Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Watu wa Rangi Mbalimbali Waunganishwa Katika Afrika ya Kusini!
IMBALI ni mji wa watu weusi nje kidogo tu ya Pietermaritzburg, Natal, katika Afrika ya Kusini. Wakati yale makundi mawili ya Imbali ya Mashahidi wa Yehova yalipopewa kipande cha ardhi, wazee katika makundi ya weupe na ya machotara katika Pietermaritzburg walikutana pamoja bila kukawia wapange jinsi wangeweza kusaidia ndugu zao weusi wajenge Jumba la Ufalme katika muda mfupi iwezekanavyo. Ingawa kazi ya kujenga iliendelea kwa zaidi ya miezi tisa, kwa kweli ilichukua siku 48 tu za kazi ili kumaliza ujenzi, na sana-sana kazi yenyewe ilifanywa siku za Jumamosi.
Bila shaka ujenzi wa Jumba la Ufalme hilo ulishangaza wakaaji wa Imbali kuona likifanyika jambo ambalo walidhani lisigaliwezekana. Wazia vikundi-vikundi vya weupe, machotara, na Mashahidi Wahindi wakimiminika katika mji kutoka Pietermaritzburg na Durban na kufanya kazi bega kwa bega pamoja na makundi ya Kiafrika! (Linganisha Sefania 3:9.) Wanaume, wanawake, na watoto kadhalika walikuwa wote wakipokezana vifaa na vyombo vya ujenzi, na kula vyakula kwenye meza moja. Umoja kama huo wa jamii za rangi mbalimbali hausikiki katika mji wa Kiafrika, hasa katika wakati huu wa msukosuko! Kwa uhakika, huu ni ushuhuda usioweza kutolewa ubishi kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wenye umoja wanaojali kweli kweli mtu na mwenzake.
Akitoa maelezo juu ya umoja huo, jirani mmoja alisema: “Kuwaona weupe, weusi, machotara, na Wahindi wakifanya kazi kwa upatano sana pamoja kumetushangaza sana. Sisi hatuwi na ushirikiano kama huo katika makanisa yetu.” Kwenye wakfu wa jumba hilo tarehe ya Novemba 10, 1985, meya wa Imbali Bw. Pakkies alihudhuria na akaonyesha mshangao mkubwa kuhusu umoja na kujikaza kwa Mashahidi ili wathubutu kujijengea wenyewe jengo hilo kubwa. Alitoa muhtasari wa jinsi walivyoweza kufanya hivyo kwa kutangaza kwamba, “Upendo tu ndio unaowezesha jambo hilo.” Ni kweli kama nini! Na je, Yesu hakusema: “Kwa upendo huu mlio nao kwa mtu na mwenzake, kila mtu atajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu”?—Yohana 13:35, The Jerusalem Bible.
Mwisho wa mfumo uliopo wa mambo unapokaribia mbio-mbio, Mashahidi wa Yehova katika sehemu zote za Afrika ya Kusini wanauona uhitaji wa kujenga Majumba ya Ufalme katika miji ya weusi na sehemu zao za mashambani upesi iwezekanavyo. Jumba la Ufalme la kwanza katika Soweto liliwekwa wakfu Februari 1985. Mengine mengi yako katika hatua za kujengwa. Kwa kuwa kuna makundi 700 katika shamba la weusi, ni karibu 70 kati ya hayo yaliyo na Majumba ya Ufalme yao wenyewe, kwa hivyo kuna uhitaji mkubwa sana wa kutoshelezwa. Lile jumba la Imbali linasaidia kutosheleza uhitaji huo. Lina nafasi ya watu 400 ambao wanaweza kuketi kwa starehe, bila kusongamana sana wanapotwaa chakula cha kiroho wanachokihitaji ambacho kinapakuliwa humo. Ndiyo, katika vituo vya namna hiyo vya elimu ya Biblia, wapendao uadilifu wanajifunza jinsi wanavyoweza kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo wakapate uzima katika mfumo mpya wa Mungu ambamo wanadamu wa rangi zote wataishi milele wakiwa jamaa moja yenye umoja!