Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 1/8 kur. 18-22
  • Magumu na Baraka za Kulea Wana Saba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Magumu na Baraka za Kulea Wana Saba
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nilikuwa na Kazi Nyingi Kwelikweli!
  • Kulea Wana Wetu kwa Kutumia Kanuni za Biblia
  • Mambo ya Kitheokrasi Yenye Kufurahisha
  • Kujifunza Nidhamu Kutokana na Keki
  • Maisha Yalijaa Furaha
  • Jinsi Wana Wetu Walivyoiona Nidhamu
  • Tulipata Matatizo Pia
  • Badiliko Kubwa Katika Maisha Yetu
  • Tulipewa Mradi Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Namshukuru Yehova kwa Ajili ya Wanangu Watano
    Amkeni!—1999
  • Mbegu Zilizozaa Matunda Miaka Mingi Baadaye
    Amkeni!—1999
  • Wazazi Wetu Walitufundisha Kumpenda Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 1/8 kur. 18-22

Magumu na Baraka za Kulea Wana Saba

Kama ilivyosimuliwa na Bert na Margaret

Nilizaliwa mwaka wa 1927, kule Omaha, Jimbo la Nebraska, Marekani, nami nikakulia Jimbo la South Dakota. Bado naweza kuukumbuka ujana wangu wakati wa miaka ya magumu yaliyosababishwa na ule Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi (1929-1942). Mama alikuwa na desturi ya kupika chakula alichokiita mchuzi wa njaa. Ili kuutayarisha mchuzi huu, yeye alikuwa akiweka mafuta kidogo katika kikaango na kuyaongezea maji, nasi tukachovya mkate katika mchuzi huu. Mambo yalikuwa magumu kwa familia nyingi wakati huo.

WASHIRIKI wa familia yetu hawakujishughulisha na mambo ya dini—tuliona unafiki mkubwa sana katika dini za Kiprotestanti za kwetu. Ile miaka miwili niliyotumikia katika jeshi wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili ilibadili kufikiri kwangu. Wakati huo ndipo nilipoanza kunywa pombe na kucheza kamari.

Nikiwa likizoni kutoka kwenye jeshi, nilihudhuria dansi moja katika eneo letu nikakutana na Margaret Schlaht, msichana ambaye ni nusu Mjerumani na nusu Mwukrainia. Tukapendana, na baada ya kufanya uchumba kwa miezi mitatu, tukafunga ndoa, mwaka wa 1946. Tulizaa wana saba katika kipindi cha miaka minane, nasi kwa kweli tukatambua ugumu wa kuwa wazazi.

Mnamo mwaka wa 1951, nilijeruhiwa vibaya sana katika aksidenti kwenye kiwanda cha kupasulia mbao nusura mkono wangu wa kushoto ukatike. Ilibidi nilazwe hospitalini kwa miaka miwili ili nipandikizwe ngozi na mifupa. Nikiwa hospitalini, Margaret alichukua daraka la kuwatunza wana wetu watano. Marafiki na majirani walimsaidia kukabiliana na magumu yaliyompata wakati huo. Kule hospitalini, nilikuwa na wakati mwingi wa kutafakari juu ya kusudi la uhai. Nilijaribu kuisoma Biblia lakini sikufanikiwa kuielewa vizuri.

Muda mfupi baada ya kuondoka hospitalini, tulihamia mji wa Opportunity, ulio katika Jimbo la Washington, nami pamoja na shemeji yangu tukaanza kufanya kazi ya ujenzi. Sasa nitampisha Margaret ili asimulie mambo yake.

Nilikuwa na Kazi Nyingi Kwelikweli!

Nililelewa katika shamba moja ambamo tulikuza nafaka, tulifuga ng’ombe wachache wa maziwa, na kutia matunda na mboga makoponi. Nilikuwa na bidii ya kufanya kazi nayo ikanitayarisha kwa ajili ya magumu mengi ya wakati ujao katika maisha. Tulikabiliana na ule Mshuko wa Kiuchumi kwa njia nzuri kuliko watu wengi, kwa kuwa angalau tulipata chakula kwa ukawaida.

Wazazi wangu hawakujishughulisha na dini, ingawa mimi nilienda shule ya Jumapili mara chache. Ndipo tukafunga ndoa na Bert tukiwa na umri wa miaka 19. Hatukufunga ndoa kanisani—bali tulifanya sherehe ndogo katika sebule ya nyumba ya wazazi wetu, huku tukisimamiwa na mhudumu wa Kanisa la Congregational. Katika kipindi cha miaka michache, nilizaa wavulana saba—Richard, Dan, Doug, Gary, Michael, Ken, na mwishowe, Scott, mwaka wa 1954. Walikuwa wengi wee!

Baada ya kuhamia Opportunity, mwanamke fulani alitutembelea ili kuzungumza nasi juu ya Biblia. Nikamwuliza kama anaamini kuna moto wa helo, fundisho lililonitisha sana. Nilifarijika kama nini aliponifafanulia kwamba moto wa helo si fundisho la Biblia wala fundisho la kutokufa kwa nafsi halipatikani katika Biblia! Niliogopa sana kufa na sikuelewa jinsi ambavyo Mungu wa upendo angehusishwa na moto wa helo. Niliazimia kwamba kamwe sitawafundisha watoto wangu uwongo kama huo.

Mwaka wa 1955, nilianza kujifunza Biblia kupitia kitabu kiitwacho “Let God Be True.”a Kama ilivyotazamiwa, ni wakati huo ndipo hasa mhubiri wa kanisa la Pentecostal alianza kupendezwa na hali yangu akitaka kuniokoa kutokana na Mashahidi wa Yehova! Alifanya kosa kubwa—alianza kunihubiria juu ya moto wa helo! Hata akatuma washiriki watatu wa kike wa kanisa la Pentecostal alilosimamia ili wajaribu kunishawishi nisifunzwe na Mashahidi.

Nilipokuwa nikijifunza Biblia, Bert alisikiliza akiwa sebuleni. Baadaye, alianza kusoma Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, akaanza kuelewa mambo. Wakati huo alikuwa akifanya kazi ya zamu iliyokwisha saa sita ya usiku. Alikuwa akinipata nimelala aliporudi nyumbani. Usiku mmoja nilinyemelea polepole hadi chumba cha chini nikampata akivisoma vitabu vyangu kisiri! Nilirudi polepole kitandani, huku nikifurahi kwa sababu alikuwa akijichunguzia mambo mwenyewe. Hatimaye, yeye pia alijifunza Biblia, tukawa Mashahidi waliobatizwa mwaka wa 1956.

Kwa kuwa nilizaa wana saba katika kipindi cha miaka minane, ilikuwa kazi ngumu kuwalisha, kuwavalisha, na kudumisha nyumba ikiwa safi kila siku. Wavulana hawa walijifunza kufanya kazi walizogawiwa nyumbani. Nimezoea kusema kwamba sikuwa na mashine moja tu ya kuoshea vyombo—bali mashine saba! Kila mmoja aliosha vyombo kwa zamu. Bila shaka Bert alisaidia sana. Yeye alihakikisha nidhamu na sheria za nyumbani zinafuatwa na bado akadumisha mawasiliano kati yake nao. Wana hao walimstahi baba yao lakini hawakumwogopa. Bert kamwe hakulipuuza daraka lake la kuwafundisha wana wetu juu ya ngono na uzazi.

Richard, kifungua mimba wetu, alienda kutumikia katika makao makuu ya Watch Tower Society yaliyoko Brooklyn, New York, mwaka wa 1966. Halikuwa jambo rahisi kumwona mwana wetu wa kwanza akiondoka nyumbani. Kile kiti mezani kilichobaki wazi kila siku kilinifanya nihisi maumivu ya moyoni. Lakini nilifurahi kwa sababu alikuwa anapata ujuzi na mafunzo mazuri.

Nitampisha Bert aendelee na masimulizi haya.

Kulea Wana Wetu kwa Kutumia Kanuni za Biblia

Mimi na Margaret tulibatizwa kwenye mkusanyiko kule Spokane, Washington. Sasa tukawa na kazi ya kuwalea wana wetu kwa kutumia kanuni za Biblia—ionekanayo kuwa mtindo wa kizamani. Nilikataza uwongo wowote na viwango maradufu, na wana wetu walijua. Tuliwafundisha kwamba Yehova astahili kupewa kilicho bora kabisa.

Ingawa hivyo, walijua kwamba wanaweza kuniambia siri zao kwa sababu tulikuwa na uhusiano wa karibu na tulifanya mambo mengi pamoja. Tukiwa familia, tulifurahia kwenda ufuoni, kwenda mandari milimani, na kucheza mpira. Tulikuwa na mifugo na pia bustani, na wavulana wetu walisaidia popote palipokuwa na uhitaji. Hivyo walijifunza kufanya kazi na pia kucheza. Tulijaribu kuwa na usawaziko katika yale tuliyofanya.

Mambo ya Kitheokrasi Yenye Kufurahisha

Kwa upande wa mambo ya kiroho, sote tulihudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme pamoja, nasi tulikuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida. Mwaka wa 1957 tulihudhuria mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika Seattle, Washington. Mwito ulitolewa kwenye programu hiyo familia zihamie na kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa wa Mashahidi wa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Familia yetu ililiona jambo hilo kuwa zuri, tukaanza mpango wa kuhama. Kwanza tulienda Missouri mwaka wa 1958 halafu baadaye Mississippi mwaka wa 1959.

Tulifanya jambo la kwanza la kitheokrasi lenye kufurahisha mwaka wa 1958. Nilitengeneza trela la kukokotwa lililotumika kama makao na tulilikokota kwa kutumia gari zee lenye kutoshea watu watatu na lenye silinda sita aina ya DeSoto lililoundwa mwaka wa 1947. Sisi sote tulisafiri kwenda New York mwaka huo katika gari hilo ili kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa. Safari yetu ilichukua majuma kadhaa, tukipiga kambi njiani kuanzia Spokane, Pwani ya Magharibi hadi jijini New York—umbali wa kilometa 4,200! Wana wetu wangali wanaikumbuka safari hiyo kwa uchangamfu kuwa ni wakati uliotumiwa vizuri na wa burudani kubwa.

Kujifunza Nidhamu Kutokana na Keki

Kwenye mkusanyiko huo tulipata nakala za kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana.b Kitabu hicho pamoja na Biblia kikawa msingi wa funzo la Biblia la familia yetu kila juma. Wana wetu wote walijifunza kusoma wakiwa wachanga. Baada ya hao kutoka shuleni, Margaret alikuwa akitumia muda fulani pamoja nao, akiwasikiliza wakisoma Biblia. Hatukuruhusu televisheni itawale akili zao.

Familia yetu ilidumisha nidhamu na staha. Siku moja Margaret alioka keki kubwa—kazi aliyoijua sana. Mlo wa siku hiyo ulikuwa na karoti. Kila mara tuliwatia moyo wana wetu angalau wale mboga. Doug hakupenda karoti. Aliambiwa kwamba asipokula karoti, hataionja keki. Na bado alikataa kumaliza chakula chake. Margaret akamwambia, “usipozila karoti hizo, keki yako tutampa mbwa.” Sidhani Doug aliyaamini aliyoambiwa na mama yake hadi hapo alipomwona mbwa Blackie akiimeza keki yake tamu! Tukio hilo lilimfunza yeye na ndugu zake somo. Sisi wazazi tulifanya lile tulilosema.

Maisha Yalijaa Furaha

Mimi na Margaret tuliongozwa na maneno aliyoyasema Yesu katika Mathayo 6:33: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” Sote tukiwa familia, tulijaribu kuweka mambo ya Ufalme kwanza. Tulifurahia kuhubiri pamoja, nami nilihubiri na wavulana wangu kwa zamu nyumba hadi nyumba. Kila mmoja alikuwa na mkoba wake, Biblia, na fasihi ya Biblia. Tuliwapongeza kwa maendeleo yoyote waliyofanya. Mara nyingi Margaret aliwakumbatia. Kwa kweli, tuliwaonyesha shauku kwa ukawaida. Sikuzote tulitumia wakati pamoja na wana wetu—maisha yalijaa furaha!

Wana wetu walipoendelea kukua, walikuwa na daraka kama vile kuwapeleka watu mikutanoni, kufungua Jumba la Ufalme, na kutimiza wajibu mwingine pia. Walijifunza kuthamini sana Jumba la Ufalme kama mahali pao pa ibada nao wakafurahia kulitunza.

Tuliwatia moyo watoe maelezo kwenye mikutano ya Kikristo. Walitoa hotuba fupi za wanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na hatimaye wakawa wasemaji. Mwana wetu wa tano, Michael, hakupenda kusema mbele ya watu na hakuwa mtulivu jukwaani. Akiwa katikati ya hotuba, angeanza kutoa machozi kwa sababu ya kufadhaika. Baadaye, alilishinda tatizo hilo, na wakati huu, akiwa tayari ameoa, yeye ni mwangalizi asafiriye, akitembelea makutaniko mbalimbali na kutoa hotuba mara nyingi katika juma moja. Badiliko kubwa lililoje!

Jinsi Wana Wetu Walivyoiona Nidhamu

Mleta-habari wa Amkeni! alimhoji Michael ili apate maoni yake juu ya kulelewa kwa mtindo wa kizamani. “Tulimwona Baba kuwa mtiaji-nidhamu mzuri. Nakumbuka kwamba nikiwa tineja nilifanya kazi katika kituo cha redio. Nilitaka kununua gari ili nifanye huduma ya painia wa wakati wote. Meneja wa kituo hicho alitaka kuniuzia gari lake aina ya Ford Mustang lenye milango miwili, gari la mashindano ambalo vijana walilipenda sana. Nilitamani sana kulinunua gari hilo, hata ingawa nilijua halikufaa sana kubebea watu wengine tunaposhiriki katika huduma. Nilimwendea Baba nikiwa na wasiwasi. Nilipomwambia juu ya gari hilo, alisema, ‘Acha tuongee juu ya hilo.’ Nilifahamu maana ya usemi huo! Alinisaidia kusababu akanionyesha faida za kuwa na gari lenye manufaa mengi. Hivyo nikanunua gari la milango minne, na baada ya kuliendesha kwa zaidi ya kilometa 160,000 katika mgawo wangu wa kuhubiri, nilisema tu, ‘Baba aliniambia ukweli.’

“Safari yetu ya huku na huku tulipokuwa watoto—kutoka Washington hadi Missouri halafu Mississippi—lilikuwa jambo lenye kusisimua. Tuliifurahia. Hata ingawa familia yetu ya watu tisa iliishi katika trela lenye kukokotwa lenye ukubwa wa meta 2.5 kwa meta 11, bado tulifurahia sana na hilo likatufunza namna ya kufanya mambo kwa mpango na kuishi pamoja kwa amani katika nyumba ndogo. Bila shaka, tulicheza nje mara nyingi.

“Jambo jingine ninalokumbuka na kulithamini sana ni jinsi ambavyo Baba aliongoza andiko la siku. Yeye alienda shule ya wazee mwaka wa 1966 iliyofanywa katika Kingdom Farm, South Lansing, New York, akaona kwamba familia ya Betheli ilifanya utafiti ndipo itoe maelezo juu ya andiko la siku kila siku. Aliuanzisha utaratibu huo katika familia yetu. Tukiwa wana saba, kila mmoja wetu alipewa mgawo wa kutoa maelezo aliofanyia utafiti, kila mmoja na asubuhi yake. Ingawa nyakati nyingine tulilalamika, utaratibu huu ulituwezesha kufanya utafiti na kutoa maelezo yetu. Mazoea kama hayo hudumu muda wote wa maisha.

“Nilivutiwa sana na jinsi Mama na Baba walivyojidhabihu kwa niaba yetu. Ingawa kaka zangu Richard na Dan wangekuwa wakichumia familia yetu fedha, wazazi wetu waliwatia moyo waende Brooklyn, New York, makao makuu ya Watch Tower Society kutumikia wakiwa wajitoleaji. Pia wazazi wetu walituwekea akiba ya fedha ili watano kati yetu waweze kusafiri New York kwa ndege kujionea makao makuu. Hilo lilinitia moyo sana. Liliongeza uthamini wetu kwa tengenezo la Yehova.

“Acha sasa nimpishe Baba aendelee na masimulizi haya.”

Tulipata Matatizo Pia

Kama ilivyo kawaida ya familia zote, tumepata matatizo na vivunja-moyo pia. Wavulana wetu walipofikia umri wa kufanya uchumba, ilinibidi kuwashauri dhidi ya kuharakisha kufunga ndoa na msichana wa kwanza kuwavutia. Pia tulihakikisha kuna mtu wa kuwachunga wakati wa uchumba. Tulitaka wapate uzoefu katika maisha kabla ya kuoa. Nyakati nyingine walilia na hata kupata huzuni ya muda mfupi, lakini baadaye walithamini hekima ya shauri la Biblia—hasa linalohusu kuoa “katika Bwana tu.” Tuliwapongeza kwa kutenda kwa hekima.—1 Wakorintho 7:39.

Scott, ambaye ni kitinda mimba wetu, alitufanya tulie. Alijiingiza katika mashirika mabaya kazini. Mwishowe, alitengwa na ushirika. Hilo lilikuwa pigo kubwa kwetu sote, ingawa hivyo tuliiheshimu hukumu iliyotolewa na wazee. Scott alijifunza somo gumu kwamba kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha.

Hatukukata tamaa kwamba siku moja atarudi kutanikoni. Kwa furaha, baada ya miaka mitano alirudishwa kutanikoni. Yeye akumbuka kwa kusema, “Jambo lililonisaidia nilipokuwa nimetengwa ni kujua kwamba familia yetu ilinipenda, hata ingawa ushirika na familia ulikuwa kidogo sana.” Scott alifanya maendeleo naye ametumikia akiwa mzee kwa miaka minane iliyopita.

Kwa kuhuzunisha, wajukuu wetu wawili walitengwa na ushirika katika miaka ya majuzi. Lakini sisi twatumaini kwamba nidhamu kutoka kwa Yehova yaweza kutokeza mabadiliko mazuri.

Badiliko Kubwa Katika Maisha Yetu

Mwishowe, kufikia mwaka wa 1978, wavulana wetu wote walikuwa wametoka nyumbani. Kwa miaka mingi, nilipata ujuzi wa kushughulika na vifaa vya kupasha joto na kupitisha hewa safi. Mwaka wa 1980, mimi na Margaret tulipata mwaliko wa kushangaza wa kutumikia kwa miezi tisa katika makao makuu ya Watch Tower Society yaliyoko Brooklyn. Kufikia sasa ni miaka 18, na tungali twatumikia hapa!

Tumepata baraka tele. Halikuwa jambo rahisi sikuzote kuwalea wana wetu kwa mtindo wa kizamani, ule wa kutumia kanuni za Biblia, lakini huo umetokeza mema kwetu. Hali ya sasa ya familia yetu ni kwamba watoto wetu watano wanatumikia wakiwa wazee kutanikoni, na mmoja ni mwangalizi asafiriye. Tuna wajukuu 20 na vitukuu 4—wengi wao wako katika kweli na ni waaminifu kwa Mungu.

Tumeona ukweli wa maneno ya mtunga-zaburi: “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA, uzao wa tumbo ni thawabu. Kama mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani.”—Zaburi 127:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., mwaka wa 1946; sasa hakichapishwi.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Tukiwa na wana wetu na wake zao (kulia) na wajukuu wetu pia (mbali kulia), mwaka wa 1996 tukiadhimisha mwaka wa 50 wa arusi yetu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki