Ufalme wa Mungu Utamaanisha Nini Kwako?
“Utafuteni kwanza ufalme wake na haki [ya Mungu]; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mt. 6:33.
INGEMAANISHA nini kwako kuishi chini ya serikali inayoongozwa na kuendeshwa na Mungu Mwenye Nguvu Zote? Maisha yangekuwaje ‘ikiwa mapenzi ya Mungu yangefanywa duniani kama huko mbinguni’?—Mt. 6:9, 10.
Wazo la yale ambayo ungemaanisha linapatikana katika maneno ya mtunga zaburi aliyesema hivi juu ya Mungu: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zab. 145:16) Ebu wazia hilo! Wakati unakuja ambapo mahitaji na tamaa zifaazo za kila mtu zitatoshelezwa, na inaelekea kwa kadiri kubwa ajabu kuliko vile sisi wanadamu wasiokamilika tunavyoweza kuwazia sasa!
WINGI WA MAMBO YA KIUCHUMI
Inaelekea kwamba mojawapo la mambo makubwa ambayo ungefanya ni kuweka taratibu ya kiuchumi yenye kuleta ufanisi na iliyo imara. Kuleta hali nzuri ya maisha ndiyo mojawapo la mambo ya maana sana katika jamaa zote leo. Lakini sasa, ni wachache sana walio na wingi wa vitu.
Pasipo shaka, ungetaka kuondoa umaskini na kuwapa wote vitu kwa wingi—si wachache tu wenye kufanikiwa. Mpaka sasa hakuna taratibu ya utawala wa kibinadamu ambayo imekuwa na uwezo wa kutimiza jambo hili. Kwa kweli, tukiangalia historia ya mwanadamu, inaonekana kwamba wingi wa mambo ya kiuchumi ulimwenguni pote ni jambo lisilowezekana. Na ndivyo ilivyo—kwa maoni ya kibinadamu!
Walakini, ebu ifikirie kanuni hii iliyotolewa na Yesu Kristo: “Kwa wanadamu hilo haliwezekani; bali kwa Mungu [mambo] yote yawezekana.” (Mt. 19:26) Usisahau kwamba aliyeumba ulimwengu ana hekima na uweza mwingi, zaidi kuliko mwanadamu ye yote. Alitumia uweza huo kutengeneza ulimwengu wote wa ajabu sana wenye mabilioni ya makundi ya nyota, kila kundi likiwa na mabilioni ya nyota kama vile jua letu, na vyote vikifanya kazi kwa kupatana ajabu. Vilevile yeye aliumba namna zote za vitu vyenye uhai vilivyo duniani, ambazo ni ngumu sana kufahamika na za namna mbalimbali hata kwamba wanasayansi hawajazifahamu mpaka sasa. Bila shaka lisingekuwa jambo kubwa sana kwa Muumba Mwenye Nguvu Zote kama huyo kufanyiza na kuongoza jamii ya kibinadamu ambayo ingetumia dunia hii na mali zake kwa faida ya wote.
Kwa mfano, kwa kupendeza, Yesu alisema hivi kuhusu chakula: “Waangalieni ndege wa angani, kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao.” Vilevile alitaja hili juu ya mavazi: “Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.”—Mt. 6:26-29.
Hii inaonyesha kwamba Muumba anaweza kutoa vitu kwa wingi kwa viumbe vyake vya kidunia vilivyo “vinyonge zaidi.” Hakika, chini ya utawala wake wa Ufalme Mungu ataonyesha uweza huu juu ya viumbe vyake vya kibinadamu. Kwa kweli, ahadi yake ni hii: “[Yehova] wa majeshi atawafanyia [watu wote, si wachache wao tu] . . . karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo yake.” (Isa. 25:6) Na zaidi ya hayo, Biblia inasema hivi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” (Zab. 72:16) Ndiyo, chini ya utawala wa Ufalme, Mungu atahakikisha kwamba “nchi imetoa mazao yake.”—Zab. 67:6.
Wala wingi huu hautakuwa matokeo ya kazi ngumu isiyopendeza, yenye kuchosha, Twawezaje kuwa na hakika juu ya hili? Basi, Mungu alipoumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, aliwaweka katika paradiso, ambapo kazi ilikuwa inapendeza. (Mwa. 2:8, 9, 15; 1:31) Naye Yesu aliahidi kwamba paradiso hiyo iliyopotea itarudishwa chini ya utawala wa Mungu wa kimbinguni. (Luka 23:43, ZSB) Kwa hiyo wakati huo kazi itakuwa yenye kupendeza. Ufundi wa mtu wa kutumia mikono yake, na ufundi na kazi nyingine zitaonekana zaidi sana, kwa uzuri na kwa utaratibu.
Hata hivyo, wingi huo wote wa mambo ya kiuchumi ungekuwa na maana gani ikiwa ungeharibiwa na vita, ghasia ya raia na mapinduzi, kila baada ya miaka michache, kama vile imekuwa ikifanyika chini ya utawala wa kibinadamu? Baraka za mambo ya kimwili zaweza kufurahiwaje pasipo usalama?
USALAMA WA KWELI
Ikiwa ungekuwa na uwezo wa kuondoa mambo ambayo sasa yanaleta ukosefu wa usalama, je! usingefanya hivyo? Basi ungetarajia kwamba Mungu Mwenye Nguvu Zote hatafanya hivyo chini, ya utawala wake? Hapana, kwa maana yeye anatuhakikishia kwamba “avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” (Zab. 46:9) Hivyo inamaanisha usalama ulimwenguni pote kwa mara ya kwanza katika historia, tofauti na ilivyo leo wakati usalama au amani yo yote ni ya muda tu, kwani vita, ghasia ya raia, na kuasi serikali na yanayofanana na hayo yanakuwa yakiendelea mahali mahali karibu kila wakati.
Si kwamba tu serikali ya Ufalme wa Mungu itafikiliza amani duniani pote. Itafanya zaidi ya hilo. Itaendelea kuelimisha raia zake katika njia za amani: “Naye atatufundisha njia zake, . . . wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isa. 2:3, 4) Mungu akiwa Mfikilizaji sheria na Mwalimu, Waweza kuona sababu Biblia inasema kwamba chini ya utawala wa Ufalme watu “watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zab. 37:11.
Usalama unaharibiwa vilevile na uvunjaji wa sheria. Leo serikali za kibinadamu haziwezi kuzuia wimbi la tabia ya kuasi sheria. Walakini dunia ikiwa inatawalwa na serikali moja tu, ile ya Mungu, na ikiwa chini ya orodha ya sheria zile zile za haki, uvunjaji wa sheria utaondolewa upesi. Ye yote ambaye atataka kuendelea kuasi sheria za Mungu za haki, hataruhusiwa aharibu amani ya taratibu hiyo mpya. Sheria itakuwa hii: “Watenda mabaya wataharibiwa, . . . asiye haki hatakuwapo.” (Zab. 37:9, 10) Hivyo, jamii ya kibinadamu haitakuwa na gereza, polisi, makufuli milangoni, ndiyo, hakutakuwapo hofu. Basi, ahadi ya Mungu ni kwamba katika utawala wa Ufalme wake, watakaokuwa wakiishi chini yake “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mik. 4:4.
Walakini, je! lisingekuwa jambo baya kujifurahisha wingi wa mambo ya kiuchumi, kazi ya kupendeza, katika hali zenye amani kamili, kisha, tupatwe na magonjwa, kuzeeka na kufa?
AFYA NA UZIMA VYARUDISHWA
Ikiwa wewe ni daktari kisha upate dawa yenye kuponya kila namna ya ugonjwa, je! usingeitumia? Zawadi za Nobel zinatolewa kwa madaktari wanaoleta sehemu tu ya faida za namna hiyo. Walakini, lo lote ambalo madaktari wanaweza kufanya kupunguza maumivu, kuzuia magonjwa yasienee pote, na kuongeza miaka michache katika maisha za watu, ukweli ni kwamba, mwishowe, wote wanapatwa na magonjwa, uzee na mauti.
Walakini, chini ya ufalme wa Mungu, “wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Ufu. 21:4; Isa. 33:24) Mfuatano wote wa magonjwa, kuzeeka na kufa utamalizwa kwa uwezo wa Mungu hivi kwamba, miili na akili zitafanywa upya. Watarudishwa kwenye afya kamili hata kwamba ‘nyama za mwili wa mtu zitakuwa laini kuliko wakati wa utoto wake.’ (Ayubu 33:25) Hali zitakuwa kama zile zinazosimuliwa katika Isa-ya 35:5, 6. “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”
Lakini ikiwa watu hawawi wagonjwa, au kuzeeka, basi wasingekufa. Na ndivyo ‘itakavyokuwa. Hakuna mtu mwenye akili nzuri angependa kufa. Chini ya utawala wa Ufalme hawatakufa, kwa maana ahadi ni kwamba: “Mauti haitakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Hivyo, “wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zab. 37:29.
Na zaidi ya hayo, Mungu, aliyeumba mwanadamu kutokana na vitu vya asili vya dunia, anaweza vilevile kumwumba upya. Kwa sababu hiyo Biblia inasema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Kwa hiyo, wafu pia, waliomo katika kumbukumbu la Mungu (lililo bora zaidi sana ya lile la mashine yo yote ya kumputa iliyoundwa na mwanadamu) watarudishwa kwenye uhai na kupewa nafasi ya kuishi milele katika mazingira yenye haki, katika dunia ya paradiso. Lo! namna wakati huo utakavyokuwa wenye furaha!
WATU WANAOJALI
Hata kukiwa na faida hizo zote, bado furaha yaweza kuharibiwa na watu wenye uadui, watu wachoyo wasiojali faida zako. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.” (Mit. 15:17) Lakini kwa kuwa Mungu atarudisha hali ya urafiki kati ya wanyama wa kondeni na wanadamu, je! hatafanya vivyo hivyo kati ya wanadamu?—Isa. 11:6-9; Eze. 34:25.
Elimu ii hii ya duniani pote itakayoelimisha watu ‘wasijifunze vita tena’ itawaelimisha vilevile namna ya ‘kupenda jirani zao kama vile wanavyojipenda wenyewe.’ (Isa. 2:4; Mt. 22:39) Zaidi ya hayo, nguvu ya utendaji ya Mungu, roho takatifu yake, ikifanya kazi katika watu itatokeza faida za ajabu, kama vile itakavyofanya kwa habari ya wanyama. Tunda la roho hiyo ni “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.”—Gal. 5:22, 23, NW,
Lo! namna zilivyo sifa njema kwa wanadamu kuwa nazo! Nao watakuwa nazo, kwa sababu roho itakayokuwa ikitawala katika taratibu Mpya itakuwa ile ya Mungu. Nguvu hiyo ikiwa inafanya kazi katika watu, na hali za sasa zenye huzuni zinazofanya watu wengi kuwa wenye chuki, zikiwa zimeondolewa, uhusiano utasitawi kati ya wanadamu ambao utakuwa wenye kuchangamsha moyo na wenye kufurahisha kweli kweli. Ndipo, hali ya kijamii itakuwa kama inavyosimuliwa: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”—Zab. 133:1.
Je! utawala wa Ufalme unakuvutia? Ikiwa ndivyo, basi itafaa ujitahidi kujifunza mengi zaidi juu yake. Kwa mfano, ni nani hasa watakaoshiriki katika serikali ya Mungu ya kimbinguni? Kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini ili apate kibali ya Mungu ya kuishi milele duniani? Je! kuna ushuhuda wo wote, duniani sasa, kuonyesha kwamba utawala wa Ufalme unaleta matokeo kweli kweli? Je! Mungu amepata kuonyesha wakati wo wote kwamba anaweza kuletea wanadamu faida za ajabu kama vile kuponya wagonjwa, kufufua wafu, au kuwaleta watu wa makabila na mataifa mbalimbali katika umoja na upendo wa kweli? Na ikiwa watu wataishi milele chini ya ufalme wa Mungu, je! kutakuwako tatizo la kuijaza dunia watu sana?
Maulizo haya na mengine mengi juu ya ufalme wa Mungu yanajibiwa katika Biblia. Sababu gani usimwulize mmoja wa Mashahidi wa Yehova akusaidie kuona ni wapi maelezo haya yanapopatikana katika Biblia? Ufanyapo hivyo, na kujifunza kabisa juu ya baraka za ajabu za wakati ujao, ndipo utakapofahamu sababu ya Yesu kuwaambia wafuasi wake: “Utafuteni kwanza ufalme wake na haki [ya Mungu].”—Mt. 6:33.