“Sababu Gani Mungu Anaruhusu Uovu?”
Watu Wengi Wanauliza, “Ikiwa Kuna Mungu, Sababu Gani . . . ”
WATU wengi wanauliza maulizo yakiwa na maneno haya yakitangulia, ‘Ikiwa kuna Mungu, sababu gani . . . ” Wengine wa waulizaji wa maulizo hayo wanakuwa wakitaka tu kuwadhihaki wale wanaoamini kuwako kwa Mungu. Walakini, wengine wengi wanasumbuka sana nao wanatafuta, majibu yanayoweza kutia nguvu imani yao inayopungukiwa nguvu. Labda ulizo linaloulizwa zaidi kati ya maulizo ya namna hii ni hili, “Ikiwa kuna Mungu, sababu gani yeye anaruhusu Uovu?”
Ni kweli kwamba Mungu huuruhusu.Walakini kuna watu wengi sana duniani ambao si kwamba wanauruhusu tu; bali pia wanaufanya. Wao wanatokeza vita; wanaangusha makombora juu ya wanawake na watoto; wanaiunguza nchi, wakitokeza njaa; wanaeneza magonjwa na vifo kwa kuchafua hewa, maji na ardhi—wakati wa vita na wa amani vilevile. Si kwamba tu wanaongeza uovu katika mataifa yote kwa ujumla na katika taifa moja moja, bali pia wanajiletea taabu wao wenyewe mmoja mmoja.
Wanakula kupita kiasi na kuwa na tumbo kubwa sana, wanakunywa kupita kiasi na kupatwa na ugonjwa wa ini, wanavuta tumbako na kupatwa na donda baya mapafuni, wanafanya uzinzi na kulalana wanaume kwa wanaume na kupatwa na kaswende na kisonono, wanaendesha magari bila kujali na kuua watu makumi ya maelfu kila mwaka, wanafuatilia kwa pupa fedha na mali, na kwa kufanya hivyo, wanaleta mikazo inayotokeza vidonda na ugonjwa wa moyo —nayo orodha ya mambo kama hayo inaongezeka.
KWA KWELI WAO WANATAKA NINI?
Kwa kweli watu wa namna hiyo hawataki uovu uondolewe; wao wanataka tu adhabu ya kufanya uovu iondolewe. Wanataka kufanya uasherati ovyo ovyo pasipo kupatwa na kaswende na kisonono, kuvuta tumbako pasipo kupatwa na donda baya la mapafuni, kunywa kupita kiasi pasipo kupatwa na matatizo ya ini, kuendesha magari bila kujali pasipo kupatwa na misiba ya barabarani, na vivyo hivyo. Wanataka kupanda uovu lakini wasiuvune. Wanataka kuchuma matofaa (apples) kutoka kwa magugu na kukusanya zabibu kutoka kwa mibaruti.
Ndipo, wavunapo mavuno yenye ole ya uovu walioupanda, wanalia na kuugua na kuinua kilio chao chenye uchungu: ‘Sababu gani ni mimi tu, Mungu? Sababu gani ni mimi?’ Lakini sababu gani isiwe wewe? “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Wanatenda sawa-sawa na vile Yehova alivyotangulia kuona: “Upumbavu wa mtu hupotosha njia yake; na moyo wake [unakasirika] juu ya [Yehova].”—Mit. 19:3.
Yehova Mungu analaumu dhambi na kutokuwa na kiasi. Milioni nyingi za watu wanalaumu Mungu kwa kuruhusu uovu, lakini mwingi wa ole wao unatokana na kuvunja amri zake. Kwa kuwa wanauruhusu na kufanya uovu, sababu gani Mungu asifikiri kwamba wanaupendelea? Na kama Mungu angeukomesha, kama angeleta mkono wake na kutoa sigara vinywani mwao, au bilauri za mvinyo kutoka mikononi mwao, au kutenganisha wenye kufanya uasherati, au kupunguza mwendo wa magari yao kutoka maili 75 kwa saa kwenye maili 55 kwa saa (kilometres 120 mpaka 90), je! wasingelalamika sana na kusema kwamba uhuru wao unaingiliwa? Akiuruhusu analaumiwa; akiukomesha analaumiwa.
Wakati unakuja ambao katika huo Yehova ataukomesha kwa kuwaondoa waovu:
“Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mit. 2:21, 22
Huenda wengine wakalaumu tendo hilo la Mungu na kusema kwamba ni ukatili, lakini ni katika njia gani nyingine uovu utakomeshwa? Kwa kutengeneza upya tabia za watu? Jamii za watu zimetumiwa fedha milioni nyingi wakijaribu kufanya hivyo. Mipango hiyo inashindwa. Wahalifu wanaofunguliwa kutoka gerezani wanarudia njia zao za zamani. Upesi wanaanza kutaabisha watu zaidi. Ikiwa waovu wanakataa kubadili njia zao, suluhisho ni nini? Je! unaweza kuwa na bustani ya maua ya waridi katika shamba la magugu, au kuwa na kuku pamoja na mbweha katika ua wa nyumba, au kuwa na paradiso yenye amani kukiwa na wahalifu wakifanya wapendavyo humo?
SABABU YEHOVA AMERUHUSU UOVU
Yehova aliumba wanadamu watunze dunia ya paradiso. Yeye hakuwafanya wawe kama mashine, bali aliwapa uhuru wa kuchagua. Je! wangechagua kuitunza dunia kulingana na kusudi la Mungu? Shetani alisema kwamba hawangefanya hivyo, naye akatokeza mashaka akijidai kwamba angegeuza wanadamu wote wamwasi Mungu. Yehova alimruhusu Shetani ajaribu. Wakati ulihitajiwa ili kujibu suala (ulizo) hilo.
Kwamba suala hilo lilitokezwa inaonyeshwa kwa habari ya Ayubu. Yehova alivuta fikira za Shetani kwa Ayubu, akisema: “Yeye ananiabudu mimi na ni mwangalifu asifanye lo lote ovu.” Shetani akajibu hivi: “Je! Ayubu angekuabudu kama hangepata cho chote kutokana nayo [ibada]? Wewe sikuzote umemlinda.” Ndipo Yehova alipomruhusu Shetani amtese Ayubu, akijaribu kuvunja ukamilifu wake. Mke wa Ayubu alidhani alifahamu chanzo cha taabu ya mumewe naye akamkemea, akisema: “Wewe bado ni mwaminifu kama [ulivyokuwa] sikuzote, sivyo? Sababu gani usimkufuru Mungu ukafe?” Walakini Ayubu alishika ukamilifu, akamthibitisha Shetani kuwa mwongo, naye akabarikiwa na Mungu.—Ayubu 1:6-12; 2:1-10; 42:12, Today’s English Version, ya Kiingereza.
Je! ninyi wazazi mmepata kuwaaminisha watoto wenu kitu fulani au kuwapa daraka fulani, ili mwone kama wanastahili kuaminishwa vitu vikubwa hata zaidi? Vivyo hivyo Yehova Mungu anawajaribu wanadamu, aone ni watu gani mmoja mmoja watakaoaminishwa kutunza dunia ya paradiso chini ya ufalme wa Kristo. Yeye anauruhusu uovu kwa kusudi, walakini yeye hautokezi. Misiba mingine huja bila kutazamiwa: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhu. 9:11, NW) Misiba mingine hutokezwa na upumbavu wa wanadamu. “Mungu alifanya mutu mwenye haki; lakini wao wametafuta hila nyingi.” (Mhu. 7:29, ZSB) Bado mingine inaletwa na Shetani katika jitihada zake za kuwageuza wanadamu wote wamwasi Mungu, akijua kwamba watamlaumu Mungu, mahali pa kumlaumu yeye, akijua kwamba wengi hata hawaamini kwamba yeye Shetani yuko.—Ufu. 12:12.
Kuna Mungu, naye ana sababu za kuuruhusu uovu. Lakini wakati wake kuukomesha hauko mbali sana.