Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 11/1 kur. 5-7
  • Hizi Ndizo Nyakati Mbaya Zaidi, Lakini Ndizo Nyakati Bora Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hizi Ndizo Nyakati Mbaya Zaidi, Lakini Ndizo Nyakati Bora Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati Wetu​—Kizazi Kilichotiwa Alama
  • Maana ya Yote Hayo
  • Ahadi za Mungu
  • Kuna Faida Hata Sasa
  • Uharibifu wa Ulimwengu Uliotabiriwa Utakuja Lini?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu!
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Mfumo wa Sasa Utaendelea Kuwapo Mpaka Lini?
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 11/1 kur. 5-7

Hizi Ndizo Nyakati Mbaya Zaidi, Lakini Ndizo Nyakati Bora Zaidi

CHARLES DICKENS alianza utangulizi wa kitabu chake cha hadithi ya historia kiitwacho A Tale of Two Cities, kinachohusu Mapinduzi ya Ufaransa, kwa maelezo haya: ‘Zilikuwa ndizo nyakati bora zaidi, zilikuwa ndizo nyakati mbaya zaidi.” Kwa njia hiyo alijaribu kueleza mchafuko wa wakati huo, na pia matumaini maangavu kwamba mabadiliko makubwa katika historia yalikuwa yakitokea.

Lakini kwa sababu ya yale tuliyoandika katika makala iliyotangulia, nyakati zetu zaweza, kwa njia nyingi, kuitwa kwa kufaa sana “nyakati mbaya zaidi.” Hata hivyo, je, kipindi cha magumu makubwa chaweza kuwa sababu ya furaha wakati uo huo? Je! kweli kweli chaweza kuwa “nyakati bora zaidi”? Ndiyo, ikiwa tumehakikishiwa kwamba siku zilizo bora zaidi ziko mbele karibu.

Kama tulivyokwisha kuona, katika njia nyingi ulimwengu sasa unapitia nyakati zenye taabu sana. Lakini kuna kila ya sababu kusadiki kwamba wokovu umekaribia kwa jamii ya kibinadamu​—wokovu kutokana na uhalifu, vita, njaa kubwa-kubwa, magonjwa. Biblia inatoa tumaini hilo. Hata hivyo, ili tufanye tumaini hilo liwe letu, tunahitaji kutambua kipindi tunamoishi na kujifunza katika Maandiko Matakatifu ni mwendo gani tunaopaswa kufuata.

Wakati Wetu​—Kizazi Kilichotiwa Alama

Katika karne ya kwanza, mitume wa Yesu hapo kwanza walimtazamia anyakue mamlaka katika Israeli akiwa ndiye Masihi aliyeahidiwa. Walipoona kuondoka kwa Yesu kulikuwa kumekaribia, na mataraja yao yalikuwa hayajatimizwa bado, walimuuliza juu ya kurudi kwake hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Unabii aliotoa Yesu katika kujibu haukutimizwa kikamili katika karne ya kwanza. Na baadaye maandishi yaliyoongozwa na Mungu yalielekeza kwenye utimizo mkubwa zaidi wa baadaye katika historia. (Ufunuo 6:2-8) Je! ingeweza kuwa ni katika wakati wetu?

Yesu alionyesha kwamba ufahamu kidogo ungehitajiwa ili kutambua kipindi hicho kilichotabiriwa, kwa maana aliwaonya wanafunzi wake kwamba walio wengi sana hawangeelewa maana ya matukio makubwa yenye kutokea. Akitumia Gharika ya dunia yote ya siku za Nuhu kuwa ufananisho, Yesu alisema: “Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa [kuwapo] kwake Mwana wa Adamu. . . . Wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.”​—Mathayo 24:37, 39.

Watu wangefahamuje ‘kuwapo’ kwake na kwa hiyo wachukue hatua za kuepuka kufagiliwa mbali katika uharibifu kama walio wengi katika siku za Nuhu? Yesu alitoa “ishara” ya kiunabii yenye sehemu nyingi ambayo imeandikwa katika Injili. Ebu tuone kama “ishara” hiyo inaonekana leo, na kama ndivyo, inaonyesha kuna nini mbele.

VITA VYA MATAIFA YOTE​—ONGEZEKO LA KUTOKUTII SHERIA: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” (Luka 21:10) “Kuongezeka kwa kutokutii sheria.”​—Mathayo 24:12, NW.

Vita vingi vimetokea tangu mwaka 1914, kutia ndani viwili vya ulimwenguni pote. Hata wakati huu askari na magaidi karibu milioni moja wanapigana, na vijana zaidi ya 100 wanauawa kila siku, kulingana na gazeti New Zealand Herald. Pia uhalifu unasitawi, kama ambavyo kwa kusikitisha huenda ukawa unajua. Mwandishi wa habari za magazetini Anthony Lewis, hivi karibuni alisema: “Kutoka nchi zenye kutofautiana sana kama Uingereza . . . na Urusi kuna ripoti za ongezeko la uhalifu wa jeuri na kushindwa kwa wenye mamlaka kukabiliana nao.”

MATETEMEKO YA ARDHI: “Matetemeko ya ardhi mahali hapa na mahali hapa.”​—Mathayo 24:7, NW.

Ingawa kumekuwako matetemeko makubwa-makubwa ya ardhi pindi fulani fulani wakati wa karne nyingi, siku zetu zimetiwa alama hasa katika jamho hilo. Matetemeko ya ardhi yamekuwa mengi sana katika makumi machache ya miaka iliyopita. Kuanzia 1970 mpaka 1979, kwa wastani watu 80,000 kila mwaka walipoteza uhai wao katika matetemeko ya ardhi. Hesabu hiyo hata haitii ndani msiba wa mwaka 1976 katika China, ambapo, kulingana na makadirio fulani, watu 800,000 walipoteza maisha zao!

NJAA KALI​—MARADHI: “Njaa na tauni mahali mahali.”​—Luka 21:11.

Kulingana na shirika la UNICEF, watoto milioni 12 waliuawa na njaa ulimwenguni pote mwaka wa 1979. Katika Afrika karibu mtoto mmoja kati ya kila watatu anauawa na njaa kali. Ugonjwa, pia, unaendelea kuleta msiba ulimwenguni pote. Watoto 500000 wanauawa na ugonjwa shurua (ukambi), na watu bilioni moja ni wenye kutaabishwa na maradhi ya sehemu zenye joto kali. Wala wale walioko kwenye nchi zilizofanya maendeleo ya ufundi wa viwanda hawawezi kujiona salama, kwa maana huko kansa, maradhi ya moyo na maradhi ya kisonono na kaswende yanashambulia mamilioni mengi.

USHUHUDA WA ULIMWENGUNI POTE: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu.”​—Mathayo 24:14, NW.

Katika kipindi cha miezi 12 tangu Septemba 1982 mpaka Agosti 1983, Mashahidi wa Yehova walitumia saa zaidi sana ya milioni 436 wakieneza habari njema na kuwafundisha watu kweli za Biblia. Wahudumu zaidi ya milioni mbili walihubiri katika nchi na visiwa vya bahari 205.

Maana ya Yote Hayo

Baada ya kutabiri matukio hayo tofauti, Kristo alifunua maana yayo:

“Utazameni mtini na miti mingine yote. Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu. Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie.”​—Luka 21:29-32.

Utimizo wa hayo yote ambayo Yesu alikuwa ameeleza ungefanyiza “ishara” yenye sehemu nyingi, ambayo ingedokeza ukaribu wa Ufalme wa Mungu bila kukosea sawa na ambavyo miti ‘iliyochipuka’ inavyotangaza kiangazi kimefika. Lakini mambo hayo yalianza kutokea wakati gani?

Akieleza juu ya tukio moja lililobadili sura ya ulimwengu, mwanauchumi Mfaransa, Alfred Fabre-Luce alisema: “Vita ya 1914 ndiyo iliyokuwa tetemeko la kwanza lililotokeza mitikiso ambayo ingali inatutikisa leo.” Wanahistoria na watawala wengi wengine wamekubali kwamba kipindi chenye kutokeza tofauti kilianza mwaka wa 1914 wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipoanza. Kwa kupendeza, Pius wa 11, aliyekuwa papa tangu mwaka 1922 mpaka mwaka 1939, alitambua kwamba matukio ya tangu 1914 yalikuwa “ishara za siku za mwisho, kama ilivyotangazwa na Bwana Wetu.” Kama tulivyokwisha kuona, matukio tofauti ya ulimwengu yaliyotabiriwa yanaendelea mpaka leo hii. Kwa hiyo tuna sababu nzuri kusadiki kwamba kizazi kilichoshuhudia mshtuo wa kwanza mwaka wa 1914 na ambacho kingali kinawakilishwa na watu walio hai leo lazima kiwe ndicho kitakachoshuhudia utimizo wa mwisho wa unabii huo.

Basi, nia yetu yapasa kuwa nini kwa kadiri “kizazi” hicho kinavyosonga mbele? Hatupaswi kushindwa na kuvunjika moyo wala kuwa wenye ubaridi. Badala yake, tunahitaji kufuata shauri ambalo Yesu alitoa baada ya kutaja sehemu mbalimbali za “ishara” hiyo. Alisema: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Tunaweza kuwa wenye nia hiyo tunapojua wakati ujao umetuwekea nini chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.

Ahadi za Mungu

Wengi wana maoni kwamba wasiwasi wao wa wakati huu ungeweza kupunguzwa kama wangeweza kufanya kazi katika mazingira yenye kupendeza zaidi na wakiwa na usalama. Maandiko hayatupilii mbali wazo hilo. Manabii kama Isaya walitabiri juu ya hali bora ambazo zingemwezesha mwanadamu afurahie maisha: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.”​—Isaya 65:21, 23.

Lakini, Maandiko yanavuta fikira hasa kwenye uhakika wa kwamba baraka zenye kutoka kwa Yehova pia zitakuwa pamoja na baraka za kiroho. Wanadamu wanahitaji zaidi ya kuwa na hali nzuri ya kimwili. Tunahitaji kuheshimu kanuni za upendo na haki na kuishi pamoja na wengine wanaoheshimu kanuni hizo. Ufalme wa Mungu utaleta mazingira hayo mazuri duniani, na kuwezesha wenye mioyo minyofu wasitawi kikamili. Nabii huyo aliyetangulia kutajwa anaongeza hivi: “Maana hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.”​—Isaya 26:7-9.

Ufalme wa Mungu utatimiza jambo ambalo hakuna serikali nyingine inaweza kutimiza, yaani, kuokoa wanadamu kutokana na dhambi na matokeo yake: ole, magonjwa na kifo. Mungu atakapotimiza hilo kupitia Yesu Kristo, wale wote wanaopenda na wanaozoea uadilifu watapata uzima wa milele.​—Yohana 3:16.

Kuna Faida Hata Sasa

Hatupaswi kusahau uhakika wa kwamba sehemu kubwa ya furaha inapatikana sasa hivi tukiishi kwa kupatana na makusudi ya Mungu. Mambo mabaya yanayotendeka duniani yanawapata wote wala mambo hayo yenyewe hayaleti furaha. Hata hivyo, tukifahamu maana yayo na hivyo tuitambue “ishara,” tunaweza kuelewa ni kwa sababu gani nyakati zetu kwa njia fulani ni kionjo cha kimbele cha nyakati bora zaidi, kwa maana tutashuhudia kujiingiza kwa Mungu, amalize daima matatizo ya wanadamu.

Ingawa wanaishi katikati ya ulimwengu huu wenye msukosuko, Mashahidi wa Yehova wameweza kuvuna faida ambazo wewe pia unaweza kupata. Maarifa yao ya sheria za Mungu yanatoa ulinzi wa kiadili na yanawawezesha kuishi maisha yenye usawaziko. Wana amani ya akili inayoletwa na tumaini lenye msingi wa ahadi za kimungu, pamoja na mwenendo wa utawa. (Zaburi 119:165; 1 Timotheo 4:8) Pamoja na hayo, ukombozi wakati Kristo anapoharibu adui za Mungu katika wakati ujao ulio karibu na kufungua nafasi ya kupokea baraka za kudumu za Mungu.​—Sefania 2:2, 3; Zaburi 29:11.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kuhusu nyakati zetu, Yesu alisema kwamba tunaweza kujifunza kutokana na mtini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki