambia: “Mimi najua ya kwamba hakuna jema kwao kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhubiri 3:12, 13.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]
Mtakatifu Jerome akiwa katika Pango/The Complete Woodcuts of Albrecht Dürer/Dover Publications, Inc.