Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 24 kur. 183-189
  • Wakati Uliowekwa Hatari Ianze Umekaribia Kumalizika!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati Uliowekwa Hatari Ianze Umekaribia Kumalizika!
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MATUKIO AMBAYO BADO YAKO MBELE
  • WAINGIZWA KATIKA “DUNIA MPYA” ILIYO BORA SANA
  • Amani Kutoka kwa Mungu Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • “Amani na Usalama!”—Halafu “Uharibifu wa Ghafula”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Jinsi Ufalme huo ‘Unakuja’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Uharibifu wa Ulimwengu Uliotabiriwa Utakuja Lini?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 24 kur. 183-189

Sura 24

Wakati Uliowekwa Hatari Ianze Umekaribia Kumalizika!

1. Kulignana na wanasayansi mashuhuri, “siku ya maangamizi” ni karibu sana kadiri gani?

HUKO nyuma mwaka wa 1947, wanasayansi walibuni “saa ya siku ya maangamizi.” Inaonekana katika jalada la kichapo The Bulletin of the Atomic Scientists na inatumiwa kukazia wazi jinsi wao wanaamini ulimwengu ulivyo karibu sana na hatari ya kupatwa na maangamizi ya kinyukilia. Mara nyingi mikono ya “saa” hiyo imesogezwa—mara nyingine mbele, mara nyingine nyuma, ikitegemea jinsi hali ya mataifa yote ilivyoonwa kuwa yenye hatari. Mapema mwaka wa 1984 mikono hiyo ilisogezwa mbele dakika tatu kabla ya usiku wa manane. Ikiwa mikono hiyo ingefika usiku wa manane, ingekuwa na maana kwamba vita ya nyukilia inayoogopwa sana ingekuwa imeanza.

2. Yehova alianza kuweka wakati wake lini, na kumalizika kwao kutakuwa na maana gani?

2 Lakini ilikuwa miaka kama 6,000 iliyopita wakati Yehova Mungu alipoanza kuweka wakati ambao umesonga mbele bila kuzuiwa, usirudi nyuma kamwe. Katika saa hiyo iliyowekwa, ukomo ni wakati ambao Mungu ameweka ili enzi kuu yake itetewe, enzi ambayo amani na hali njema ya ulimwengu mzima wote inategemea. Yeye amesema waziwazi kusudi lake na ametoa alama za wakati zinazotuwezesha kufahamu unavyoendelea. Mara baada ya uasi uliotukia katika Edeni, Yehova aliahidi kwamba angetokeza kwa “mwanamke” wake, tengenezo lake la viumbe vya kiroho, “uzao” ambao ungemponda kichwa Shetani, “nyoka wa zamani,” na mwishowe umwangamize kabisa asiwepo milele. (Mwanzo 3:15; Ufunuo 12:9; Warumi 16:20) Wapendao uadilifu wanatamani sana wakati huo kama nini!

3. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba wakati wa kuja kwa Masihi ulihesabiwa kwa uangalifu? (b) Ni nini kilichowekewa msingi wakati huo?

3 Kwa wakati uliowekwa na Mungu, uliotangulia kutabiriwa zamani, “uzao” huo ulioahidiwa, yule Masihi, Mwana wa Mungu mwenyewe, akatokea duniani. Likiwa jibu lenye mvumo wa kuenea kote kote la shtaka lenye ukaidi, Yesu alidumisha utawa mkamilifu mpaka kufa. Na kwa kufa akiwa binadamu asiye na dhambi alitoa pia njia ya kukombolea watoto wa Adamu katika dhambi na kifo. Kwa njia hiyo msingi uliwekwa ili mwishowe ‘kazi za Ibilisi zije zivunjwe.’—1 Yohana 3:8; Danieli 9:25; Wagalatia 4:4, 5.

4. (a) Ni kikundi gani ambacho Yesu alianza kukusanya alipokuwa hapa duniani? (b) Kupatana na ratiba ya kimungu, Kristo alianza lini kutawala akiwa Mfalme? (c) Ni hatua gani ya kwanza aliyochukua?

4 Yesu alipokuwa angali duniani, alianza kukusanya wanaume na wanawake ambao wangekuwa warithi washirika pamoja naye katika ufalme wa kimbingu. Watu ambao wangetiwa humo ni 144,000 tu waliochaguliwa, wakajaribiwa na walio washikamanifu. Ulipofika wakati wa kuwakusanya washiriki wa mwisho wa kikundi hicho, “mamlaka, na utukufu, na ufalme” alipewa Yesu mwenyewe mbinguni. (Danieli 7:13, 14) Ulipotimia wakati barabara, mwaka wa 1914, akaanza kutawala akiwa Mfalme. Shetani na mashetani wake walivurumishwa mara hiyo watoke mbinguni, tendo hilo likasafisha makao ya serikali. (Ufunuo 12:7-12) Mfumo wa ulimwengu wa sasa ukawa umeingia katika siku zake za kumalizia.

5. Nani watakaokuwa hai ili wajionee kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova?

5 Wakati ambao umekuwa ukihesabiwa kwa muda wa miaka 6,000 sasa umekaribia kumalizika. Ni karibu sana hata watu waliokuwa hai mwaka wa 1914, na ambao sasa ni wazee wa miaka, hawatakwisha wote kabla ya kutimia matukio yenye kusisimua, ambayo yatatia alama ya kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova.—Marko 13:30.

6, 7. (a) Ni mambo gani ya hakika juu ya “mkutano mkubwa” yanayoonyesha kwamba ni lazima dhiki kubwa iwe iko karibu sana? (b) Kwa nini wanatazamia wakati ujao kwa shauku sana?

6 Watumishi wengine wa Mungu walio washikamanifu, pia, watakuwapo ili wayaone matukio ya siku hiyo iliyo kuu. Hasa kuanzia mwaka wa 1935, wakati “mkutano mkubwa,” au “umati mkubwa” ulipotambuliwa na kufahamiwa waziwazi, hesabu kubwa za hao zilianza kujitokeza. Kwanza walikuwa mamia, ndipo maelfu, baadaye mamia ya maelfu, na sasa kuna mamilioni walioenea kuzunguka dunia yote. Neno la Mungu lisilokosea linakisimulia kikundi hicho kuwa ‘kikitoka katika dhiki kubwa,’ wakiwa waokokaji wayo, wakiendelea kuishi na kuingia katika Utaratibu Mpya bila kuwa na lazima ya kufa wakati wo wote. (Ufunuo 7:9, 10, 14; Yohana 11:26) Washiriki wa kwanza wa kikundi hicho sasa ni wenye umri wa miaka 60 na kitu au 70 na kitu au zaidi ya hiyo. Yehova hakuruhusu kukusanywa kwa kikundi hicho kuanze upesi mno. “Mkutano mkubwa,” kutia na wengi wa washiriki wao wa mapema sana, utaokoka uingie katika “dunia mpya.”

7 Tumaini la “mkutano mkubwa” halitazuiwa na maangamizi ya nyukilia yo yote ambayo yangeangamiza wanadamu wote. Wakiwa na sababu nzuri ni wenye matumaini mazuri na ni wajasiri. Wakati matukio ya “siku za mwisho” yamekuwa yakitokea, wameyatazama kwa shauku sana, wakilitumia shauri hili la Yesu kuwa likiwahusu wao: “Mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Lakini katika wakati unaobaki kabla ya ukombozi huo, matukio zaidi yenye umaana wa kutikisa ulimwengu yanatazamiwa kutukia.

MATUKIO AMBAYO BADO YAKO MBELE

8. (a) Ni tukio gani lenye kutokeza sana lililotabiriwa katika 1 Wathesalonike 5:3 ambalo bado linakuja? (b) Miaka mingi iliyopita, hali ya jambo hilo kutokea iliwekwaje? (c) Miaka ya majuzi, ni mkazo gani mkubwa ambao umekuwapo ili kuhakikisha kuna amani ya ulimwengu?

8 Akielekeza kwenye mojapo matukio hayo, mtume Paulo aliandika hivi: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 Wathesalonike 5:3) Jinsi tangazo hilo litakavyokuwa, ni jambo linalobaki kuonwa. Lakini inafaa kuangaliwa kwamba hali hiyo iliwekwa upesi baada ya ulimwengu kuingia katika “siku za mwisho.” Mwaka wa 1919 kusudi la Ushirika wa Mataifa lilitangazwa kuwa ni kuleta “amani na usalama.” Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, ile Katiba ya Umoja wa Mataifa iliweka tena “amani na usalama” kuwa ndio mradi mkuu wa shirika hilo la mataifa yote. Haujatimiza lengo hilo. Ingawa hivyo, miaka ya majuzi watu wa namna zote za maisha wameshiriki maandamano makubwa mno ya peupe katika nchi nyingi, wakiwaomba sana viongozi wa ulimwengu waache uundaji wote wa silaha za nyukilia, waache kuzilipua katika kujaribia na waache kuziweka tayari kushambulia. Wanataka uhakikisho wa amani ya ulimwengu na wanaogopeshwa na kile wanachoamini kitatokea ikiwa hatua za amani hazichukuliwi.

9. Kwa nini uharibifu wa ghafula utakuja juu ya wale watakaotia saini ya tangazo hilo lililotabiriwa la “amani na salama”?

9 Kwamba ni matokeo ya hilo au kwamba ni kwa hatua fulani nyingine yao, karibuni viongozi wa kibinadamu watafanya tangazo la “amani na salama” lenye kutokeza jambo kubwa! Itakuwa ni udanganyifu tu. Lakini wale watakaolitilia saini (sahihi) watakuwa wakitangaza kwamba wameufikia mradi wao kwa njia yao wenyewe, pasipo kuuhitaji Ufalme wa Mungu. Wakati watakapoikataa kuwa haifai kitu enzi kuu ya Yehova, ‘ndipo uharibifu utakapowajia kwa ghafula.’

10. Tayari hali ya kuangamizwa kwa Babeli Mkuu imeanzaje kutukia?

10 Matukio yatasonga upesi sana. Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, itaharibiwa na vipenzi vyake vya zamani vya kisiasa. Tayari, watawala wamejua sana kwamba dini ni nguvu yenye kuchochea ambayo imetokeza uchukivu, umwagaji wa damu na vita kuzunguka dunia yote. Wanasiasa wanaendelea kuchoshwa na mkazo wa viongozi wa dini. Katika sehemu nyingi za ulimwengu, hudhurio mahali pa kuabudia limepungua sana. Watu wengi wanaongozwa na maoni ya kutoamini kuwako kwa Mungu, iwe kwa kelele ya majivuno au kwa siri. Pia, nchi nyingi zilizo wanachama wa Umoja wa Mataifa zina maongozi makali yenye kupinga dini. Utakapofika wakati wa Yehova mwenyewe uliowekwa ili atekeleze hukumu, atawaruhusu watawala wa kisiasa, wakiwa wameungana mataifa yote, waigeukie Babeli Mkuu na kuiangamiza kabisa.—Ufunuo 17:15, 16; 19:1, 2.

11. (a) Watakaofuata kushambuliwa na mataifa ni akina nani? (b) Na hilo litaongoza kwenye matukio gani zaidi?

11 Kwa sababu ya kulewa ushindi na kusukumwa na Shetani Ibilisi, mtawala wao asiyeonekana, ndipo mataifa yatakaposhambulia mashahidi waaminifu wa Yehova mwenyewe duniani. (Ezekieli 38:14-16) Uhakika wa kwamba hao ni watu wenye amani na wenye kutii sheria na wasiojiingiza katika siasa wala hawana lawama la kuchochea vita hautafikiriwa. Mataifa hayo yatadai yaungwe mkono kabisa, yatadai mfumo wa kisiasa uabudiwe kabisa. Lakini watakapochukua hatua ya kutaka kuliharibu tengenezo lionekanalo la Yehova, Mungu atachukua hatua ya kukata maneno kwa ajili ya watumishi wake washikamanifu, awaokoe. Majeshi ya mbinguni yataangamiza kabisa kila sehemu itakayosalia ya tengenezo lionekanalo la Shetani, yawaharibu wote wanaoling’ang’ania. Ndipo, yule adui mkuu, Shetani Ibilisi mwenyewe, atabambwa na kuzuiwa kabisa asitende kazi kwa miaka elfu moja. Wakati huo matokeo yote ya uvutano wake mbaya sana yataondolewa kabisa kisha dunia igeuzwe kuwa Paradiso. Baada ya hapo, Shetani atafunguliwa kwa muda mfupi, aje ajaribu wanadamu waliokamilishwa. Wanadamu wote watakaochagua kumfuata wataangamizwa, pamoja na Shetani na mashetani wake.—Ufunuo 19:19-21; 20:1-3, 7-10.

WAINGIZWA KATIKA “DUNIA MPYA” ILIYO BORA SANA

12. (a) “Mkutano mkubwa” utahesabia nani wokovu wao? (b) Ni nani watakaojiunga nao katika kumsifu Mungu?

12 Matukio yenye kutia woga ya mwisho wa ulimwengu wa sasa yatakapokuwa yameachwa nyuma yao, na Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo ukiwa mbele yao, waokokaji wenye kupendelewa duniani watajawa na shukrani nyingi watakapoziinua sauti zao kwa kumshukuru Mungu. Kwa kujisikia kwingi kutoka ndani-ndani moyoni “mkutano mkubwa” utalia kwa sauti kuu, ukisema: “Wokovu una Mungu [Yehova] wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo [Yesu Kristo].” Na wote wa tengenezo shikamanifu la Mungu mbinguni, kwa kuvutwa na uthamini wa maana kuu ya matukio hayo, watajiunga pamoja nao katika kuabudu, wakisema: “Amina; Baraka na utukufu na hekima na shukrani na heshima na uweza na nguvu zina Mungu wetu hata milele na milele. Amina.”—Ufunuo 7:10-12.

13. Biblia inafananishaje mwandalio utakaofanywa ili kuendeleza uzima na kutibu wanadamu?

13 Hatimaye wanadamu wote watakuwa jamii ya kibinadamu yenye umoja inayomheshimu Mungu wa kweli, “dunia mpya” chini ya “mbingu mpya” zitakazotoa wonyesho wa enzi kuu ya Yehova yenye upendo. Kwa kutumia mfano wenye kupendeza, kitabu cha mwisho cha Biblia kinasimulia faida za ajabu zitakazotiririkia wanadamu wakati huo kuwa zikiwa “mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo” ukipita katikati ya njia kuu ya Yerusalemu Mpya wa kimbingu. Kandokando ya kingo za mto huo kuna ‘miti ya uzima’ inayozaa matunda ya kuendeleza uzima wa wale wanaoyala na majani ya kutibia mataifa. Kinachofananishwa hapa ni mwandalio mzima utakaofanywa na Mungu ili kutibu na kuendeleza uzima wa wanadamu waaminio, watiifu na kuwawezesha wafurahie uzima wa milele kupitia Yesu Kristo.—Ufunuo 21:1, 2; 22:1, 2.

14. Hali katika “dunia mpya” zitakuwa tofauti na zile zilizomo ulimwenguni leo kwa njia zipi?

14 Hali zitakazokuwapo duniani wakati huo zitakuwa zenye kuburudisha kwa njia tofauti na cho chote ambacho ulimwengu wa kale umepata kufanyiza. Kupitia kutumiwa kwa faida za dhabihu ya Kristo na kupitia elimu ya mapenzi ya Mungu, watiifu, kutia na wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu, wataondolewa kila alama ya dhambi. Na watasaidiwa waendelee kimwili, kiakili, kimoyo na kiroho mpaka watakapofikia ukamilifu. Badala ya kuzaa “kazi za mwili,” kila mtu atajifunza kuzaa kwa wingi matunda ya kimungu kama upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza. (Wagalatia 5:19-23, NW) Kwa sababu ya kuenea kwa roho hiyo, mazao ya dunia yatatumiwa ili kutoa kwa ukarimu mahitaji ya wanadamu wote. Wanadamu watakapokuwa wakifanya kazi pamoja ili walitimize kusudi la awali la Muumba kwa dunia hii na wakazi wayo, maisha yatakuwa yenye maana kubwa kuliko wakati wo wote uliotangulia.

15. (a) Ni mwaliko gani wenye kuvutia ambao tayari unatolewa kwa jamii ya wanadamu? (b) Basi, imetupasa sisi mmoja mmoja tuwe tukifanya nini?

15 Kwa kutazamia kwa furaha hayo yote, roho na bibi-arusi wa Kristo anawatolea sasa mwaliko wa bidii watu kila mahali, akisema: “‘Njoo!’ Kila mtu asikiaye hilo, na aseme, ‘Njoo!’ Kisha, ye yote aliye na kiu na aje; anayetaka maji ya uzima na apokee bila malipo yo yote.” (Ufunuo 22:17, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hiyo, sasa sio wakati wa kungojea tu mpaka saa iliyowekwa ya kuanzwa kwa siku ile kuu ya Yehova ifikie upeo wayo kwenye dhiki kubwa. Ukiwa umekwisha kuukubali mwaliko wenye fadhili wa ‘kuyapokea maji ya uzima bila malipo,’ sasa wewe una pendeleo la kuwapa wengine mwaliko huo. Ni wakati wa utendaji wenye bidii upande wa wote wanaotamani sana kuja kuwa waokokaji wa kuingia katika “dunia mpya” ya Mungu iliyo bora sana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki