Ni Manufaa Zipi Nyingine Hutiririka Kutoka kwa Mungu?
JE! WEWE unafurahia maua mazuri, harufu nzuri ya waridi, wimbo wa ndege? Je! wewe ulisisimuliwa na tabasamu ya kwanza ya mtoto wako? Je! wewe huthamini harufu nzuri zinazokupa hamu ya chakula? Naye ni nani asiyependezwa sana na upindemvua, machweo yenye fahari nyingi, au nyota katika usiku usio na mawingu? Maandalizi mazuri ajabu ya Mungu hayana mwisho, sivyo?
Hata hivyo kuna taabu nyingi sana. Ijapokuwa uwezo wa dunia wa kuzaa chakula kingi kwa ajili ya wote, mamilioni hawalishwi vya kutosha. Mamilioni zaidi wanapatwa na sumu ya uchafuzi. Na mabilioni leo wanaathiriwa na uhalifu, pupa, ubinafsi, na woga wa yale yatakayoletwa na wakati ujao.
Kwa kuwa Muumba ametoa kwa wingi sana, ni kwa sababu gani kuna ukosefu mwingi sana wa furaha? Sayari hii ni mahali pazuri ajabu, ilifanywa ili sisi tuifurahie. Lakini ulimwengu —wanadamu—umo katika hali yenye kuhuzunisha sana. Kwa wakaaji walio wengi wa dunia matazamio yao hayana tumaini, ni yenye kuogopesha. Kwa sababu gani? Kasoro ilitokea wapi? Je! Mungu alimfanya mwanadamu kisha akamwacha? Je! kuna mwangaza wo wote juu ya hali hii yenye kutatanisha? Je! sisi tuna tumaini lo lote kwa wakati ujao?
Chanzo cha Mwangaza na Tumaini
Karibu miaka 2,000 iliyopita mtoto mvulana wa pekee sana alizaliwa—wa pekee sana kwa sababu mamaye, Mariamu, alikuwa binadamu, na babaye alikuwa Mungu mwenyewe! ‘Haiwezekani!’ je! wengine wanasema hivyo? Hapana, si kwa Mwanzilishi wa utungaji-mimba, yule Mfanyi wa zile aina zote za uhai zilizo ngumu sana kufahamika. Mvulana huyo mdogo alikua akawa “mwanadamu,” mkamilifu “Kristo Yesu.”—Mathayo 1:18-25; 1 Timotheo 2:5.
Huo ulikuwa uzawa wa kufanyiza historia. Kwa kweli, mataifa yaliyo mengi yanakubali hilo kwa kuweka tarehe za matukio ya kihistoria ya kabla ya siku yake kuwa K.K.—kabla ya Kristo. Na hata hivyo miaka yake ya kwanza-kwanza ilitumiwa kwa utulivu akiwa seremala msaidizi nyumbani mwa baba yake mlezi katika Nazareti. Miaka 30 ikapita. Ndipo, kwenye Mto Yordani, Yesu akajitoa mwenyewe kufanya mapenzi ya Mungu na akabatizwa, na roho takatifu ya Yehova Mungu ikamshukia. (Mathayo 3:13-17) Ndipo Yesu akaanza kampeni yenye nguvu ya kuhubiri na kufundisha. Kama ilivyotabiriwa na Isaya, “watu wale waliokaa katika giza [wakaona mwangaza] mkuu.”—Mathayo 4:14-17; Isaya 9:2.
Yesu akawa Mwalimu mwenye kujulikana sana na kuheshimiwa katika mahali pengi wa wakati wote. Hakuna mwalimu mwingine wa kibinadamu ambaye ametumia mavutano yenye nguvu sana juu ya wanadamu au akaandaa mwangaza mwingi sana hivyo wa kiroho na tumaini. Kitabu chake cha mafundisho kilikuwa nini? Ni Biblia, kama ilivyokuwa wakati huo —Maandiko ya Kiebrania. Yesu aliyafanya yawe hai. Unabii mwingi mbalimbali wa kale ulitimizwa katika yeye. (Linganisha Mika 5:2 na Mathayo 2:3-6.) Alithibitisha simulizi la Mwanzo kuhusu asili ya wanadamu. (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:3-6) Yesu aliendeleza, akakuza, na kutangaza kwa mapana na marefu kile kichwa kikuu cha Biblia—kuondolewa malawama kwa Yehova kwa njia ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:23; 6:10) Tena, masimulizi ya maisha na kazi za Yesu Kristo ni sehemu kuu za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya.” Ndiyo, Biblia ni zawadi nzuri ajabu kutoka kwa Mungu, mwangaza wenye kumeta-meta katika ulimwengu wenye giza, wenye huzuni.—Zaburi 119:105.
Ni kwa Nini Wanadamu Wamo Katika Mvurugo?
Je! Biblia inajibu swali hilo? Ndiyo. Inaonyesha kwamba hakikuwa kisa cha Mungu kuachilia wanadamu bali, badala yake, kilikuwa kisa cha wanadamu kumwacha Mungu. Pia, kanuni ya msingi ya uhuru wa kuchagua ilihusika. Binadamu hawakuumbwa wakiwa mashine-watu, wakiwa wameingizwa miongozo ya kufuata bila hiari. Sisi tunaweza kuchagua kutii au kutokutii.
Mungu alipowaumba wale binadamu wawili wa kwanza katika Paradiso nzuri sana ya Edeni, ni lazima wawe walikuwa wenye furaha na bila hangaikio kama nini! Hakuna magonjwa, hakuna woga, hakuna wasiwasi. Walikuwapo ndege na wanyama wenye kupendeza, na chakula kitamu kilikuwako kwa wingi. (Mwanzo 1:26; 2:7-9) Hata hivyo, baada ya wakati fulani, adui asiyeonekana akaja kwenye mandhari hiyo. Kiumbe wa kiroho mwenye nguvu akawa mwenye kujitakia makuu, akitamani kuwa kiongozi juu ya jamaa ya kibinadamu ya wakati ujao. Kwa kusema ule uwongo wa kwanza, alimtongoza Hawa, naye Adamu alisadikishwa kutoitii amri ya Mungu iliyosema wasile lile tunda lililokatazwa. (Mwanzo 3:1-7) Kama ilivyo kwa watu wengi leo, binadamu wawili wa kwanza walifikiri wangeweza ‘kufanya kivyao wenyewe.’ Lakini kwa kufanya hivyo kwa kweli walijiweka wenyewe chini ya uongozi wa Shetani, yule mungu wa mfumo mbovu wa mambo uliopo.—2 Wakorintho 4:4, NW.
Hilo lilizusha suala kubwa la maana sana: Je! mwanadamu angeweza kujitawala mwenyewe kwa kufaulu bila Mungu? Wakati mwingi ungetakwa ili kujibu suala hilo vya kutosha. Kwa sasa, Adamu na Hawa walilazimika kulipa adhabu ambayo Mungu alikuwa amewaandikia —kifo. Na kwa kuwa walikuwa wamekuwa watenda dhambi wasiokamilika, wala wao wala wazao wao hawakuwa na taraja la uzima wa milele bila kumtegemea Mungu.—Warumi 5:12; 1 Wakorintho 15:21, 22.
Wakati Ujao Wenye Utukufu
Tangu siku za Adamu vizazi vingi vimekuja vikaenda. Na katika tamasha ya mambo ya wanadamu yenye kubadilika-badilika, namna nyingi za serikali za kibinadamu zimejaribiwa —otokrasi, demokrasi, soshalisti, ukomunisti, na nyinginezo. Lakini zote zimeshindwa. Magumu ya kisiasa, kijamii, na ya kimataifa yanaongezeka sana. Ndivyo na silaha zenye kutisha sana za kuangamiza kwa wingi sana ambazo zinatisha kuleta kujiangamiza kwa ulimwengu. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, wanasiasa wa Magharibi waliahidi kwamba ushindi ungeleta uhuru wa bila umaskini na woga. Lakini yote mawili yanaongezeka.
Utatuzi ni nini? Tatizo kubwa lahitaji utatuzi mkubwa—hakuna jingine ila kusafisha kabisa tufe lote na kuuleta ulimwengu mpya. Ni nani awezaye kutimiza hilo? Bila shaka si Umoja wa Mataifa au muungano mwinginewo wote wa mamlaka za kisiasa ambazo mara nyingi huvunja mapatano ya amani—hata kabla wino wa sahihi zao haujakauka! Wao ni vibaraka hoi waliokabwa katika uwezo wa Kishetani. (1 Yohana 5:19) Ni Yehova tu, Mwenye Nguvu Zote, anayeweza kumwondoa Shetani na mashetani wake, akomeshe ulimwengu mpotovu uliopo, na kuleta mwingine mpya wenye utukufu chini ya Ufalme wa kimbingu, Mwanaye Yesu Kristo, akiwa Mfalme wa wafalme.—Mathayo 6:9, 10; Danieli 2:44; Ufunuo 20:1-3.
Ufalme huu utatimiza nini? Ni nani atakayeokoka uharibifu wenye kusafisha tufe lote, au Har–Magedoni? Uhakika wenye kupendeza ambao watu wanaozidi kuongezeka wanakuja kuutambua ni kwamba serikali hii ya kimbingu tayari inatenda kazi na kutayarisha watu waje kuokoka Har–Magedoni! (Ufunuo 16:14-16) Ni lazima wao wawe watu wa namna gani? Yesu Kristo alisema: “Wenye furaha ni wale wapole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5, NW) Hapo yeye alithibitisha unabii huu wa kale: “[Kabla] haijawajilia siku ya hasira ya [Yehova]. Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].”—Sefania 2:2, 3.
Si kwamba tu wanyenyekevu wataokoka Har–Magedoni bali, kwa kubaki waaminifu kwa Mungu, pia wataurithi uzima wa milele. Jinsi gani? Kama ilivyotangulia kutajwa, jamaa kubwa ya wazao wa Adamu ilipoteza taraja la uzima wa milele kupitia dhambi yake ya kutokutii. Kifo kikaifikia jamii yote kupitia Adamu. Kwa kuwa yeye alikuwa mwanamume mkamilifu, mwanamume mwingine mkamilifu alihitajiwa ili kukomboa au kununua tena, alichopoteza Adamu. Yesu Kristo alijaza uhitaji huo na akautoa uhai wake “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
Mwandalio huo wa ukombozi ndiyo zawadi iliyo kubwa zaidi ya zote ya Mungu kwa wanadamu. Itatumika si kwa wale tu watakaookoka na kuingia katika ulimwengu mpya bali pia kwa wale watakaorudi kutoka kwa wafu. Je! hilo lasikika kuwa jambo la kustaajabisha mno? Yesu alisema: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.” Ni jambo lenye kusisimua kama nini! Ni jambo la kufurahisha kama nini kwa waokokaji wa Har–Magedoni, watakaoweza kuwakaribisha wapendwa wao kutoka kwa wafu! —Yohana 5:28, 29.
Ni taraja na tumaini tukufu kama nini! Na yote hayo yameandaliwa na Muumba mwenye upendo, Yehova, kupitia Mwanaye mpendwa, Yesu. Ijapokuwa leo matazamio yamekosa sana tumaini na ni yenye kuogofya, wakati ujao umejaa mwangaza na tumaini kwa wale wanaojifunza Biblia na kutenda kulingana na ujumbe wayo wenye kutia moyo. Sisi tunaishi katika nyakati zenye kusisimua. Ufalme wa Mungu u karibu! (Mathayo 24:33, 34) Msifuni Yehova, Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu”!—Yakobo 1:17, NW.
Unapotafakari juu ya njia nyingi ambazo katika hizo tunanufaika na maandalio na makusudi ya Mungu, huenda ukahisi sana kuwa na shukrani na ukatamani kuonyesha shukrani hizo katika njia fulani. Ikiwa ndipo tu unaanza kufahamu na kukubali tumaini halisi kwa wakati ujao, huenda ukahisi uhitaji wa kuchunguza zaidi. Sisi tunakutia moyo ufanye ilo hilo. Endelea kujifunza Neno la Mungu pamoja na vichapo kama hiki vinavyoweza kukusaidia kuzidisha maarifa yako na uthamini kwa makusudi matukufu ya Mungu.
Wale ambao tayari wana usadiki ulio wazi kwamba Ufalme wa Mungu ndio utatuzi pekee kwa taabu za wanadamu huenda wakahisi kama mtunga zaburi aliyeongoza kwa roho aliyesema hivi: “Nimrudishie [Yehova] nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?” (Zaburi 116:12) Watu mmoja mmoja kama hao wataona kwamba kuwaambia wengine juu ya yale ambayo Mungu ametufanyia sisi na wakati ujao mtukufu anaowatolea wale wanaompenda na kumtumikia kunaleta uradhi mwingi na furaha halisi. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kama alivyosema Yesu: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
YESU KRISTO—
◆ Alitimiza unabii mwingi wa kale, kwa mfano, Mika 5:2; Mathayo 2:5, 6
◆ Alithibitisha simulizi la Mwanzo juu ya asili ya mwanadamu—Mathayo 19:3-6
◆ Alikuza na kutangaza kichwa kikuu cha Biblia, kuondolewa malawama kwa Yehova kupitia Ufalme—Mathayo 24:14; Luka 8:1
◆ Alilipa kilichopotezwa na Adamu, uhai mkamilifu wa kibinadamu, hivyo akawezesha wale wanaozoea imani katika Yeye kupata uzima wa milele—Yohana 3:16
[Picha katika ukurasa wa 7]
‘Utamrudishia Yehova Nini kwa Yote Aliyokutendea?’