Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
‘Ripoti Njema Kutoka Mabara ya Mbali’
◻ KATIKA Greenland yenye barafu wahubiri fulani wakiwa katika ziara ya kuhubiri walikutana na Mnorowei kijana aliyekubali kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Hata hivyo, yeye hakuonyesha upendezi mwingi. Walipofanya ziara ile nyingine katika mahali hapa pa mbali, yeye aliwaambia kwamba alikuwa amesoma kitabu kile mara kadhaa na alitaka vitabu zaidi. Aliachiwa vitabu na broshua kadhaa. Alihuzunika kwamba kwa muda wa mwaka mwingine mmoja wahubiri hao hawangeweza kurudi lakini akajipatia anwani ya Mashahidi hao. Mwezi mmoja baadaye, wao walishangaa alipobisha hodi mlangoni pao. Alisimulia kwamba alikuwa ameanguka akipita katika barafu kwa skuta yake ya thelujini akiwa njiani kwenda kwenye mashua yake, halafu ikamchukua muda wa saa sita akisafiri majini ili awafikie Mashahidi hao. Alitaka kujipatia fasihi zaidi na kuzungumza juu ya ukweli. Alihudhuria mkutano jioni hiyo na akafanya mipango ya kuhudhuria mara moja kwa mwezi. Alikuja kwa ajili ya ziara ya mwangalizi wa mzunguko na kutiwa moyo sana. Amejiondoa kwenye kanisa na sasa anahubiri habari njema katika eneo lake. Wakati barafu ya kipupwe imzuiapo asifike mikutanoni kwa mashua, yeye hutumia helikopta, ikimgharimu dola 150 kwa safari moja.
Ni wangapi kati yetu hulazimika kujitahidi kadiri hiyo ili tusonge mbele katika huduma yetu?
◻ Watu wengi wanaziitikia habari njema katika Madagascar. Kukiwa na wahubiri wa Ufalme wanaozidi kidogo tu 3,200, watu 16,205 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Akina ndugu wanafanya jitihada kubwa za kufikia watu wote katika kisiwa hicho.
Kwa kielelezo, 17 kati ya wale wahubiri 30 wa Kundi ya Isaonjo waliamua kutoa ushuhuda katika eneo la umbali wa kilometa 50 hivi. Waliondoka kwenye kijiji chao nusu-saa baada ya saa sita usiku. Kwa muda wa saa mbili walitembea katika vijia vilivyoinama sana na kupitia mabwawa yenye utopetope. Halafu wakauingia msitu wa kitropiki saa 8:30 usiku. Kwa sababu giza lilifunika msitu ule, ndugu fulani walianguka kwa kujikwaa kwenye majabali. Baadhi yao walijikwaa wakaingia ndani ya vidimbwi vya maji katika miamba yenye mashimo-mashimo. Msitu ulikuwa na ruba, na wadudu wengi waliwauma. Wengi kati ya akina dada waliteseka kwa njia hii. Matope yaliwafika gotini nyakati fulani. Wahubiri wote 17 waliumia kwa njia moja au nyingine, lakini mwishowe wakaibuka kutoka msitu huo saa 12:30 asubuhi!
Utumishi wa shambani ulianza saa 12:45 asubuhi. Wengi kati ya watu wa huko walipokea wahubiri hao kwa fadhili. Mmoja asiyewapokea hapo kwanza alikuwa mke wa kiongozi wa kidini Mprotestanti. Mwanamke huyo alisema hivi: “Mimi nina dini yangu mwenyewe; hiyo yanitosha. Mimi najua yote ambayo Biblia yasema.” Mara tu mhubiri alipotoa gazeti Mnara wa Mlinzi, mwanamke huyo alilikataa kwa kujigamba, akisema: “Tayari mimi nina vitu vingine vingi vya kusoma.” Lakini akaanza kuuliza maswali: “Nyie ni akina nani, na mwatoka wapi, na nani kawatuma?” Baada ya wao kujibu kwa upole na kusimulia kifupi juu ya jitihada yote waliyokuwa wamefanya ili wafikie kijiji chake, bibi huyo alikubali Mnara wa Mlinzi, akisema: “Nitalinunua. Nani ajuaye kama nyinyi mmetumwa na Mungu?”
Saa 7:30 alasiri, hao 17 waliondoka eneo hilo kwenda nyumbani, wakimaliza safari ile kwa muda ulio chini ya saa nne kwa sababu kulikuwa kungali mchana. Walikuwa wamechoka lakini wakiwa salama, na nyuso zao ziling’aa shangwe. Walisema: “Ilikuwa siku isiyosahaulika kwa sisi watu 17 kutoka Kundi la Isaonjo.”
Kwa uhakika, roho ya Yehova inasukuma watumishi wake waliojiweka wakfu ili wazihubiri habari njema za Ufalme “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia,” na wengi wanaitikia jitihada nzuri za Mashahidi.—Matendo 1:8, NW.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Bandari ya Umanak, Greenland