Vijana Huuliza . . .
Namna Gani Ikiwa Wazazi Wangu Wapinga Ndoa Yangu?
Lakesha na rafiki yake wa kiume wanafikiria kuoana, lakini mama yake hakubali. “Nitakuwa na umri wa miaka 19 mwaka huu,” asema Lakesha, “lakini mama yangu asisitiza kwamba tungoje mpaka nitakapofikia umri wa miaka 21.”
IKIWA unapangia kuoa au kuolewa, ni jambo la kawaida tu kutaka wazazi wako wakuunge mkono. Kwa kweli yaweza kuumiza ikiwa wazazi wako wanakosa kumkubali mwenzi uliyemchagua. Wapaswa kufanya nini? Kupuuza wanalotaka, na kuendelea na mipango yako ya ndoa?a
Hili laweza kushawishi ikiwa una umri wa kutosha na unaweza kuoa au kuolewa kisheria bila kibali cha wazazi wako. Hata hivyo, Biblia haiweki kiwango cha umri katika kuonyesha heshima na staha kwa wazazi wako. (Mithali 1:8) Na ikiwa utapuuza hisia zao, ungeweza kusababisha madhara yenye kudumu katika uhusiano wako pamoja nao. Zaidi ya hayo, pia kuna uwezekano—pengine hata yaweza kutokea kuwa kweli—kwamba wazazi wako wana sababu halali za kupinga ndoa yako.
Ni Katika Umri Gani Mtu Anapokuwa Mchanga Sana Kuoa au Kuolewa?
Kwa kielelezo, je, wazazi wako wanakuambia kwamba wewe ni mchanga sana kuoa au kuolewa? Bila shaka, Biblia haiweki umri wa chini kabisa kwa ajili ya ndoa. Lakini hupendekeza kwamba kabla ya kuoa au kuolewa, mtu apaswa kuwa “amepita mchanuko wa ujana”—miaka inayofuatia ubalehe wakati ambapo tamaa za ngono ziko kwenye kilele. (1 Wakorintho 7:36) Kwa sababu gani? Kwa sababu watu hao wachanga wako tu katika hatua za mapema za kusitawisha ukomavu wa kihisia-moyo, kujidhibiti, na sifa za kiroho zilizo za lazima katika kushughulika na maisha ya ndoa.—Linganisha 1 Wakorintho 13:11; Wagalatia 5:22, 23.
Wakati ambapo Dale mwenye umri wa miaka 20 alipoamua kuoa, alivunjwa moyo na upinzani wa wazazi wake. “Walisema nilikuwa mchanga sana na kwamba nilikosa uzoefu,” akataarifu. “Nilihisi tulikuwa tayari na tungeweza kujifunza baada ya kuoana, lakini wazazi wangu walitaka kuhakikisha kwamba sikuwa nikiongozwa tu na hisia-moyo. Waliuliza maswali mengi. Je, nilikuwa tayari kushughulika na maamuzi ya kila siku, mambo ya kifedha, daraka la kuandalia familia kimwili, kihisia-moyo, na kiroho? Je, nilikuwa tayari kuwa mzazi? Je, kwa kweli nilikuwa nimejifunza jinsi ya kuwasiliana? Je, kwa kweli, nilifahamu mahitaji ya mwenzi? Walihisi nilipaswa kujijua mwenyewe vizuri zaidi nikiwa mtu mzima kabla ya kuanza kutunza mtu mzima mwingine.
“Ingawa hatukutaka kungoja, tuliahirisha ndoa yetu kusudi tujipatie muda wa kufikia ukomavu. Wakati tulipooana mwishowe, tuliingia katika uhusiano huo tukiwa na msingi bora na uwezo wa kutegemeza ndoa.”
Wakati Tofauti za Kidini Zinapohusika
Wakati Terri alipositawisha hisia za kimahaba kwa mwanamume ambaye hakushiriki imani yake ya kidini, alimpatia miadi ya kijinsia kisiri. Baada ya kutangaza mipango yao ya kuoana, Terri alifadhaishwa kupata kwamba mama yake alipinga hiyo ndoa. “Sitaki mama yangu ahisi namna hii kunielekea,” akaomboleza Terri. “Bado nataka tuwe na ule uhusiano wa mama na binti.”
Lakini ni nani aliyekuwa akizuia huo uhusiano? Je, mama ya Terri alikuwa mkatili au asiyekubali sababu? La, alikuwa tu akitegemeza shauri la Biblia kwa Wakristo la kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kwa kweli, Biblia huamuru: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14, 15) Kwa nini hivyo?
Sababu mojawapo ni kwamba, upatano wa kidini ni hali inayosaidia sana katika ndoa yenye furaha na mafanikio. Wataalamu husema kwamba shida na mikazo zinazoshirikishwa na ndoa za mchangamano wa imani mbili mara nyingi huongoza kwenye talaka. Ingawa hivyo, sababu iliyo ya maana zaidi, ni ule uwezekano wa mtu kusongwa ili kuridhiana itikadi zake za kidini—au kuziacha kabisa. Hata ikiwa mwenzi asiyeamini hataingilia ibada yako, bado ungelazimika kuishi na ile huzuni kubwa ya kutoweza kushiriki masadikisho yako yenye kina kirefu pamoja naye. Je, hii yasikika kama mbinu kwa ajili ya maisha ya ndoa yenye raha mustarehe?
Kwa hiyo Terri alikuwa na uamuzi mgumu wa kufanya. “Nampenda Yehova Mungu,” akasema Terri, “lakini sitaki kumpoteza rafiki yangu wa kiume.” Kwa wazi huwezi kufanya yote mawili. Huwezi kuridhiana viwango vya Mungu na bado uonee shangwe upendeleo na baraka zake.
Ingawa hivyo, labda, wazazi wako wanapinga usioane na Mkristo mwenzako fulani. Je, yawezekana kufungiwa nira isiyosawazika na mwamini? Ndiyo, ikiwa mtu huyo hashiriki miradi yako ya kiroho au ujitoaji kwa Mungu. Ikiwa mambo yako hivyo au ikiwa mtu huyo ‘haripotiwi vema’ na akina ndugu walio katika kutaniko lake, wazazi wako waweza kuhangaika ifaavyo juu ya kuoana na mtu huyo.—Matendo 16:2.
Namna Gani Tofauti za Kijamii au za Kitamaduni?
Wazazi wa Lynn walitokeza vipingamizi kwa sababu tofauti: Alitaka kuolewa na mtu wa jamii tofauti. Biblia hufundisha nini katika suala hili? Hutuambia kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi” na kwamba “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Matendo 10:34, 35; 17:26) Wanadamu wana asili moja na ni wenye thamani sawa mbele ya macho ya Mungu.
Ijapokuwa hivyo, ingawa wenzi wote wa ndoa huteseka kutokana na “dhiki katika mwili,” wenzi kutoka jamii tofauti waweza kupatwa na magumu zaidi. (1 Wakorintho 7:28) Kwa nini? Kwa sababu watu wengi katika ulimwengu wa leo uliojaa chuki hawakubali maoni ya Mungu juu ya jamii. Ingawa ndoa kati ya jamii tofauti zinazidi kuwa za kawaida katika nchi fulani za Magharibi, bado kuna maeneo ambayo wenzi waliochangamana hukabiliwa na ubaguzi mkali. Kwa hiyo huenda wazazi wako wakahofia kwamba hujajiandaa kushughulika na misongo ya namna hii.
“Wazazi wangu walifikiri kwamba ingekuwa vigumu sana kwetu,” akakiri Lynn. Kwa hekima, Lynn alistahi hisia zao na hakukimbilia ndoa. Wazazi wake walipochunguza kwa makini ukomavu wa Lynn na kujuana vizuri zaidi na mwanamume aliyempenda, hatua kwa hatua walianza kuhisi uhakika fulani wa kwamba angeweza kushughulika na misongo ya ndoa hii. Lynn asema: “Mara walipohisi kwa kweli tungeweza kuwa wenye furaha pamoja, wao pia walifurahi.”
Ingawa hivyo, nyakati nyingine, suala si jamii bali utamaduni. Wazazi wako huenda wakahangaika kwamba, hatimaye, ungepata ikiwa vigumu kufurahia kuishi pamoja na mtu fulani ambaye mtindo-maisha, mataraja, na mapendezi katika chakula, muziki, na vitumbuizo ni tofauti sana na yako. Kwa vyovyote vile, kuoana na mtu wa jamii tofauti au wa utamaduni tofauti kwaweza kutokeza magumu makubwa. Je, umejiandaa kushughulika na haya magumu?
Wakati Upinzani wa Wazazi Unapoonekana Kuwa Usio Wenye Kukubali Sababu
Lakini namna gani ikiwa wahisi kuwa wazazi wako wanakosa kukubali sababu kabisa katika upinzani wao? Mwanamke kijana aitwaye Faith, asema hivi kuhusu mama yake: “Mama yangu ametalikiwa kwa mara kadhaa. Anasema huwezi kamwe kumjua kikweli mtu mnayeoana naye mpaka inapokuwa ni kuchelewa sana. Amesadiki kwamba sitakuwa mwenye furaha katika ndoa.” Nyakati nyingi, wazazi ambao wamekuwa na ndoa zilizokosa kufaulu hawawezi kuona ndoa ya mtoto wao kwa njia iliyosawazika. Katika visa vingine, wazazi wanakuwa na nia yenye kutiliwa shaka ya kupinga ndoa ya mtoto wao, kama vile tamaa ya kudhibiti maisha ya mtoto daima.
Ikiwa wazazi wako hawataki kusababu waweza kufanya nini? Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazee wa kutaniko waweza kuitwa ili kutoa msaada katika kutatua matatizo ya familia. Bila kupendelea, wanaweza kusaidia washiriki wa familia kuzungumza juu ya matatizo kwa njia ya utulivu, amani, na yenye matokeo.—Yakobo 3:18.
Kutafuta Amani
Bila shaka, sababu nyingine zingeweza kuchochea upinzani wa wazazi wako juu ya kuoa au kuolewa kwako, kama vile mahangaiko ya kifedha au utu wa anayetazamiwa kuwa mwenzi. Na katika kizazi cha UKIMWI na maradhi mengine yanayoambukizwa kingono, wazazi wako wangeweza kuhangaikia ifaavyo afya yako ikiwa mchumba wako alikuwa na maisha ya ovyoovyo kabla hajawa Mkristo.b
Maadamu unaishi katika nyumba ya wazazi wako, unawajibika kutambua mamlaka yao juu yako. (Wakolosai 3:20) Hata ikiwa unajitegemea na una umri wa kutosha kufanya maamuzi yako mwenyewe, usifanye upesi kuachia mbali mahangaiko ya wazazi wako. Uwe na nia ya kusikiliza. (Mithali 23:22) Chunguza kwa uangalifu matokeo yanayowezekana ya kuoana.—Linganisha Luka 14:28.
Baada ya kufanya hivyo, waweza kuamua kwamba bado unataka kuolewa. Kiasili, utalazimika kuchukua kikamili daraka linaloletwa na uamuzi kama huo. (Wagalatia 6:5) Ikiwa umefanya jitihada zote za kufikiria kwa uangalifu maoni ya wazazi wako, labda watachochewa kutegemeza uamuzi wako, ingawa kwa kusita. Lakini ikiwa wao waendelea kutokeza vipingamizi, usijaribu kuwa mchungu wala usiwe mwenye hasira. Kumbuka: Wazazi wako wanakupenda na wanajali furaha yako ya wakati ujao. Fuliza kujaribu kufanya amani pamoja nao. Kadiri ufanikiwavyo katika ndoa yako, labda mtazamo wao utakuwa mzuri kidogo.
Kwa upande mwingine, ikiwa kwa kweli utafikiria kwa uangalifu kila jambo ambalo wazazi wako watasema na kujichunguza mwenyewe kabisa na mtu yule uliye na hamu ya kuoa au kuolewa naye, usishangae ikiwa utafikia ule mkataa wenye kushtua kwamba huenda hata wazazi wako walisema kweli.
[Maelezo ya Chini]
a Habari iliyo katika makala hii inaelekezwa kwa vijana walio katika mabara ambapo ni desturi kwa mtu kujichagulia mwenzi wa ndoa.
b Ona makala “Kusaidia Wale Walio na UKIMWI,” katika toleo la Amkeni! la Machi 22, 1994.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Huenda wazazi wako wakahisi u mchanga sana kuoa au kuoleway