Ni Nani Atakayesafisha Dunia Yetu?
“NINATABIRI kwamba kufikia mwaka wa 2025 neno ‘uchafuzi’ litatoweka kwa kiasi kikubwa kwenye msamiati wa taifa letu kwa kadiri ambavyo viwanda vyetu vinahusika.” Huo ulikuwa utabiri wa hivi majuzi uliofanywa na msimamizi wa shirika la kemikali. Je, unaamini kwamba jambo hilo litatukia? Ikiwa ndivyo, jambo hilo litatimizwa namna gani?
Mara nyingi kutamani faida ndiko huchochea mauzo ya bidhaa zisizokuwa salama. Kwa kielelezo, sheria zinazohusu siri za biashara huruhusu makampuni ya kutengeneza dawa za kuua wadudu zihifadhi fomyula fulani zenye kuleta faida zikiwa siri kwa kuweka kibandiko “tepetevu” kwenye viambato vyao, neno ambalo hufasiriwa kwa urahisi kuwa “-siodhuru.” Lakini, “angalau viambato 394 tepetevu vimetumiwa kuwa dawa kali za kuua wadudu,” laripoti gazeti Chemical Week. Kati ya viambato hivi, 209 ni vichafuzi hatari, 21 vimeainishwa kirasmi kuwa vyaweza kusababisha kansa, na 127 husababisha hatari za kiafya zinazohusiana na kazi!
Kweli, mara nyingi sheria za kuhakikisha usalama za serikali zimekuwa zenye faida. Lakini mahangaiko makubwa ya serikali kadhaa, asema mwandishi mmoja, ni “ukuzi wa kiuchumi na faida inayoletwa na viwanda.” Hivyo, wanakabiliwa daima na mambo mawili wasiyoweza kuyapata wakati mmoja—hatari dhidi ya faida. Kwa asili, matokeo ni ‘uchafuzi uliodhibitiwa.’
Kwa hiyo tutapata wapi majibu? Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimzushia swali hili mwenye nyumba mwenye urafiki. Akionyesha itibari kwa viongozi wa kibinadamu na wanasayansi, mtu huyo alijibu: “Siku moja watarekebisha mambo.”
“Lakini ni nani hao?” akauliza Shahidi huyo. “Je, wao si watu kama wewe na mimi? Huenda wakawa na elimu zaidi, lakini wana mapungukiwa yao, udhaifu wao. Wanakosea.” Ongezea matatizo makubwa sana yanayowakabili vilevile pupa na ufisadi katika jamii ya kibinadamu.
Je, wewe pia waamini kwamba wao watarekebisha mambo? Historia ndefu ya binadamu ya kutoweza kufanya hivyo haitoi sababu ya kuwa na imani katika wanadamu. Gazeti Outdoor Life lilisema: “Wanasayansi na vyombo vyao ni stadi zaidi katika kuchunguza matatizo ya uchafuzi kuliko kuyatatua.” Kuna mataraja gani kwamba wanadamu wanaweza kutatua tatizo hili kubwa?
Je, Wanadamu Wanaweza Kulitatua Peke Yao?
Kudhibiti uchafuzi wa kemikali si tatizo tu la wenye mamlaka wa mahali penu. Hii ni kwa sababu kemikali zinazotumiwa katika nchi moja huathiri watu katika nchi jirani, hata watu ulimwenguni pote! Na wanadamu wameshindwa kushirikiana kutatua matatizo ya namna hiyo ya ulimwengu. Biblia inaonyesha ni kwa nini inaposema: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa has[a]ra yake.” (Mhubiri 8:9) Kwa nini wanadamu wanakosa kufaulu kujitawala? Tena, Biblia yaeleza: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Jambo hilo linamaanisha nini?
Linamaanisha kwamba wanadamu kamwe hawakuumbwa wajitawale wenyewe bila mwelekezo wa Mungu. Ni kweli, wanadamu wamefanya mambo yasiyo na kifani—wamejenga makao ya kustaajabisha, wakatengeneza vyombo stadi, hata wakasafiri kwenye mwezi—lakini wanashindwa kujitawala wenyewe bila mwongozo wa kimungu. Hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha, na historia inathibitisha usahihi wa Biblia.
Dunia Iliyosafishwa —Kupitia Njia Gani?
Sikuzote Muumba wetu Yehova Mungu, anahangaika kuhusu wanadamu na dunia hii, aliyoitayarisha kwa ajili ya mwanadamu. Baada ya kuwaumba wanadamu, aliagiza kwamba watunze dunia na uhai ulio juu yake. (Mwanzo 1:27, 28; 2:15) Baadaye, wenzi wa kwanza wawili walipoasi maagizo yake, aliagiza taifa la kale la Israeli kuhusu kutunza nchi, kutia ndani takwa la kuiacha ipumzike kwa mwaka mzima baada ya kila miaka saba. Hii iliruhusu nchi istarehe. (Kutoka 23:11; Mambo ya Walawi 25:4-6) Lakini watu wakawa na pupa na wakakosa kumtii Mungu. Wao pamoja na nchi wakateseka.
Bila shaka, uchafuzi wa kemikali kama tulio nao sasa, haungeweza kupatikana huko nyuma. Lakini, nchi ikaharibiwa kwa sababu Waisraeli walikosa kuiacha ipumzike kulingana na kusudi la Mungu, na watu wasiokuwa na hatia wakateseka. Hivyo Mungu aliruhusu Wababiloni washinde Israeli na kuchukua taifa hilo kwenye utekwa huko Babiloni kwa miaka 70. Adhabu hii iliruhusu nchi hiyo ipumzike ili kwamba ipate nguvu tena.—Mambo ya Walawi 26:27, 28, 34, 35, 43; 2 Mambo ya Nyakati 36:20, 21.
Historia hii hutufundisha kwamba Mungu huwatoza hesabu wanadamu kwa yale wanayofanyia dunia. (Waroma 15:4) Kwa kweli, Mungu anaahidi kwamba ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’ (Ufunuo 11:18) La maana, Biblia hufafanua aina ya watu wanaochangia ‘uangamizi’ huu. Tabia zao kuu, kama zinavyoorodheshwa katika Biblia kwenye 2 Timotheo 3:1-5, zinatia ndani kujishughulisha sana na pesa na ubinafsi kufikia kiwango cha kutojali sana Mungu, na zaidi sana, uumbaji wake, kutia ndani wanadamu wenzao.
Kwa hiyo, mafungu haya mawili ya Biblia—2 Timotheo 3:1-5 na Ufunuo 11:18—yaelekeza kwenye mikataa miwili thabiti. Mkataa wa kwanza, akili chafu huongoza kwenye dunia iliyochafuliwa. Mkataa wa pili, Mungu ataingilia kuokoa sayari hii na wanadamu wanaomcha Mungu wakati uchafuzi huo wa aina mbili utakapofikia kilele chake. Mungu ataingiliaje mambo?
Kupitia nabii wake Danieli, Mungu alitabiri hivi: “Katika siku za wafalme hao [kwa wazi akirejezea serikali za kisasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Ufalme huo ni serikali halisi ya ulimwengu. Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake waiombee serikali hiyo aliposema: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, . . . acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.
Chini ya usimamizi wenye upendo wa Ufalme wa Mungu, wakazi wa dunia watafurahia pendeleo kubwa la kuifanya dunia yote kuwa paradiso. Hewa itakuwa safi na yenye kupendeza, vijito vitakuwa na maji safi, na ardhi itatokeza mimea isiyochafuliwa. (Zaburi 72:16; Isaya 35:1-10; Luka 23:43) Baada ya hapo, Biblia inaahidi: “Mambo ya kwanza [magonjwa ya kisasa, kuteseka, uchafuzi, na ole nyingine nyingi] hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Dunia iliyosafishwa—je, wewe utaishi uione?