Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 12/22 kur. 13-16
  • Tumaini Limenitegemeza Kuvumilia Majaribu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tumaini Limenitegemeza Kuvumilia Majaribu
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwanzo wa Majaribu Yetu
  • Kuishi na Wazazi Wangu
  • Nategemezwa na Tumaini
  • Wanangu Ni Chanzo cha Shangwe
  • Huduma Yetu ya Wakati Wote
  • Nimetegemezwa na Baraka Nyingi
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
  • Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Yehova Huwavuta Wanyenyekevu Kuijua Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 12/22 kur. 13-16

Tumaini Limenitegemeza Kuvumilia Majaribu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MICHIKO OGAWA

Katika Aprili 29, 1969, nilipokea simu kutoka kwa polisi. Mume wangu Seikichi, alikuwa amelazwa hospitalini kutokana na majeraha aliyopata katika aksidenti ya gari. Niliwaacha wanangu wawili wachanga kwa rafiki yangu kisha nikaenda hima hospitalini. Tangu wakati huo Seikichi amepooza na hajapata tena fahamu. Acheni niwaeleze juu ya familia yetu na jinsi ambavyo tumemudu hali.

NILIZALIWA mnamo Februari 1940 huko Sanda, karibu na Kobe, Japani. Mimi na Seikichi tumefahamiana tangu tulipohudhuria shule ya watoto wadogo pamoja. Tulifunga ndoa katika Februari 16, 1964. Mume wangu hakuwa mzungumzaji, lakini alipenda watoto. Baada ya muda, tulipata wavulana wawili, Ryusuke na Kohei.

Seikichi aliajiriwa na kampuni moja ya ujenzi huko Tokyo, kwa hiyo baada ya kufunga ndoa tuliishi katika mojawapo ya viunga vya Tokyo. Katika Oktoba 1967, nilitembelewa na mwanamke mmoja kijana aliyejitambulisha kuwa mwalimu wa Biblia. “Pole sana. Nina Biblia yangu,” nikasema.

“Naweza kuiona Biblia hiyo?” akaniuliza.

Niliichukua Biblia kutoka kwenye rafu yetu ya vitabu—ilikuwa ya Seikichi—nikampa. Alinionyesha jina Yehova katika Biblia hiyo. Sikujua kamwe kwamba hilo lilikuwa jina la Mungu. Mwanamke huyo alipowaona watoto wangu wawili wachanga, alinisomea hivi kutoka kwenye Biblia: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Kwa kweli nilikuwa nikihangaika jinsi ambavyo ningeweza kuwalea wanangu kwa mafanikio. Kwa hiyo mara moja nilitaka kujifunza Biblia.

Nilimkaribisha mwanamke huyo chumbani, kisha tukaanza kuzungumzia kijitabu “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya.” Nilifikiria, ‘Ingekuwa bora kama nini ikiwa sote tukiwa familia tungeweza kuonea shangwe maisha yenye furaha!’ Seikichi alipowasili nyumbani, nilimwambia: “Nataka kujifunza Biblia.”

“Mpenzi, huhitaji kuelimika sana,” akasema. “Nitakufunza jambo lolote lile unalotaka kujua.” Hata hivyo, nilianza kujifunza Biblia kila juma na Mashahidi wa Yehova na punde si punde nikaanza kuhudhuria mikutano yao.

Mwanzo wa Majaribu Yetu

Nilipowasili hospitalini usiku huo wa Aprili 1969 niliotaja mwanzoni, nilishtuka niliposikia kwamba rafiki ya Seikichi, mume wa mwanamke niliyemwachia wanangu, alikuwa pia katika teksi hiyo ilipopata aksidenti. Rafiki ya mume wangu alikufa juma moja baadaye.

Usiku huo wauguzi wa hospitali waliniambia nimwite kila mtu ambaye nilifikiri angepaswa kumwona Seikichi, kwa kuwa angekufa. Fuvu lake la kichwa lilikuwa limevunjika shinani na damu ilivuja ubongoni. Siku iliyofuata watu wa ukoo wanaoishi eneo la Kobe waliwasili hospitalini upesi-upesi.

Mara tangazo likapitishwa hima-hima kwa kikuza sauti: “Watu wote wa ukoo wa Seikichi Ogawa, tafadhali mtembeleeni mara moja.” Tulienda haraka-haraka katika chumba cha wagonjwa mahututi na tukamuaga kwa zamu. Hata hivyo, alibaki mahututi kwa mwezi mzima. Uchunguzi wa mwisho ulionyesha kwamba angekuwa mahututi kwa muda mrefu.

Kwa hiyo Seikichi alihamishwa kwa ambulansi kutoka Tokyo hadi Kobe, umbali wa kilometa zipatazo 650. Nilielekea nyumbani kwa treni ya kasi baada ya kumuaga, huku nikisali apone. Baadaye jioni, nilifurahi sana kumwona akiwa hai hospitalini huko Kobe. Nikamnong’onezea hivi, ‘Mpenzi, uliendelea kuishi!’

Kuishi na Wazazi Wangu

Nilirejea na wanangu nyumbani kwa wazazi wangu huko Sanda, ambako walijiunga na shule ya watoto wadogo. Nilinunua tiketi ya muda ya kusafiri kwa treni hadi Kobe, umbali wa kilometa 40 hivi, mimi na mama-mkwe wangu tulisafiri kwa zamu kila siku kwa mwaka mzima uliofuata kumzuru hospitalini. Ningefikiria, ‘Je, Seikichi atapata fahamu leo? Ataniambia nini kwanza? Nijibuje?’ Hasa nilipoona familia iliyoonekana kuwa na furaha ningefikiria, ‘Laiti Seikichi angekuwa mzima, wana wetu wangefurahi sana.’ Hapo machozi yalitiririka machoni mwangu.

Miaka hiyo ya mapema, niliposoma magazetini kwamba mtu fulani alipata fahamu tena baada ya kuzimia kwa miezi kadhaa, ningefikiri kwamba huenda Seikichi pia atapata fahamu tena. Pindi moja nilimwambia shemeji yangu: “Nataka kumpeleka katika hospitali iliyoko kaskazini-mashariki mwa Honshu.” Lakini aliniambia kwamba hakuna ponyo, na akanishauri nitumie fedha tulizoweka akibani kwa ajili ya washiriki wengine wa familia.

Mzee mmoja Mkristo katika mojawapo ya makutaniko ya Kobe ya Mashahidi wa Yehova aliishi karibu na hospitali hiyo, ningepitia nyumbani kwake kabla ya kumzuru Seikichi. Mke wake alinifunza Biblia mara moja kwa juma. Na wana wao wawili wangekuja kwenye chumba chetu hospitalini ili kuleta kaseti ya mrekodio wa mikutano yao ya kutaniko. Familia hii ilinitia moyo sana na kunifariji.

Nategemezwa na Tumaini

Siku moja, mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova alituzuru hospitalini na akanisomea Waroma 8:18-25. Lasema hivi kwa sehemu: “Nahesabu kwamba mateso ya majira yaliyopo si kitu kwa kulinganisha na utukufu utakaofunuliwa katika sisi. . . . Kwa maana twajua kwamba viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa. . . . Maana mtu aonapo kitu, je, hukitumainia? Lakini tukitumainia kile tusichoona, twafuliza kukingojea kwa uvumilivu.”

Mazungumzo hayo juu ya tumaini letu la Kikristo yalinikumbusha kwamba mateso ya sasa si kitu yanapolinganishwa na shangwe inayoahidiwa na Yesu—uhai katika dunia Paradiso inayokuja. (Luka 23:43) Mazungumzo hayo yalinisaidia kukabili mambo halisi yaliyopo nikiwa na tumaini na kukazia fikira mambo halisi ya wakati ujao ya baraka katika ulimwengu mpya.—2 Wakorintho 4:17, 18; Ufunuo 21:3, 4.

Katika Juni 1970, Seikichi alihamishwa hadi hospitali moja huko Sanda, nilikoishi na wazazi wangu. Mwezi uliofuata wa Januari, nilihuzunika sana na kulia machozi nilipopokea hati kutoka kwa wakili wetu iliyojulisha rasmi kwamba mume wangu hajiwezi kwa sababu ya aksidenti. Mama-mkwe wangu aliniambia hivi mara nyingi: “Pole sana, Michiko kwa sababu ya wakati mgumu ulio nao kwa ajili ya mwanangu.” Angesema pia: “Laiti ningeweza kuchukua mahali pa Seikichi.” Tungelia sote.

Baba yangu alinisihi nitafute kazi ya wakati wote, lakini niliazimia kumtunza Seikichi. Ingawa alionekana akiwa amezimia, alitambua hali ya joto na baridi na aliathiriwa na namna alivyotunzwa. Baba alitaka niolewe na mume mwingine, lakini nilitambua kwamba haingefaa kufanya hivyo, kwa kuwa mume wangu alikuwa angali hai. (Waroma 7:2) Baada ya hapo, Baba alipolewa angesema: “Nitakufa pamoja na Seikichi.”

Nilikuwa na shangwe sana mnamo 1971 kutaniko lilipoanzishwa katika Sanda. Nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa majini katika Julai 28, 1973. Hilo lilitukia wakati wa mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika Uwanja wa Osaka wa Maonyesho ya Kimataifa.

Baadaye mwaka wa 1973, mwanangu Kohei alishikwa na uvimbe mbaya wa mafigo na akalazwa hospitalini kwa miezi mitano. Baba yangu alilazwa pia hospitalini kwa sababu aliugua kifua kikuu. Kwa hiyo katika Januari 1, 1974, nilimtembelea baba yangu, mume wangu, na mwanangu katika hospitali tatu mbalimbali. Siku ya Jumapili nilipoenda na mwanangu wa kwanza Ryusuke kumwona Kohei, nilijifunza nao kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Baada ya hapo, mimi na Ryusuke tulihudhuria mkutano katika Kobe na tulirejea nyumbani tukiwa wenye shangwe mioyoni.

Sikuzote mimi huwashukuru wale walionisaidia kumtunza Seikichi. Niliazimia kushiriki nao ujuzi wa Biblia. Mtunzi mmoja aliitikia vizuri nilipomwonyesha tumaini tukufu la ufufuo linaloahidiwa katika Biblia baada ya kumpoteza dadake kwenye kisa cha moto. (Ayubu 14:13-15; Yohana 5:28, 29) Alikubali funzo la Biblia akiwa hospitalini, na hatimaye akabatizwa kwenye mkusanyiko mnamo 1978.

Wanangu Ni Chanzo cha Shangwe

Kazi ya kuwalea wanangu pasipo msaada wa mume wangu imekuwa ngumu, lakini yenye kuthawabisha kama nini! Niliwafunza kuwa na adabu nzuri na kujali hisia za wengine. Ryusuke alipokuwa na umri wa miaka mitatu tu, alikuwa akiomba radhi kwa ajili ya utovu wake wa adabu, angesema: “Pole Mama.” Kohei aliasi pindi kwa pindi, nyakati nyingine alikasirika nilipojaribu kumsahihisha. Pindi moja alipotaka nimnunulie kitu fulani alilala sakafuni mbele ya duka moja huku akilia. Lakini nilisababu naye, na kumwonyesha shauku nikiwa mwenye subira. Baada ya muda, akawa mtiifu, kijana mzuri. Jambo hilo lilinisadikisha kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu.—2 Timotheo 3:15-17.

Ryusuke alipojiunga na kidato cha tatu katika shule ya sekondari, aliwaeleza walimu kwa nini hangeweza kufanya mazoezi ya karate. (Isaya 2:4) Siku moja, alirejea nyumbani kutoka shuleni akiwa mwenye shangwe nyingi kwa sababu aliweza kujibu maswali yaliyozushwa na walimu kadhaa katika mkutano fulani.

Ushirika wenye kujenga kutanikoni uliwasaidia sana wanangu. Mara nyingi wazee Wakristo waliwaalika kwa mlo wa jioni na kuwakaribisha kwenye funzo la Biblia la familia zao na tafrija vilevile. Kulikuwa pia na fursa za kufurahia ushirika wenye kupendeza, kutia ndani kushiriki michezo mbalimbali. Ryusuke alionyesha wakfu wake kwa Yehova kwa kuzamishwa majini mnamo 1979, na Kohei akabatizwa mwaka uliofuata.

Huduma Yetu ya Wakati Wote

Wakati mmoja nilimwambia mwangalizi asafiriye aliyetuzuru kwamba nilitaka kuwa painia, kama waitwavyo wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa wakati huo halingekuwa jambo la hekima kupainia kwa sababu ya hali zangu, alinikumbusha kwa fadhili uhitaji wa kuwalea wanangu kwa uthabiti katika kweli ya Biblia. “Jambo la muhimu,” akasema, “ni kudhihirisha roho ya painia.” Kwa hiyo nikawa painia msaidizi, nikishiriki utendaji huo pamoja na wanangu wakati wa likizo ya shule. Upainia ulinisaidia sana kudumisha shangwe na amani ya akili nilipokuwa nikimtunza Seikichi.

Hatimaye, niliweza kuwa painia wa kawaida katika Septemba 1979. Ryusuke pia akawa painia katika Mei 1984, mwaka mmoja baada ya kufuzu katika shule ya sekondari. Kohei akajiunga naye katika kazi ya upainia mwezi wa Septemba 1984. Hivyo, sote watatu tumefurahia huduma hii ya wakati wote. Ninapokumbuka zaidi ya miaka 20 ambayo nimekuwa painia, wakati ambao nimekuwa na pendeleo la kuwasaidia watu kadhaa kuja kumtumikia Yehova, nahisi kwamba utendaji huu umenisaidia kuvumilia majaribu yangu.

Ryusuke alijitolea kufanya kazi katika ujenzi wa jengo litakalotumiwa na Mashahidi wa Yehova karibu na Jumba la Kusanyiko la Kansai. Baadaye akawa msimamizi wa Jumba la Kusanyiko la Hyogo kwa miaka saba. Sasa yeye hunitunza akiwa mzee Mkristo katika kutaniko lililo karibu la hapa Kobe. Tangu mwaka wa 1985, Kohei amekuwa akitumikia akiwa mjitoleaji katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Ebina.

Nimetegemezwa na Baraka Nyingi

Kwa miaka mingi nilienda hospitalini mara kadhaa kwa siku kumtembelea na kumwosha Seikichi. Mbali na utunzi wangu, alitunzwa pia na mtunzi mwingine wa kawaida. Seikichi alirejeshwa nyumbani katika Septemba 1996 kwa msaada wa mtunzi, baada ya kuwa hospitalini kwa miaka 27. Yeye hutumia vyakula vioevu kupitia kwa neli iliyo puani. Ijapokuwa macho yake yamefunga tu, yeye huitikia kidogo tunapomwambia jambo. Mimi huhisi uchungu ninapomwona Seikichi akiwa katika hali hii, lakini ninategemezwa na tumaini tukufu la wakati ujao.

Punde tu kabla ya Seikichi kurudi, nilikuwa nimemwandalia mwangalizi asafiriye na mkewe mahali pa kuishi, na kwa mwaka mmoja tuliishi pamoja watu watano katika nyumba yetu ndogo. Sikudhani kamwe kwamba ningepata kuishi tena na Seikichi, namshukuru Yehova kwa ajili ya jambo hilo. Kwa miaka mingi nilitamani sana kumwona Seikichi akifungua macho yake, lakini sasa natamani tu kwamba mapenzi ya Yehova yatendeke.

Kwa kweli naweza kusema hivi: “Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.” (Mithali 10:22) Licha ya kwamba maisha yenye furaha pamoja na Seikichi aliyekuwa mzima yalikatishwa, nimebarikiwa kuwa na wana wawili ambao ‘wamemkumbuka Muumba wetu Mtukufu.’ Nashukuru sana kwa ajili ya jambo hilo!—Mhubiri 12:1.

Kwa sasa, ningependa kuendelea kupainia—na hivyo kuwasaidia wengine wapate “uhai ulio halisi”—na wakati huohuo, nimtunze Seikichi kwa njia ya upendo. (1 Timotheo 6:19) Mambo yaliyonipata yamenifunza ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza. Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”—Zaburi 55:22.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa na mume wangu na Ryusuke

[Picha katika ukurasa wa 13]

Seikichi akiwa na wana wetu wawili, miezi sita kabla ya aksidenti

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tulibarikiwa kupata wana wawili, Ryusuke na Kohei (juu), ambao ‘wamemkumbuka Muumba wetu Mtukufu’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki