Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Nisiwe Mwenye Urafiki Zaidi?
“Kuwa mwenye haya ni jambo linalofadhaisha. Ni hofu inayokushika kabisa unayohitaji kupambana nayo. Ni halisi kwelikweli.”—Richard.a
“Nilikuwa na tatizo la haya kwelikweli nilipokuwa nikikua. Ilikuwa kana kwamba nilikuwa katika ulimwengu wangu mwenyewe ulio mdogo.”—Elizabeth mwenye umri wa miaka 18.
‘JE, NINA kasoro fulani? Kwa nini nisiwe mwenye urafiki zaidi?’ Je, wewe hujiuliza maswali hayo nyakati fulani? Kama Richard aliyenukuliwa juu, huenda ukaona haya au wasiwasi unapokutana na mgeni. Huenda ukajikunyata unapokuwa katikati ya watu wenye mamlaka. Au labda una wasiwasi mwingi sana kuhusu jinsi watu wanavyofikiri juu yako hivi kwamba unapopewa nafasi ya kueleza hisia au maoni yako, unanyamaza kimya. “Mimi huona ugumu sana wa kuzungumza na watu nisiowajua vizuri,” akiri Tracey mchanga.
Ni nini kinachohusika katika hisia hizo? Hatua ya kwanza ya kushinda tatizo hilo ni kulielewa. (Mithali 1:5) Mwanamke mmoja alisema: “Sikujua kamwe kwa nini nilikosa kustarehe nilipokuwa katikati ya watu. Lakini sasa kwa kuwa nimetambua tatizo langu, naweza kulishughulikia.” Kwa hiyo acheni tuone sababu chache zinazofanya vijana fulani waone ugumu wa kuwa wenye urafiki.
Tatizo la Haya
Labda haya ndiyo sababu iliyo ya kawaida zaidi. Ingawa kijana mwenye urafiki kwa kawaida hufurahia urafiki wa namna nyingi, kijana mwenye haya, anayejitenga na watu anaweza kuhisi akiwa mpweke na kupuuzwa na watu. “Nilikuwa na tatizo la haya kwelikweli nilipokuwa nikikua,” asema Elizabeth mwenye umri wa miaka 18. “Ilikuwa kana kwamba nilikuwa katika ulimwengu wangu mwenyewe ulio mdogo.” Diane akumbuka mikazo aliyokabili katika mwaka wake wa kwanza kwenye shule ya sekondari. “Sikupenda kujulikana. Nilikuwa na mwalimu ambaye alituomba tukadirie namna tulivyohisi kuhusu umaana wa kupendwa. Kwenye kipimio cha sufuri hadi tano, sufuri ilimaanisha mtu asiye wa maana kabisa na tano ilimaanisha mtu wa maana. Wasichana wote waliopendwa shuleni walichagua tano. Nilichagua sufuri. Kwa upande wangu, haya ilikaribia kuwa hofu ya kupendwa. Hutaki kutambuliwa au kuelekezewa uangalifu kwa sababu unahofu huenda wengine wasikupende.”
Bila shaka, mwelekeo wa kuwa mwenye haya kidogo si mbaya kabisa. Haya inahusiana kwa ukaribu na kiasi—kutambua kupungukiwa kwetu. Kwa kweli tunaamriwa katika Biblia ‘twende kwa unyenyekevu na Mungu wetu.’ (Mika 6:8) Ni rahisi kuwa karibu na mtu mwenye kiasi au hata mwenye haya kwa njia fulani, kuliko mtu mwenye kiburi, mchokozi, au mwenye kudai. Na ingawa ni kweli kwamba kuna “wakati wa kunena,” pia kuna “wakati wa kunyamaza.” (Mhubiri 3:7) Watu wenye haya huenda wasiwe na tatizo la kunyamaza. Kwa sababu wanaelekea kuwa “wepesi sana juu ya kusikia [na] wa polepole juu ya kusema,” mara nyingi wanathaminiwa na wengine kuwa wasikilizaji wazuri.—Yakobo 1:19.
Hata hivyo, mara nyingi, kijana huwa kimya sana, mwenye haya, au mwoga sana hivi kwamba anakabili ugumu wa kutafuta marafiki. Na katika visa fulani vinavyopita kiasi, haya yaweza kutokeza hali ambayo mwandishi mmoja aiita “jela ya kibinafsi ya kukosa usawaziko wa kihisia-moyo”—kujitenga na jamii.—Mithali 18:1.
Haya—Tatizo la Kawaida
Ikiwa unakumbwa na haya, ng’amua kwamba hilo ni tatizo la kawaida sana. Katika uchunguzi mmoja uliofanyiwa wanafunzi wa shule ya sekondari na wa chuo, “asilimia 82 ya wanafunzi hao walijiona kuwa wenye haya wakati fulani maishani mwao.” (Adolescence, cha Eastwood Atwater) Haya ilikuwa tatizo hata kwa wengine katika nyakati za Biblia. Wanaume wakomavu, kama vile Musa na Timotheo, huenda walikabiliana nayo.—Kutoka 3:11, 13; 4:1, 10, 13; 1 Timotheo 4:12; 2 Timotheo 1:6-8.
Mfikirie Sauli, mfalme wa kwanza wa taifa la kale la Israeli. Kwa kawaida Sauli alikuwa mwanamume mjasiri. Baba yake alipopoteza kundi la wanyama, Sauli alitoka kwa ujasiri kwenda kuwaokoa. (1 Samweli 9:3, 4) Lakini alipowekwa kuwa mfalme wa taifa hilo, alipatwa na haya kwa ghafula. Badala ya kukabili umati mchangamfu, Sauli alijificha penye mizigo!—1 Samweli 10:20-24.
Huenda kukosa kujitumaini kwa Sauli kukashangaza. Hata hivyo, Biblia humfafanua kuwa mwanamume kijana mwenye kuvutia. Kwani, “tangu mabega yake kwenda juu alikuwa mrefu kuliko watu wote”! (1 Samweli 9:2) Isitoshe, nabii wa Mungu alikuwa amemhakikishia Sauli kwamba Yehova angebariki utawala wake akiwa mfalme. (1 Samweli 9:17, 20) Ijapokuwa hivyo, Sauli hakujitumaini. Alipoambiwa kwamba angekuwa mfalme, alijibu hivi kwa haya: “Je, mimi si Mbenyamini, mtu wa kabila iliyo ndogo kuliko kabila zote za Israeli? na jamaa yangu nayo si ndogo kuliko jamaa zote za kabila ya Benyamini? Kwa nini basi, kuniambia hivyo?”—1 Samweli 9:21.
Ikiwa mtu kama Sauli angekosa kujitumaini, haishangazi kwamba huenda ukakosa kujitumaini nyakati fulani. Maadamu wewe ni kijana, uko katika hatua ya maisha ambapo mwili wako unabadilika haraka-haraka. Unaanza kujifunza tu jinsi ya kutenda katika ulimwengu wa watu wazima. Kwa hiyo, ni jambo la asili tu kujifikiria kupita kiasi na kukosa usalama nyakati fulani. Dakt. David Elkind aliandika katika gazeti Parents: “Katika mwanzo-mwanzo wa kubalehe, vijana wengi hupitia kipindi chenye haya, wanapokuza kile ninachofikiria kuwa watazamaji wa kuwaziwa—itikadi ya kwamba wengine wanawatazama na wanajishughulisha sana na sura na matendo yao.”
Kwa kuwa mara nyingi vijana huhukumiwa na vijana wengine kwa kutegemea sura zao, wengi husumbuka kuhusu sura yao. (Linganisha 2 Wakorintho 10:7.) Hata hivyo, si jambo linalofaa kuhangaikia sana sura yako. Mwanamke mmoja kijana katika Ufaransa anayeitwa Lilia akumbuka jambo lililompata kuhusu habari hii: “Nilikuwa na tatizo ambalo vijana wengi wako nalo. Nilikuwa na chunusi! Huwezi kuthubutu kuwakaribia wengine kwa sababu una wasiwasi kuhusu sura yako.”
Tatizo Linaloendelea
Kwa sababu watu wenye haya mara nyingi hueleweka vibaya, wanaweza kunaswa kwa urahisi na mtego wa zoea la kujitenga na watu. Kitabu Adolescence chasema: “Wabalehe wenye haya wana tatizo kubwa zaidi la kutafuta marafiki kwa sababu mara nyingi wanaonwa na wengine kwa njia isiyofaa. Watu wenye haya huonwa kuwa wanaojitenga na watu, waliochoshwa, wasiopendezwa na wengine, wanaojishusha, wasio na urafiki, na wenye uhasama. Wanapotendewa kwa njia hiyo hiyo, huenda wakahisi kuwa wametengwa hata zaidi, wakiwa wapweke, na kushuka moyo.” Bila kuepukika, jambo hilo huwafanya wajiendeshe wakiwa na haya hata zaidi, jambo ambalo bila shaka, huimarisha maoni yasiyofaa ya kwamba wao hupuuza watu au kwamba wao hujiona kuwa wa maana sana.
Bila shaka, kwa kuwa ukiwa Mkristo unakuwa “kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa ulimwengu,” unapaswa kuhangaikia wazo ambalo wengine hupata wanapokutazama. (1 Wakorintho 4:9) Je, wewe huepuka kuwasiliana na wengine ana kwa ana? Je, mkao wako na ishara zako za mwili hutoa wazo la kwamba hutaki kusumbuliwa? Basi ng’amua kwamba huenda wengine wakakuelewa vibaya na kujiepusha nawe. Jambo hilo laweza kufanya iwe vigumu hata zaidi kusitawisha urafiki.
Mambo Mengine
Lakini tatizo jingine la kawaida ni hofu ya kutofaulu. Ni kweli kwamba ni kawaida kabisa kuhisi ukosefu wa usalama kwa kiasi fulani au kusitasita unapofanya jambo jipya, ambalo hujalizoea. Lakini vijana wengine hupita kiasi kwa habari hiyo. Alipokuwa kijana, Gail alikuwa na ile anayoiita hofu ya watu. Asema: “Singetoa maelezo yoyote darasani. Na wazazi wangu walikuwa wakiambiwa daima mambo kama vile, ‘Hanyoshi mkono wake. Hajielezi.’ Nililiona kuwa jambo lisilostarehesha na lenye mkazo. Unajua hata sasa, bado ni vigumu kwangu.” Hofu ya kutofaulu yaweza kufadhaisha. “Nina wasiwasi wa kufanya makosa,” asema kijana anayeitwa Peter. “Kwa kweli sina hakika na mambo ninayofanya.” Utani wa kinyama na kuchambuliwa na marika kwaweza kuchochea hofu za kibinafsi na kusababisha madhara ya kudumu kwa hali ya kijana ya kujitumaini.
Kukosa stadi za kijamii ni tatizo jingine la kawaida. Labda unasita-sita kujijulisha kwa mgeni fulani, kwa sababu tu hujui la kusema. Huenda ukashangaa kujua kwamba hata watu walio na umri mkubwa zaidi huona haya wanapokuwa kati ya watu nyakati nyingine. Mfanyabiashara mmoja anayeitwa Fred asema: “Katika ulimwengu wa biashara, ninajua jinsi ya kufanya jambo ambalo mimi hulifanya vizuri kabisa. Ikiwa ninaongea tu kuhusu biashara sina shaka yoyote kuhusu kutoa wazo linalofaa. Lakini ninapoanza mazungumzo ya kirafiki na watu walewale, ninasita-sita. Huenda nikajulikana kuwa mwenye kuchosha au mwenye maneno mengi au mwenye kutumia maneno magumu au asiyependeza sana.”
Hata iwe una haya, unajifikiria, au si mwenye urafiki tu, utapata faida kwa kujifunza jinsi ya kuwa mwenye urafiki zaidi. Biblia huwatia moyo Wakristo ‘wapanuke’ na wapate kuwajua wengine! (2 Wakorintho 6:13) Lakini unaweza kufanyaje hivyo? Jambo hilo litazungumziwa katika toleo la wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mara nyingi watu wenye haya huonwa kuwa wanajitenga na watu
[Picha katika ukurasa wa 26]
Hofu ya kutofaulu hufanya vijana fulani wajitenge na watu