Maoni Yetu ya Wakati Ujao
Unabii wa Biblia unaogeuza sana maoni yetu juu ya maisha ni ule unaopatikana katika Ufunuo 21:3, na 4. Unasema hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja [na wanadamu]. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”
Biblia inaeleza mara nyingi ulimwengu bora ambao Mungu atafanya. “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13, New World Translation; Zaburi 37:9-11, 29; Isaya 11:6-9; 35:5, 6.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba njia moja tu ya kuondoa matatizo ya wanadamu ni utimizo wa ahadi hiyo. Ni kama Yesu alivyoonyesha alipofundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Sisi tunaamini kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi. (Isaya 9:6, 7) Ndiyo serikali pekee inayoweza kuondoa hali zote zinazofanyiza taabu ya kibinadamu zitoke katika dunia, kisha ilete amani ya milele.
Unabii mwingine wa Biblia unaeleza kitakachozipata serikali zote za sasa wakati wa kuja kwa Ufalme wa Mungu: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Kwa kuwa sisi tunasadikishwa kwamba badiliko hilo liko karibu sana, watoto wetu wanaamini inafaa kujiweka tayari kwa ajili ya kazi ya maisha inayopatana na imani yetu ya kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi. Shabaha yetu kuu ni kuwaambia watu juu ya wakati ujao wenye tumaini zuri. Kwa hakika sisi tunatazamia kuondolewa kwa huzuni na taabu za sasa kisha tuokoke tuzifurahie baraka ambazo Mungu amewekea akiba wale wanaomtumikia. Ahadi hakika ya Mungu ni: “Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadamu milele.”—1 Yohana 2:17, New World Translation.
Waliojitenga na Ulimwengu
Kama unavyoweza kutazamia, pia maoni hayo juu ya wakati ujao yaligeuza sana Wakristo wa kwanza. Yaliwafanya wawe watu tofauti, waliojitenga na ulimwengu. Ni kama mwanahistoria E. G. Hardy alivyoeleza katika kitabu chake Christianity and the Roman Government: “Wakristo walikuwa wageni na wapitaji katika ulimwengu uliowazunguka; uraia wao ulikuwa mbinguni; ufalme ambao walitazamia haukuwa wa ulimwengu huu. Hivyo kutopendezwa na mambo ya wingi wa watu kunakostahili kuwa sehemu yenye kuangaliwa katika Ukristo kulitokea tangu mwanzo wenyewe.”
Yesu alionyesha wazi kwamba kujitenga kwao na ulimwengu kungekuwa tabia yenye kutokeza ya wanafunzi wake. “Wao si sehemu ya ulimwengu,” akasema. (Yohana 17:16; 15:19, New World Translation) Kupatana na kanuni hiyo, Mashahidi wa Yehova wanajaribu kutokuwa “sehemu ya ulimwengu.” Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba sisi tunaunga mkono hali ya watu wenye kukaa peke yao katika nyumba za utawa, wakijifungia ndani mbali na ulimwengu. Sisi tunapendezwa kwa unyofu wa moyo na hali njema ya wengine katika jumuiya na katika shule. Watoto wetu wanataka kushiriki kuleta manufaa ya masomo ya darasani.
Lakini, vilevile sisi tunaamini Biblia inasema waziwazi kwamba “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19; 12:31; 2 Wakorintho 4:4, New World Translation) Kwa sababu hiyo, sisi tunahangaikia matokeo mabaya yanayoweza kuletwa na uvutano wa ulimwengu juu ya watoto wetu. Mara nyingi ulimwengu unafanya mitindo ya maisha tunayoamini kuwa mibaya ionekane kuwa yenye kupendeza macho. Hata shule zimepatwa na uvutano huo. Hivyo, Mashahidi wa Yehova wanataka watoto wao waepuke mavutano hatari hayo kwa kadiri inavyowezekana.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Ulimwengu unapita . . . lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17, New World Translation