Kukunjulia Wenye Shida Mkono kwa Ukarimu
MUNGU wetu Yehova hutuwekea mfano wa kuwa wakarimu. Hiyo si kwa sababu ana haki ya kuwa mkarimu kwa sababu ndiye Mwenye vitu vyote. Ni kwa sababu yeye ni upendo na kila sifa ya ukarimu. Ni kama vile mwimbaji mwenye maneno matamu wa Israeli alivyotangaza: “[Yehova] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zab. 145:16) Hunyesha mvua yake na kuangaza jua lake hata juu ya wale wasiostahili. (Mt. 5:45) Yeye anatufikiria sana sisi sote tulio viumbe vidogo sana katika sayari ndogo hii!
Kwa habari ya wale wanaomkaribia wamwabudu, anawafundisha wajitahidi kuwa kama yeye wanaposhughulika na wengine. Huko nyuma katika kizazi ambacho watu wanaoitwa wenye hekima wa siku zetu wamekiona kama kizazi ‘cha kale,’ Mungu huyu mkarimu aliagiza waabudu wake hivi: “Mfumbulie kwa kweli mkono wako nduguyo, mhitaji wako, maskini wako, katika nchi yako.” (Kum. 15:11) Kama fundisho hili lingekazwa kabisa ndani ya watu kusingekuwa na haja ya kuwa na shughuli za kuomba watu watoe michango mingi, kusingekuwa na haja ya kulipa walioajiriwa kazi ya kuchangisha pesa mishahara mikubwa. Watu wangeitikia mafundisho na mfano wa Yeye “awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei.”—Yak. 1:5.
Waabudu wa kisasa pia wa Yehova wamejifunza somo hili la ukarimu. Wamevutwa sana na maneno ya Bwana wao, Kristo Yesu, yaani: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Pia, wameona ukweli wa maneno hayo, kwa sababu wanaangalia ni nani walio na shida katika ujirani wao na kuwagawia mali zao bila kujionyesha. Vilevile, wanaposikia kwamba waabudu wenzao wa Yehova katika sehemu nyingine za dunia wamepatwa na msiba fulani, wamekuwa wenye haraka sana kuwapelekea misaada! Wanakunjulia wenye shida mikono yao kwa ukarimu.
KUGAWANA ZAWADI YENYE THAMANI ZAIDI
Walakini, kuna uhitaji mkubwa zaidi ambao watu wa Yehova wameujua, uhitaji wa umati mkubwa sana wa watu duniani mwote, uhitaji ambao Kristo Yesu alikazia fikira wakati wa huduma yake ya pekee alipokuwa hapa duniani. Alipokuwa akihutubia kundi kubwa la wenye shida wakati mmoja, alishauri hivi: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa.” (Yohana 6:27) Tena, alisema hivi: “Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”—Mt. 4:4.
Kwa hiyo kuna kitu chenye thamani zaidi kuliko chakula na maji, ambavyo ni vya lazima. Mitume wa Yesu walijua sana hivyo. Kwa mfano, wakati Petro alipoendewa na mwombaji aliyelemaa, alimwambia hivi: “Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende.” Walimpa mtu huyo nini? Si mapozo tu, ingawa hayo peke yake yalitosha. Ni wazi kwamba waliamsha mtu huyo akathamini sana yule ambaye mapozo yalifanywa kwa jina lake, Yesu wa Nazareti, na Yule aliyemtuma Yesu ulimwenguni, Yehova Mungu. Masimulizi yanaendelea kueleza vile mwanamume huyo ‘alikwenda akirukaruka, na kumsifu Mungu’ huku akiingia hekaluni.—Matendo 3:6-8.
Leo Mashahidi wa Yehova hawana uwezo huo wa kufanya miujiza na kuponya watu magonjwa yao ya kimwili, lakini wana furaha na hamu ya kueleza wengine mambo waliyo nayo. Mambo gani? Kuwafahamisha habari za Yehova Mungu na makusudi yake kwa wanadamu na dunia hii kama yanavyoelezwa katika Maandiko Matakatifu. Wanawapa wengine maarifa haya kwa kwenda katika barabara za miji na mashambani wakawatafute wanaotaka kusikiliza habari wanazowapelekea. Habari hizo ni za kuwapa watu uzima, kwa maana katika sala Yesu alimwambia Baba yake wa mbinguni hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
Mashahidi Wakristo wanatumia saa nyingi katika utumishi huu, wakifanya hivyo kwa kutumia pesa zao wenyewe, ili waweze kueleza wengine kwa moyo mkunjufu mambo mema ambayo wamepokea kwa Mungu. Hata ikiwa wengi wanaowaendea hawathamini kusudi lao, au hata ikiwa wanatia shaka juu ya unyofu wa kusudi lao, Mashahidi hawa wanaendelea na kazi yao ya kutafuta wanaostahili, watu wanaoweza kujifunza kuthamini ujumbe wa Biblia.
Jambo linalostahili kuangaliwa ni hili: Hakuna mtu anayepaswa kuambia mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo kiasi cha msaada wa kimwili wala wa kiroho atakaotolea walio na uhitaji. Hiyo ni kwa sababu kanuni ya Biblia inayoelezwa katika Kumbukumbu la Torati 16:17 inawahusu wao pia: “Kila mtu na atoe kama awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya [Yehova], Mungu wako, alivyokupa.” Na ni nani ajuaye kadiri ya baraka ambayo kila mtu amepokea kwa Mungu? Ni Mungu na Kristo Yesu na mwenye kuabudu peke yao. Kwa hiyo Mkristo atafakaripo baraka zote ambazo Mungu mkarimu amempa, si lazima aombwe agawie wengine. Anaongozwa na moyo wenye shukrani afanye hivyo.
KUTAYARISHWA ILI KUTOA
Ushirika wa mashahidi Wakristo umefikiria uhitaji wa haraka wa umati mkubwa wa watu duniani pote wa kusikia ujumbe wenye kutoa uzima wa ufalme wa Mungu, kisha wakafanya matayarisho kuwatimizia uhitaji huo. Kwa kusudi hilo wameunda mashirika katika nchi mbali-mbali, kama vile International Bible Students Association hapa Afrika Mashariki. Kulingana na sheria ya nchi hizo nyingi mashirika hayo yanatumiwa kuangalia mambo ya ufundi, kama kuchapa Biblia na vitabu vya lugha nyingi vya kusaidia watu wajifunze Biblia na kuvisafirisha, kutunza pesa zinazochangwa na Mashahidi wa Yehova na watu wengine wanaowatakia mema, kutuma wajumbe wenye kusafiri na kuwatunza na kuangalia kazi nyingine mbalimbali kama hizo.
Hakuna ye yote wa maafisa wala wasimamizi wa mashirika hayo anayelipwa mshahara. Wote wanafurahia kutumia wakati na nguvu zao kuendeleza utumishi huu wa kutangaza ‘habari njema za ufalme’ katika dunia yote. (Mt. 24:14, NW) Halafu tena, wako wanaume na wanawake walioacha nafasi za kupata vyeo vyenye kuwaletea faida nyingi ili washiriki katika kazi inayohitajiwa ya kuchapa na kutayarisha na kupelekea watu vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia katika karibu kila sehemu ya dunia. Wanatumikia katika zaidi ya maafisi ya matawi 90 na viwanda vya uchapaji vinavyoendeshwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 90. Wanafurahi kwamba wanaweza kutumia miaka mingi ya maisha zao katika utumishi usio wa kichoyo, nao wanapewa chakula na makao na alawansi (posho) ndogo ya mahitaji yao.
Mashirika haya yote, maafisi ya matawi na viwanda vya kuchapia vitabu na wafanya kazi wao, yanafanya kazi yakiwa chini ya usimamizi wa Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova, nayo baraza hiyo inawakilisha waabudu wote waliotiwa mafuta wa Yehova Mungu walio duniani. Hivyo jitihada nyingi za watu wote wa Yehova zinaunganishwa ili kazi ambayo Mungu ameagiza ifanywe itimizwe kabla ya mwisho wa taratibu hii ya mambo ya kale kuja. (Marko 13:10) Zaidi ya Mashahidi wa Yehova 2,000,000 wametayarishwa hivyo kwa utumishi wa kufundisha na kuhubiri duniani pote. Wote wanafurahi kushiriki kutolea watu ushuhuda katika mitaa yao wenyewe. Ikiwa hawawezi kufikia watu wengine katika majimbo na nchi nyingine, wenzao waliomo katika tengenezo la ulimwenguni pote wanawafikia. Wanapelekea afisi ya tawi ya nchi yao michango midogo waliyo nayo.
Hivyo maneno yaliyosemwa na Mwana wa Mungu mwenyewe katika mahubiri yake juu ya mlima yanatumika sana wakati wetu: “Heri wenye njaa na kiu ya haki; maana hao watashibishwa.” (Mt. 5:6) Mungu mwenye moyo mkunjufu hutumia roho yake kuongoza waabudu wake duniani wafuate uongozi wake na kufikia umati wa watu wenye shida na msaada wa kiroho, lakini bila kusahau mahitaji ya kimwili ya wenye kustahili. Nao waabudu hawa wenye kushikamana na Mungu ambaye hutoa kila zawadi kamilifu wanathamini sana mashirika wanayotumia kushiriki kwa umoja wajitahidi kutolea wenye njaa na kiu michango yao katika nchi za mbali.
Kwa kweli sisi tuabuduo Mungu huyo tuna pendeleo kubwa sana! Twaweza kuiga ukunjufu wake wa moyo na kuonyesha tu wana na binti zake. Tutafurahi sana maelezo yaliyoongozwa na Mungu ya mtu mkarimu yatakapoweza kutumiwa kwetu: “Heri atendaye fadhili na kukopesha; . . . amekirimu, na kuwapa maskini, haki yake yakaa milele.”—Zab. 112:5, 9.