Mchimbuzi wa Vitu vya Kale Aliyethamini Ukweli wa Biblia
“SASA ule msingi wa mwisho wa kuwa na shaka lo lote kwamba Maandiko yametufikia sisi ‘ kama yalivyoandikwa umeondolewa.” Maneno hayo ya Sir Frederic Kenyon, yaliyotolewa katika ukurasa 289 wa kitabu chake kinachoitwa The Bible and Archaeology (1940), yametajwa katika ukurasa 53 wa kitabu cha Sosaiti yetu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Kwa sababu gani Kenyon alikata shauri hivyo? Ni kwa sababu hati za mafunjo zilizogunduliwa karibuni zilikuwa za tarehe iliyokaribiana sana na wakati wa kutungwa kwa Maandiko hivi kwamba angeweza kukieleza kipindi kilichopita katikati kuwa ni “kisichostahili kufikiriwa.” Hata hivyo mafunjo hayo hayakuonyesha utofautiano mkubwa na hati za hivi majuzi zaidi. Jambo hilo lilithibitisha “ukweli na ukamilifu wa ujumla’’ wa maandishi ya baadaye ambayo yametumiwa kuitafsiri Biblia.
Jambo la kupendeza ni kwamba, mmoja wa Mashahidi wa Yehova anaandika hivi kuhusu mchimbuzi huyo wa vitu vya kale anayejulikana sana; “Sir Frederic Kenyon alikuwa na vichapo kadha vya Sosaiti, kwa maana muda wa miaka iliyopita lilikuwa pendeleo langu kumwachia vitabu mbalimbali na kuandikiana barua naye. Nilipata kufahamiana naye mwanzoni wa mwaka 1936. . . . Kitabu kilichoandikwa na Dak. Kenyon ndicho kilichonipa nuru juu ya asili za Biblia. Mimi nilimwandikia nikamwambia hivyo. Kitabu chake The Story of the Bible kilinifikia baadaye kikiwa kimepigwa maandishi yenye kusema, ‘Kwa kutakiwa kila fanaka na mtungaji, F. G. Kenyon, Mei 1,1937.’
“Yeye alipopokea kitabu ‘The Truth Shall Make You Free, ‘kilichochapishwa na Sosaiti yetu, aliniandikia hivi: ‘Shabaha yenu ni sawa na yangu mwenyewe, kusihi watu waisome na kuiamini Biblia; ninyi mnashughulikia watu wengi zaidi. Vitabu vyangu vinaelekezwa hasa kwa wale wanaosumbuliwa na mambo wanayoambiwa juu ya matokeo ya uchambuzi na ugunduzi wa kisasa, hali kitabu chenu kinasema na wasomaji wa matabaka yote na aina zote. Mimi nawatakia ninyi mafanikio yote kwenye kazi yenu.”
“Akiandika kuhusu vingine viwili vya vichapo vya Sosaiti yetu, yeye alitaja tena shabaha moja tuliyo nayo pamoja naye, ‘kuwatia watu moyo waisome Biblia, tena waisome kwa kuielewa,’ kisha akaongeza: ‘mimi nafurahi kusikia kwamba vitabu vyenu vinaenezwa mahali pengi sana na katika nchi nyingi.’ . . .
“Katika mwaka 1948 Sir Frederic alichapisha kitabu The Bible and Modern Scholarship, ili kupinga kitabu cha Dak. Barnes, Askofu wa Birmingham, aliyekuwa ameeleza sehemu za Biblia, kutia na zile zinazohusu kukombolewa na Kristo Yesu, kuwa ni ‘hadithi za uwongo za watu wa kale.’ Katika utangulizi wake Dak. Kenyon anasema: ‘Uchunguzi mrefu wa kitabu cha Askofu huyo ulinisadikisha kwamba hicho hakikuwa kiwakilishi kinachopatana na matokeo ya kisasa ya wanachuo, bali kilikuwa ni marudio ya uchambuzi uliopendelewa sana karibu miaka sabini iliyopita, na ukapuuza karibu matokeo yote ya miaka hamsini iliyopita.’ Kwa habari ya kitabu chake mwenyewe, Kenyon alisema hivi: ‘Mimi naamini kwamba wakati umefika . . . wa kuanza tena kuwa na uhakika kwamba Biblia ni kiongozi cha kuelekeza kwenye ukweli na msingi wa kuongoza mwenendo wa maisha. . . . Ninaloweza tu kutumaini ni kwamba [kitabu hiki] kitakuwa usaidizi fulani kwa wale wanaotazamia Ukristo kuwa ndilo tumaini moja tu la ulimwengu wetu ulipotoshwa fikira, na wenye kuitazamia Biblia kuwa ni msingi uliohakikishwa wa imani ya Kikristo.’
“Msomi huyo wa Biblia aliye mashuhuri ulimwenguni, aliyekuwa ameandika kwa fadhili sana kuhusu kazi na vichapo vya Mashahidi wa Yehova, alikuwa mtu mnyenyekevu, mwenye fadhili za kweli. . . . Mwaka 1889, baada ya kufaulu zaidi ya wengine akiwa mwanafunzi katika Oxford, aliingia Jumba la Makumbusho la Uingereza akiwa msaidizi katika Idara ya Hati za Vitabu. Baadaye alipandishwa cheo akawa mwekaaji msaidizi wa hati za vitabu na katika mwaka 1909 akawa Mkurugenzi na Mkutubi Mkuu wa Jumba la makumbusho la Uingereza Wakati wa sehemu ile ya kwanza ya kushikilia cheo chake kwa muda mrefu, jambo kubwa aliloshughulikia ni hati za Kibiblia na ugunduzi wa mafunjo; baadaye, akawa mwenye daraka la kuwa Mkurugenzi wa safari za uchimbuzi wa vitu vya kale za kwenda Karkemishi na Uru. Baada ya kustaafu alishiriki kukipata kitabu Codex Sinaiticus na kuchapisha mafunjo ya Chester Beatty yaliyosaidia kuthibitisha ukweli wa Maandiko ya Kigiriki.
“Kwa kumalizia, inafaa kutaja maneno ya kitabu chake kinachoitwa The Story of the Bible kama yafuatavyo: ‘Biblia ina historia ya kibinadamu na pia uongozi wa kimungu. Ni historia iliyojawa na upendezi, nayo ni aina ambayo wote wale wanaoithamini Biblia yao wanapaswa kuijua. . . . Ni jambo lenye kutumainisha mwishoni kukuta kwamba matokeo ya ujumla ya ugunduzi wote huo na uchunguzi wote huo ni kutia nguvu uthibitisho wa ukweli wa Maandiko, na usadiki wetu kwamba sisi tunalo Neno la Mungu linaloweza kuthibitishwa kuwa la kweli, likiwa na habari zenye ukamilifu.’”