Mkumbuke Muumba Mtukufu Wako Katika Ujana Wako
“VIJANA Wasioridhika: Uhakika wa Maisha ya Kimataifa.” Ndivyo kilivyosema kichwa kikuu cha makala moja katika The Star ya Johannesburg, Afrika Kusini. Maelezo ya utangulizi wa makala hiyo yalisomeka hivi: “Huku idadi kubwa sana za vijana zikikabiliana na fursa chache ambazo zinapunguzwa hata zaidi na kuzorota kwa uchumi ulimwenguni pote, kutoridhika kwa vijana katika majiji yenye kupanuka sana kumekuwa uhakika wenye kuonekana wazi wa maisha ya kimataifa. Katika ghasia zilizotokea katika Miami, katika San Salvador, katika Managua, katika Teheran na katika Cape Town mlikuwamo jambo moja la kawaida—katika kila kisa waliokuwa wa kwanza kuua na kuuawa walikuwa vijana.”
Hiyo ilichapishwa yapata miaka kumi iliyopita, na hali zimekuwa mbaya zaidi tangu wakati huo. Kwa nini kuna ukosefu huo wa kuridhika miongoni mwa vijana ulimwenguni pote? Ni wazi kabisa kwamba ukosefu wa imara wa mfumo huu wa mambo husababisha jambo hilo. Ukosefu wa kazi ya kuajiriwa umeongezeka ajabu. Na huku maisha ya familia yakiendelea kuzorota kwa kasi, kuna usalama gani kwa vijana? Si ajabu kwamba baadhi yao huushambulia ulimwengu wasioweza kuudhibiti. Je! hii si kwa sababu wao hawana tumaini la kutilia nanga maisha zao?
Mtu angetarajia dini za ulimwengu zijaze tumaini hilo katika watu. Hata hivyo, kijana mmoja aliandika hivi: “Mimi nimevurugika sana. . . . Nina marafiki wengi, wa dini nyingi tofauti-tofauti, nao wako kama mimi kabisa. Mimi nimevurugika sana hivi kwamba sijui tena jambo la kuamini. Tafadhali, mngeweza kunipa ushauri fulani?” Wewe ungempa ushauri gani kijana wa jinsi hiyo?
Vijana ambao hushikamana karibu-karibu na Neno la Mungu na kundi la kweli la Kikristo huepushwa na mvurugo na umivu hilo la kichwa. Ijapokuwa vijana walio wengi hawana tumaini hakika kwa wakati ujao, vijana Wakristo hutumaini katika Yehova Mungu na Neno lake la ukweli lililo hakika. Kwa hiyo, wao wana tazamio la kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo wakiwa na taraja la kupata uhai wa milele. Baada ya hapo, katika dunia yenye kusafishwa sana isiwe na ukosefu wa haki na uovu, wao watafanyiza sehemu ya msingi wa “dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13, NW; Yohana 17:3) Ili wapate utimizo wa matazamio hayo matukufu, vijana hushauriwa ‘wakumbuke Muumba Mtukufu wao.’ (Mhubiri 12:1) Na ushauri mzuri kabisa ambao ungeweza kutolewa ni kwamba wao wawe sehemu yenye umaana kamili ya kundi la Kikristo na kubaki humo. Kwa nini?
Walio wengi wa nyinyi vijana katika kundi la Kikristo mna wazazi wanaoamini ambao wawapenda na kuwajali. Kila kundi lina wazee waliowekwa, ambao hupendeza sana na halinjema yenu ya kiroho. Msaada na utunzi huo haupasi kupuuzwa. Ukweli kutokana na Neno la Mungu, pamoja na mwelekezo wa kitheokrasi, utawapa nyinyi usalama, uhuru wa kutokuwa na mvurugiko wa fikira, na tumaini hakika kwa wakati ujao. Yote haya yatawasaidia nyinyi ‘mshike imani na dhamiri njema’ na kujishikiza sana kwenye tumaini lililo kama nanga inayozuia chombo kuvunjika-vunjika katika bahari zenye dhoruba.—1 Timotheo 1:18, 19; linganisha Waebrania 6:19.
Epuka Kabisa Vishawishi vya Kilimwengu
Zijapokuwako baraka nyingi za kiroho ambazo nyinyi wachanga mwaweza kuzionea shangwe katika kundi la Kikristo, elekeo la baadhi ni kufuatia njia za ulimwengu. Ni kana kwamba wanahisi wanakosa kitu fulani cha ustahiki ambacho chaweza kupatikana katika ulimwengu ulio nje ya kundi la Kikristo. Lakini je! kwa kweli ulimwengu una chochote cha ustahiki cha kutoa?
Baada ya kutumia miaka zaidi ya 40 katika huduma ya wakati wote, mmoja wa watumishi wa Mungu aeleza mambo hivi: “Sehemu moja tu ya maisha yangu niliyo na majuto nayo ni ile sehemu niliyoishi kabla zijaingia katika ukweli. Wakati huo nilikuwa sehemu ya ulimwengu. Niliishi kwa ajili ya ulimwengu tu. Nilipofika umri wa miaka 18 na kutazama nyuma kwenye maisha yangu yaliyopita, niling’amua kwamba yalikuwa matupu. Hakukuwa na shabaha yoyote, kusudi lolote, kwenye maisha yangu. Anasa za kilimwengu nilizofikiri nilizionea shangwe kwa kweli zilileta mvurugiko wa fikira na majonzi tu. Nilianza kuutafuta ukweli. Niliupata na mwaka mmoja baadaye nikaanza kujitia katika utumishi wa wakati wote. Sikuwa na pesa zozote, ila ujuzi wa mwaka mmoja katika ukweli na imani ya kwamba Yehova angenitegemeza. Sasa nitazamapo nyuma kwenye maisha yangu yaliyopita, nikiwa nimetumia theluthi mbili za hayo katika utumishi wa wakati wote, nafurahi kabisa kabisa. Sitataka kamwe kubadilishana nilichopata kutokana na kutumikia Yehova kwa kitu chochote kitolewacho na ulimwengu.” Kwa kweli, huo ni mwangwi wa hisia za maelfu ya Mashahidi wa Yehova.
Kwa hiyo kwa nini utamani sana vitu ambavyo Wakristo wengine wameacha nyuma? Kwa nini uwe na hamu kubwa ya vitu vya ulimwengu unaoelekea kwenye uharibifu? (1 Yohana 2:15-17) Wewe ukiwa kijana, labda wahisi kwamba kutumikia Yehova kuna vizuizi vingi mno na kutasababisha upoteze shangwe ambayo ulimwengu hutoa. Lakini je! ni jambo la hekima kuwaona wazazi wako na wazee kuwa wazuilivu mno watakapo kukusaidia umpendeze Yehova na kupata uhai wa milele?
Mama anayetuma mtoto wake kwenye duka la hapo kwao akimkumbusha asimame na kutazama pande zote kabla ya kuvuka barabara, je! wewe ungemfikiria kuwa mzuilivu kupita kiasi? Badala ya hivyo, je! yeye hajaribu kwa upendo kumlinda mtoto wake? Namna gani kama mtoto angepuuza onyo hilo agongwe na gari na kuuawa? Je! bado wewe ungehisi kwamba mama huyo alikuwa amekuwa mzuilivu mno? Ungeweza kufikiri kwamba angalipaswa kuchukua hatua zaidi za tahadhari ili kulinda uhai wa mtoto wake! Vivyo hivyo, vikumbusha kutoka Neno la Mungu na tengenezo lake hutolewa kwa upendo, si kuwa vizuizi bali kwa ajili ya ulinzi wetu.
Kukua ukiwa katika makao ya Kikristo hakutoshi kukufanya uweze kuvumilia mikazo ya ulimwengu huu. Wahitaji pia kusadikishwa kibinafsi juu ya ukweli wa Neno la Mungu. Usadikisho huo wa kibinafsi na upendo kwa Muumba hufanyiza msingi wa kuweka maisha yako wakfu kwa Mungu. Usadikisho huo wa kibinafsi wahitajiwa kabisa pia ili wewe uweze kutetea imani yako mbele ya wengine. (1 Petro 3:15) Kuongozwa na Neno la Mungu ndio msingi wa maisha yenye mafanikio. (Yoshua 1:8; Zaburi 119:9) Lakini ili upate mafanikio katika maisha, wahitaji pia mazoezi mema.
Kutoa Mazoezi Hususa
Kwa uhakika, nyinyi wazazi Wakristo mngefurahi sana kuona watoto wenu wakichukua msimamo imara kwa ajili ya ukweli na kubaki wakiwa wameungamana nanyi katika ibada ya kweli. Hasa ni daraka la baba kulea watoto “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Lakini je! mwaweza kugundua maeneo ambamo nyinyi mwahitaji kufanya maendeleo katika kuwazoeza? Je! mnatumia wakati wa kutosha mkiwa pamoja na watoto wenu? Je! nyinyi hufanya mambo mkiwa familia? Na je! nyinyi huonea shangwe tafrija yenye mafaa mkiwa pamoja?
Msisahau kwamba kuweka kielelezo kifaacho kuna matokeo yenye nguvu juu ya watoto wenu. Ikiwa nyinyi mwataka wao wachukue ukweli kwa uzito, basi nyinyi mwapaswa kuwa na maoni hayo ya kuuona jinsi iyo hiyo. (3 Yohana 2-4) Na ikiwa mwataka wao wasitawishe staha ya kina kirefu kwa tengenezo la Yehova na wazee, basi nyinyi wenyewe mwapaswa sikuzote kuwa na maoni yenye afya.
Ingawa kuzoeza watoto ni wajibu wa wazazi hasa, wazee pia wana daraka fulani kuelekea wachanga katika kundi. Katika kutunza kundi la kondoo za Mungu, waangalizi wahitaji pia kuchunga wana-kondoo. (1 Petro 5:1-3) Lo, ni kielelezo kizuri kama nini ambacho Yehova ameweka katika kuwatunza kwa wororo hata hao walio wadogo! (Isaya 40:11) Kwa kuitikia kielelezo chake, wachungaji wa chini wa Kikristo watataka pia kuonyesha upendezi mchangamfu na wenye upendo katika vijana na kuwafanya wahisi wakiwa sehemu ya kundi. Vijana fulani wameeleza tamaa yao ya kwamba wazee waongee nao mara nyingi zaidi na kuwasaidia katika huduma ya shambani.
Kuzoeza kijana humaanisha mengi zaidi ya kumpa maarifa ya kichwani juu ya Maandiko. Kutoka moyoni mwake, ni lazima achukie yale ambayo Mungu huchukia na apende yale ambayo Mungu hupenda. (Amosi 5:14, 15) Ikiwa atamkumbuka Muumba wake katika ujana, yeye ahitaji kutiwa nidhamu Kimaandiko katika kutembea katika njia ya Yehova ya uadilifu. (Mithali 22:6; 2 Timotheo 3:16) Wazazi hawapaswi kusita-sita kutoa nidhamu inayohitajiwa. Wazazi fulani watakao kuendeleza urafiki wa mtoto wao hata igharimu nini huwa na mbetuko wa kujifanya hawaoni kosa, wakipunguza uzito walo. Wao huongozwa na uendekevu wa ulimwengu. Lakini mzazi mwenye upendo ndiye hutega sikio kwa uangalifu kwenye ripoti za kwamba mtoto wake amekuwa akijiendesha vibaya na ndiye hutoa nidhamu ifaayo kwa kadiri ambavyo yahitajiwa. (Mithali 13:24) Kwa kweli, ni mzazi gani Mkristo atakaye kuendeleza urafiki ambao msingi wao ni uendekevu lakini apoteze mtoto wake kwa ukosefu wa nidhamu ifaayo?—Mithali 22:15.
Uwe na Kusudi Maishani
Yehova Mungu alitufanya ili tupate shangwe na uradhi ulio mkubwa zaidi kutokana na kumtumikia. Fikiria shamba kubwa sana ambalo nyinyi vijana mwaweza kulima. Karibu nusu ya wakaaji wa ulimwengu ni wenye umri wa miaka 20 na wachanga zaidi ya hapo. Vijana hawa wanatatanika katika bahari ya ubinadamu. Ingawa hawana tumaini, nyinyi vijana Wakristo mna tumaini hakika na kitu chenye ustahiki cha kushirikiana nao. Kupitia mwenendo wenu mzuri wa Kikristo na bidii yenu kwa utumishi wa Yehova, huenda mkawavutia wengi wao kwenye ukweli. Hivyo mwaweza kuwasaidia waingie katika njia ya uhai.
Ni mradi gani wenye ustahiki zaidi ambao wewe ungeweza kuwa nao kuliko ule wa kutoa maisha yako kwenye utumishi wa Yehova Mungu? Je! umefikiria kuanza ile kazi ya kuokoa uhai ya kuhubiri wakati wote? Labda waweza kushiriki kueneza habari njema ukiwa painia, au waweza kutumikia kwenye moja ya ofisi za matawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ambako fasihi za Biblia hutokezwa. Hata ikiwa huwezi kufanya hivyo, je! haikupasi kufanya ibada ya Yehova iwe ndilo jambo la kukaziwa fikira zaidi katika maisha yako, hivyo ukikumbuka Muumba Mtukufu wako? Una kazi yenye ustahiki. Kwa hiyo, mpaka mwisho wa mfumo huu wa mambo piga moyo konde uwe na ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58, NW.
Kwa hiyo jikazeni kusonga mbele nyinyi vijana Wakristo. Mkumbukeni sasa Muumba Mtukufu wenu. Ndiyo, Yehova atawalinda wakati huo na kuwabariki kwa wakati ujao mtukufu usio na mwisho.